HOTUBA YA RAIS WA
ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI, MHE. AL-HAJJ DK. ALI MOHAMED
SHEIN, KATIKA
BARAZA LA IDD- EL-HAJJ:
24 SEPTEMBA, 2015
SAWA NA MWEZI 10
MFUNGUO TATU, 1436 HIJRIA
BISMILLAH RAHMAN
RAHIM
Naanza kwa kushuhudia kuwa hapana Mola
anayestahiki kuabudiwa kwa haki na viumbe vyote isipokuwa Mwenyezi Mungu
Mtukufu Subhana Wataala. Yeye ndiye
Muumba wa Dunia na Akhera na kwake Yeye ndiyo marejeo ya viumbe vyote. Tunakiri kwa kauli na kuitakidi kwa moyo kuwa
Mtume Muhammad (S.A.W) ni Mtume wake wa haki na kigezo chema cha uchamungu kwa
waumini sote.
Rehema na amani ya Mwenyezi Mungu zimshukie
Mtukufu wa daraja na mbora wa viumbe; Sayyidna Muhammad (S.A.W), Aali na Sahaba
zake pamoja na waumini wote waliofuata njia yake ya uongofu hadi siku ya
kiama. Tumuombe Mola wetu (SW) atujaalie
na sisi tulio hai, ndugu, jamaa na wale wote waliokwishatangulia mbele ya haki
tuwe miongoni mwao. Atupe ubainifu wa kuyafanya
mambo ya kheri na tuyaepuke mambo ya
shari na maovu, ili tuweze kufanikiwa hapa Duniani na huko Akhera
tuendako. Amin!
Mheshimiwa Sheikh
Khamis Haji Khamis;
Kadhi Mkuu wa
Zanzibar.
Mheshimiwa Maalim
Seif Sharif Hamad;
Makamu wa Kwanza wa
Rais,
Mheshimiwa Balozi
Seif Ali Iddi;
Makamu wa Pili wa
Rais,
Mheshimiwa Dk. Amani
Abeid Karume,
Rais Mstaafu wa
Zanzibar;
Mheshimiwa Pandu
Ameir Kificho;
Spika wa Baraza la
Wawakilishi,
Mheshimiwa Omar
Othman Makungu;
Jaji Mkuu wa
Zanzibar,
Waheshimiwa
Mawaziri,
Waheshimiwa
Mabalozi,
Wageni Waalikwa,
Ndugu Wananchi,
Mabibi na Mabwana,
Assalamu
Aleikum Warahmatullahi Wabarakatuh
IDDI
MUBARAK
Ndugu Wananchi,
Nimeanza hotuba yangu kwa kumtukuza Mola
wetu (SW) na kukiri kuwa Bwana Mtume Muhammad (S.A.W) ni Mtume wa haki wa
Mwenyezi Mungu ambaye ni wajibu wetu kumsalia, kuyazingatia na kuyafuata
mafundisho yake ili tuweze kufanikiwa katika kuyatekeleza maamrisho ya Mwenyezi
Mungu na tujiepushe na yale yote tunayokatazwa kuyafanya.
Kupitia mafundisho ya Mtume (S.A.W) kutoka
kwa Mwenyezi Mungu, tumetakiwa tuitekeleze ibada ya Hijja kwa kila mwenye uwezo
katika nyumba tukufu iliyopo Makka huko Saud Arabia. Mwenyezi Mungu katika aya ya 97 ya Surat Aali
Imran anatufahamisha uzito na umuhimu wa kuitekeleza ibada ya Hijja kwa kusema:
“Na kwa ajili ya Mwenyezi Mungu imewawajibikia
watu wafanye Hijja katika nyumba hiyo, kwa yule awezaye kwenda huko. Na atakayekufuru (atakayekanusha) basi
Mwenyezi Mungu si muhitaji kuwahitaji walimwengu”.
