Habari za Punde

Dk Shein azindua Tawi la SUZA, Pemba na kusema ni hatua kubwa katika maendeleo ya elimu nchini

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Pemba                                                                              25.8.2015
RAIS wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein leo amelizindua Tawi la Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA), Kampasi ya Benjamin William Mkapa, Pemba  na kueleza kuwa wananchi wa Pemba watarajie kupata fursa ya kuchangia maendeleo yao na ya nchi kwa jumla kwani  uzinduzi huo ni hatua kubwa katika maendeleo ya elimu hapa nchini.

Katika hotuba yake aliyoitoa mara baada ya uzinduzi huo hapo katika viwanja vya Tawi hilo, Dk. Shein alisema kuwa Chuo Kikuu ni Taasisi muhimu na taasisi kubwa katika nchi yoyote  duniani kutokana na majukumu yake ya kuongeza kasi ya maendeleo katika jamii.

Dk. Shein alisema kuwa kuna kila sababu ya kusherehekea uzinduzi huo kwani vijana wengi kutoka Pemba walikuwa wakifuata elimu ya juu katika vyuo vilivyoko Unguja, Tanzania Bara na nchi za nje.

"Leo siku ya sikukuu kwa kufungua ukurasa mpya wa  maendeleo. Ni dhahiri kuwa tuna haki na wajibu wa kusherehekea kwamba hatimae tumefikia hatua ya kuipata fursa ya masomo ya elimu ya juu katika Chuo Kikuu cha Taifa hapa hapa Pemba",alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa mbali ya kuwepo kwa mafunzo ya kitaaluma ya ngazi mbali mbali na fani tafauti, chuo kikuu kina wajibu muhimu wa kufanya tafiti zenye lengo la kutafuta ufumbuzi wa changamoto mbali mbali zinazoikabili jamii sambamba na kutoa ushauri.

Alisema kuwa  hatua hiyo ni lazima iongeze ari ya wazazi, walezi na vijana katika skuli za Zanzibar sambamba na kuongeza jitihada katika masomo ili kupata sifa za kujiunga na chuo hicho.


Alieleza kuwa kuwepo kwa Tawi hilo la SUZA hapa Pemba ni sawa na mlango wa fursa pekee ambao vijana na wananchi wengi kwa jumla wautumie huku akisisitiza kuwa kuongeza idadi ya Kampasi za Chuo ni hatua ya maendeleo ambapo sasa SUZA itakuwa na jumla ya Kamsasi 4 ambazo ni Kampasi ya Tunguu, Vuga, Nkruma na Kampasi ya Benjamin Willium Mkapa.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa viongozi wa Chuo Kikuu cha SUZA kwa kazi nzuri katika kutekeleza majukumu yao na kuanzisha kozi na mafunzo mbali mbali kwa kuzingatia mahitaji ya soko la ajira na mipango ya maendeleo.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alisema kuwa ni jambo la faraja zaidi kuona kuwa asilimia kubwa ya wanafunzi wanaojiunga na chuo hicho ni wanawake kwani ni hatua kubwa ya mafanikio na utekelezaji wa lengo la Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuona kuwa watoto wa kike wanapata fursa ya juu.

Dk. Shein alitoa wito kwa jumuiya ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kuyaendeleza mafanikio yote yaliofikiwa na chuo hicho tangu kuasisiwa kwake miaka 14 iliyopita na kuutaka uongozi wa chuo hicho kuendeleza urafiki na mashirikiano na wananchi wa Mchangamdogo pamoja na vijiji vya jirani ili wanufaike na fursa mbali mbali zitokanazo na chuo hicho.

Sambamba na hayo, alisisitiza haja kwa chuo kuongeza jitihada katika kufanya tafiti mbali mbali za maendeleo ya jamii na wanachi kwa akushirikiana na Tume ya Sayansi na Teknolojia Tanzania (COSTECH), taasisi mbali mbalizinazofanya tafiti pamoja na kuimarisha mahusiano na vyuo vyengine vya ndani na nje ya Tanzania.

Dk. Shein katika hotuba yake hiyo alisisitiza zana muhimu ya mabadiliko katika maendeleo huku akiziangiza Wizara ya Elimu na Mfyunzo ya Amali pamoja na uongozi wa chuo hicho kukaa pamoja ili kujadili suala la Skuli ya Sekondari ya Mchangamdogo ili iwe skuli ya SUZA kwa Pemba na kuwa na wanafunzi wenye vipaji na hatimae kujiunga na vyuo mbali mbali ndani na nje ya nchi.

Pia, aliiagiza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Wizara ya Kilimo na Maliasili, Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati kukaa pamoja ili kuangalia uwezekano wa kupatikana nafasi katika eneo la Tawi hilo kwa kukaa na wananchi wa eneo hilo kuzzungumzia suala hilo.

Nae, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali  Mhe. Ali Juma Shamuhuna alitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa kutimiza ahadi yake kwa vitendo aliyoitoa ya kuanzisha Tawi la Chuo Kikuu cha SUZA katika Kampasi hiyo.

Nae, Makamu Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Zanzibar SUZA, Profesa Idrisa Ahmada Rai alisema kuwa uchambuzi wa Kitaalamu unaonesha wazi kwamba Dk. Shein alipoingia madarakani kuongoza Serikali ya Awamu ya Saba alikuwa na dhamira ya kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar kwa kupitia mambo mawili makubwa yakiwemo kudumisha umoja na amani pamoja na kuwataka Wazanzibari wabadilike.

Profesa Rai alisema kuwa Kampasi hiyo itaanza kwa kuendeleza masomo ya Ualimu katika ngazi ya Diploma ya Msingi yanayotolewa Chuoni hapo, na kuanzia mwaka huu wa Taaluma, masomo ya Diploma ya Sayansi na Elimu ya miaka miwili na miaka mitatu yatasomeshwa chuoni hapo.

Aidha, Tawi hilo linaanza kutoa mafunzo ya utaalamu ya muda mfupi kwa taaluma mbali mbali kama vile masomo ya matumizi ya teknolojia ya Tehama, mafunzo ya ujasiriamali, mafunzo ya lugha za kigeni na mafunzo mengineyo.

Profesa Rais alieleza kuwa lengo la SUZA, kwa kuzingatia dhamira ya Serikali ya kuanzishwa kwa Chuo cha Ualimu cha Benjamin Willium Mkapa, ni kutanua mafunzo ya ualimu katika Kampasi hiyo na hatua zitakazofuata ni kuhamasisha masomo yote ya Diploma ya Ualimu yanayotolewa Unguja kwenye Kampasi hiyo ndani ya miaka michache ijayo lakini pia, kuanza kutoa masomo katika ngazi ya Shahada ya kwanza hadi PhD.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu Khadija Bakari alisema kuwa kuwepo kwa Kampasi ya SUZA Pemba, kutaongeza wanafunzi wanaojiunga na chuo katoka kisiwani humo na kupunguza usumbufu wa kufuata mafunzo vyuo vya mbali huku akisisitiza kuwa Wizara ya Elimu na Maafaunzo ya Amali itaendelea kuunga mkono juhudi za SUZA na kuisaidia kufikia malengo iliyojiwekea.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

1 comment:

  1. mwaka huu ndio mnakumbuka vitu vyote hivi kwani miaka yote hiyo mlikuwa hamuoni its late ,tutafanya wenyewe fungeni virago vyenu vyenu muondoke kwani hatuna shida nayo.

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.