Ndugu
Wananchi,
Leo tunaungana katika furaha ya sikukuu ya
Idd el Hajj na waislamu wenzetu kwa maelfu kutoka mataifa mbali mbali, wa rangi
na hadhi mbali mbali walioitikia wito wa Mola wetu kwenda kuitekeleza Ibada ya
Hijja katika mji Mtukufu wa Makka. Kwa
hakika, hii ni neema kubwa kwetu kwani wapo wenzetu wengi miongoni mwetu ambao
hawakuweza kuifikia siku hii. Kwa hivyo,
ni wajibu wetu kumshukuru Mola wetu kwa kuturuzuku neema hii ya kuifikia siku hii,
ambapo ni miezi michache tu iliyopita,
tulijaaliwa kuisherehekea sikukuu ya Idd-el-Fitri kwa amani na salama. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaaliya
siku hizi za furaha na kuwa pamoja katika kuzisherehekea.
Ndugu
Wananchi,
Ni jambo la kutia moyo na kumshukuru
Mwenyezi Mungu kuona kwamba idadi ya mahujaji wa Zanzibar imekuwa ikiongezeka
kila mwaka. Katika mwaka huu wa 2015, taasisi zinazosafirisha mahujaji hapa
Zanzibar kutokana na uongozi bora na uzoefu wa kuzifanya shughuli za Hijja za
Kamisheni ya Wakfu na Mali ya Amana zimeweza kusafirisha mahujaji 1,502, kati
ya mahujaji 3,000 waliosafirishwa kutoka Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Idadi hii ni ziada ya mahujaji 222
ikilinganishwa na idadi ya mwaka jana ambapo taasisi za Zanzibar zilisafirisha
mahujaji 1,280 kati ya 2,500 kwa Tanzania nzima. Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imewekewa
fursa ya kupeleka katika Hijja, mahujaji
25,000 kwa mujibu wa makubaliano ya OIC.
Ni dhahiri kuwa idadi ya mahujaji wetu kwa sasa ni ndogo ikilinganishwa
na nchi nyingine za Afrika ya Mashariki.
Aidha, imebainika kuwa mahujaji wetu wengi wanaokwenda Hijja ni watu wa
hali za kati na hali za chini kiuchumi. Wengi wao huifanya ibada hii baada ya
kupata fedha zao za kiinua mgongo.
Kwa lengo la kuwasaidia wananchi wengi zaidi
waweze kupata fursa ya kuitekeleza ibada ya Hijja kwa wepesi na mapema zaidi,
tayari Serikali imeanza kazi ya kufanya upembuzi yakinifu ili kuanzisha Mfuko
wa Hijja Zanzibar. Mfuko huo utakapoanzishwa, watu wengi zaidi watapata nafasi
na uwezo wa kuweka fedha kidogo kidogo kwa mujibu wa uwezo wao. Hatimae,
watamudu kutekeleza ibada za Hijja na Umra kwa mujibu wa makubaliano na taratibu
zitakazowekwa na mfuko. Nchi nyingi
ambazo zimeanzisha mifuko ya aina hii ikiwemo Malaysia, wanamudu kumaliza idadi
yote ya nafasi za mahujaji walizowekewa.
Bila ya shaka, kwa kupitia utaratibu wa mfuko
huu, mahujaji wetu watapata uwezo wa kufanya maandalizi mazuri ya misafara ya
Hijja. Kadhalika, kwa miezi yote Waumini wengi watapata nafasi ya kwenda
kutekeleza ibada za Umra na ziara.
Mifuko hii pamoja na kuwawezesha Waislamu kuhiji husaidia sana shughuli
za kidini na kijamii. Tayari Kamisheni
ya Wakfu ya Mali ya Amana kwa kushirikiana na Benki ya Kiislamu ya PBZ, Mfuko
wa Hifadhi ya Jamii (ZSSF), Shirika la Bima la Zanzibar (ZIC), Umoja wa Taasisi
za Hijja Zanzibar na wataalamu wa Uchumi na Utawala kutoka taasisi za kiislamu
wanalifanyia kazi suala hili na
matarajio ni kuanza kufanya kazi kabla ya Hijja ijayo. Tumuombe Mwenyezi
Mungu atufanyie wepesi katika kulitekeleza jambo hili la kheri.
Ndugu
Wananchi,
Ibada ya Hijja waliyoitekeleza ndugu zetu
mahujaji huko Makka ina mchango muhimu wa kukuza imani ya mja na uchamungu wake
kutokana na mafunzo muhimu yanayotokana na ibada hiyo yenye historia ndefu tangu
kwa baba wa Mitume Nabii Ibrahim (AS).
Miongoni mwa mafunzo muhimu ya ibada ya
Hijja ni kudhihirika kwa umoja wa Waislamu duniani ambao wanakutanika katika Mji
wa Makka kwa kuitikia wito wa Mwenyezi Mungu. Umoja wa waislamu umebainishwa
katika aya mbali mbali za Kurani ambapo katika aya 92 ya Surat Al-Anbiyaa,
Mwenyezi Mungu ametuthibitishia hilo na kututaka tumuabudu Yeye kwa kusema,
“Hakika umma wenu huu ni umma mmoja tu,
na mimi ni Mola wenu, basi niabuduni”.
Hali hii ya umoja, tunapaswa tuione umuhimu
wake na tuiendeleze katika maisha yetu ya kila siku hasa sisi tunaoishi katika
nchi moja na watu wa nasabu moja. Sote
tuna wajibu wa kuimarisha umoja wetu na kuepukana na masuala yote
yanayohatarisha umoja na mshikamano wetu kwa lengo la kutafuta radhi za
Mwenyezi Mungu na kupiga hatua kubwa zaidi za maendeleo.
Ndugu
Wananchi,
Jambo jengine muhimu linalotokea katika
kipindi cha ibada ya Hijja ni Waislamu kutoka sehemu mbali mbali duniani kupata
fursa ya kukutana na kujadili masuala yanayohusu maendeleo ya jamii ya kiislamu
katika nyanja za kisiasa, kiuchumi na ustawi wa jamii. Katika hali kama hii, masuala mengi ya msingi
huzungumzwa na Waislamu wenye taaluma, maarifa, uzoefu na kubadilishana mawazo
kwa njia ya majadiliano na kupata njia za kukabiliana na changamoto za
maendeleo zilizopo. Fatwa zinazotolewa
miongoni mwa maulamaa wa kiislamu, huwa ni dira muhimu katika kuleta ustawi wa jamii
zetu.
Hili nalo ni jambo la kuliendeleza katika
kutafuta ufumbuzi wa changamoto mbali mbali zilizomo katika jamii yetu. Majadiliano ni njia nzuri na ya pekee katika
kutafuta ufumbuzi wa changamoto zetu za maendeleo ndani ya jamii yetu. Ni wazi kwamba, jamii haiwezi kupata
maendeleo kama watu watakosa kushirikiana na kuaminiana. Kwa hivyo, kwa kutumia maarifa yanayotokana
na mafunzo ya Ibada ya Hijja ni miongoni mwa faida tunazozipata katika
utekelezaji wa Ibada hii na ni wajibu wetu tuyatumie mafunzo hayo katika maisha
yetu ya kila siku.
Ndugu
Wananchi,
Vile vile, katika ibada ya Hijja tunajifunza umuhimu wa mahujaji kuwa na subira na kwa wale tunaobaki nasi huwa tunawasubiri
ndugu, jamaa na marafiki zetu waliokwenda kuitekeleza ibada hii kwa lengo la
kutafuta radhi za Mwenyezi Mungu. Ibada
ya Hijja inajumuisha taratibu nyingi pamoja na ugumu wa safari, gharama na haja
ya kuwa na uzima wa afya na ustahamilivu.
Yote haya yanahitaji kuwa na subira ambayo ni sifa muhimu ya Mitume yote
na Masahaba. Kwa wale wanaoondokewa na
ndugu na jamaa zao kwa ajili ya kwenda kuitikia wito huo wa Mwenyezi Mungu nao
hulazimika kuwa na subira.
Kuwa na subira ni jambo lililosisitizwa sana
katika Kurani na Sunnah kupitia visa vya Mitume wa Mwenyezi Mungu na Masahaba
ili iwe ni mafunzo kwetu. Katika
kusisitiza faida ya kuwa na subira kwa muumini, Bwana Mtume (S.A.W) katika
hadithi iliyopokelewa na Al-Bukhaariy na Ahmad amesema:
“Kubakia katika subira kwa siku moja
katika njia ya Mwenyezi Mungu ni bora zaidi kuliko dunia na vyote vilivyomo
ndani yake”
Ni dhahiri kuwa kuna fadhila kubwa katika
kusubiri kwa siku hizi ambazo wenzetu wanatekeleza ibada ya Hijja huko Makka na
sisi tunaowasubiri tukiwaombea dua ili ibada zao zikubaliwe. Aidha, masheikh wetu wanatuelekeza kuwa
subira yenye malipo zaidi ni ile ya kusubiri kwa kujizuwia kutekeleza mambo
mabaya kwa kutegemea malipo mema kutoka kwa Mola wetu Subhana Wataala. Tumuombe Mwenyezi Mungu atupe subira kwa
kutegemea fadhila na kufuata maamrisho ya Mola wetu.
Ndugu
Wananchi,
Miongoni mwa masuala muhimu tuliyosuniwa
katika sikukuu hii ya Idd el Hajj ni kuchinja mnyama. Uchinjaji huu unatupa funzo la utiifu wa
Nabii Ibrahim (AS) na kutawakali kwake pamoja na mwanawe Ismail (AS) katika
kutekeleza amri ya Allah kupitia ndoto aliyooteshwa. Utiifu wao wa kweli kwa Mwenyezi Mungu
uliwawezesha kufuzu, jambo ambalo la mazingatio kwetu sote na kujifunza ili
tuweze kufanikiwa katika masuala yetu mbali mbali ya kimaisha.
Mafundisho ya uislamu yanasisitiza umuhimu
wa kuitekeleza suna hii ambayo ni ibada na hatua ya kumkurubisha mja na Mola
wake. Siku hii ya leo imesuniwa kuchinja
mnyama baada ya sala ya Idd na kutumia sehemu ya nyama na nyengine kuwapa
marafiki na wahitaji wengine waliokuwa hawana uwezo katika jamii.
Ni wajibu wetu kuyaendeleza mambo kama haya
ya kheri na uchamungu ili iwe ni sababu ya kukuza mapenzi mema baina yetu na
kutafuta radhi za Mwenyezi Mungu kwa kufanya anayoyaridhia na kujiepusha na
makatazo yake. Kadhalika, tuendelee
kuyatumia mafunzo yanayotokana na ibada zetu kwa vitendo ili iwe ndiyo dira ya
kuleta ufanisi katika maisha yetu ya kila siku.
Ndugu
Wananchi,
Tuna wajibu mkubwa wa kumshukuru Mwenyezi
Mungu Mtukufu kutuwezesha kuungana na waislamu wenzetu duniani katika
kuisherehekea sikukuu hii ya Idd el Hajj katika hali ya amani na salama. Nimepata faraja kubwa kuweza kushirikiana na
waislamu wenzetu wa Mkoa huu wa Kaskazini Unguja kwa kusali pamoja sala ya Iddi
leo asubuhi katika kiwanja cha mpira cha Polisi Mkokotoni na hivi sasa kwa
pamoja tumejumuika katika kituo hiki cha Mafunzo ya Amali kwa ajili ya Baraza
la Iddi.
Natoa shukurani zangu na naipongeza Kamati
ya Maandalizi kwa kushirikiana vyema na uongozi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja
pamoja na Wilaya zake katika kuifanikisha shughuli hii. Kadhalika, nawapongeza kwa dhati wananchi
wote wa Mkoa huu kwa kujitokeza kwa wingi katika sala ya Idd na kwa
mashirikiano yenu mnayoendelea kutupa. Tumuombe Mwenyezi Mungu azidishe
ushirikiano huu katika kuifanikisha mipango yetu ya maendeleo na kuimarisha
ustawi wa wananchi wote.
Ndugu
Wananchi,
Nimefarajika na hatua kubwa ya maendeleo
tuliyoyafikia katika Mkoa huu wa Kaskazini Unguja katika sekta za kiuchumi, huduma
za jamii na muamko wa wananchi katika kuzitumia fursa mbali mbali za
kujiendeleza kiuchumi kwa kushirikiana na Serikali. Napenda nikupongezeni sana kwa mafanikio
hayo.
Katika kuhakikisha kuwa, Mikoa yetu inazidi
kuimarika kiuchumi, kuongeza fursa za ajira hasa kwa vijana na kuimarisha
upatikanaji mzuri wa huduma za jamii, Serikali imeazimia kujenga mji wa kisasa
katika Mkoa huu wa Kaskazini kwenye vijiji vya Kijini na Matemwe. Ujenzi wa barabara wenye urefu wa kilomita
20.2 kutoka Matemwe kupitia Kijini hadi Kidoti umekwishaanza. Wananchi wa Mkoa
huu wananufaika na kuwepo kwa idadi kubwa ya hoteli za kitalii kwa kuzingatia
kauli mbiu ya utalii kwa wote.
Ndugu
Wananchi,
Inatia moyo kuona vijana na kinamama wa Mkoa
huu walivyojidhatiti kujiendeleza kiuchumi kwa kutengeneza bidhaa mbali mbali
na kuzalisha mazao kwa ajili ya kuuza katika Hoteli za kitalii. Aidha, wananchi wengi wa maeneo ya Bumbwini,
Mkokotoni, Bwekunduni, Fungurefu na vijiji nyengine vya Mkoa huu wameimarisha
uchumi wao kwa kujishughulisha na biashara ya madagaa ambayo nimearifiwa kuwa
husafirishwa hadi Kongo na nchi nyengine za jirani.
Wito wangu kwenu ni kuwa muendelee kushirikiana
na Serikali yenu katika kuziimarisha shughuli zetu hizi ili ziweze kutoa tija
zaidi. Kadhalika, vijana wanaokosa fursa
ya kuendelea na masomo wakitumie kituo cha Mafunzo ya Amali cha Mkokotoni ili
wajiendeleze kupata ujuzi wa kazi mbali mbali za amali unaotolewa na kituo
hicho. Kazi hizo ni pamoja na useremala,
ushoni, uchoraji, uwashi, ufundi bomba, magari, mafriji, mapishi ya aina mbali
mbali na huduma za mahoteli. Vile vile,
katika mwezi wa Agosti, 2015 tulifungua kituo cha ujasiriamali “Bare-foot
College” kama kiliopo huko India, kituo kinachotengeneza vifaa vya umeme wa jua
ndani ya Mkoa huu ambacho ni cha aina yake na maalum kwa kinamama. Hizo ni fursa ambazo mnapaswa kuzitumia vyema
katika kupiga hatua zaidi za maendeleo.
Ndugu
Wananchi,
Serikali kwa kushirikiana na washirika wetu
wa maendeleo pamoja na ushirikiano wa wananchi tumeweza kupiga hatua kubwa
katika kuimarisha upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama katika Mkoa huu
kwa kutekeleza miradi mbali mbali. Hali
ya upatikanaji wa maji safi katika Mkoa huu imefikia asilimia 71.68. Mafanikio hayo yamefikiwa baada ya kutekeleza
miradi mikuu mitatu ya maji safi na salama katika Mkoa huu. Miradi hiyo ni mradi wa Serikali kupitia
Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), Mradi wa Maji wa Ras-al-Khaimah na Mradi wa
Maji wa ADB ambayo kwa pamoja imewanufaisha wananchi mbali mbali wa Mkoa huu
kupata huduma za maji safi na salama.
Kadhalika, Serikali imeimarisha huduma za
hospitali ya Koteji ya Kivunge pamoja na vituo vya afya vyengine katika Mkoa
huo ili kuziimarisha afya za wananchi.
Wajibu wa wananchi ni kuzitumia huduma hizi pamoja na wazazi na walezi
kuhakikisha watoto wetu wanapelekwa kupata chanjo ili kuwakinga na maradhi
mbali mbali na kinamama wajawazito wawe wanajifungulia hospitali katika azma ya
kuziimarisha afya zao.
Ndugu
Wananchi,
Pamoja na mafanikio hayo katika kuziimarisha
huduma za jamii, napenda nitumie fursa hii, kuutaka uongozi wa Mkoa wa
Kaskazini; Unguja kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi pamoja na taasisi
zinazowasimamia madereva wachukue hatua madhubuti katika kukabiliana na tatizo
la ajali za barabarani katika Mkoa huu. Taarifa kutoka Jeshi la Polisi zinabainisha
kazi kubwa tuliyo nayo katika kukabiliana na tatizo la ajali za
barabarani. Kwa mujibu wa taarifa hiyo,
katika kipindi cha kuanzia mwezi wa Januari hadi Agosti mwaka 2014, jumla ya
ajali za barabarani 391 zimetokea Unguja na Pemba. Ajali hizo zilizosababisha vifo vya watu 104
na watu 728 wamejeruhiwa. Katika Mkoa
huu wa Kaskazini Unguja zilitokea ajali 64 zilizosababisha vifo vya watu 16 na
jumla ya watu 259 walijeruhiwa.
Katika mwaka huu wa 2015 kwenye kipindi kama
hicho, tayari zimetokea ajali za barabarani 393 Unguja na Pemba ikiwa ni ziada
ya ajali mbili ikilinganishwa na mwaka 2014.
Ajali hizo zimesababisha vifo vya watu 91 na watu 450 wamejeruhiwa. Katika kipindi hiki kwenye Mkoa huu,
kumetokea ajali za barabarani 73, zilizosababisha vifo vya watu 15 na kuwajeruhi
watu 123. Ni wazi kuwa takwimu hizo si
za kufurahisha, kwa hivyo jitihada za pamoja zinahitajika ili kupunguza na
hatimae kuliondoa kabisa tatizo la ajali za barabarani kwa vile asilimia kubwa ya
ajali hizi zinasababishwa kwa kutokuzingatiwa kwa sheria za usalama barabarani
na matumizi mazuri ya barabara zetu.
Ndugu
Wananchi,
Kwa mara nyengine napenda nikumbushe umuhimu
wa sisi viongozi wa kisiasa, kijamii na wa madhehebu ya dini kuwasisitiza
wafuasi wetu umuhimu wa kuilinda amani na kujiepusha na vitendo vyote
vinavyoweza kutuondolea amani na utulivu tuliokuwa nao. Nimekuwa nikisema mara kadhaa kuwa amani
haina mbadala. Bila ya amani hatuwezi kupata
maendeleo yoyote. Kutokuwepo kwa amani kunahatarisha
uhai wa watu na ni sababu ya kuharibu miundombinu ya aina mbali mbali na kuzua
fadhaa katika jamii. Ni dhahiri kuwa
kutoweka kwa amani huwaondolea wasaa hata waumini katika kutekeleza ibada za
kumuwabudu Mola wao. Katika aya ya 112
ya Suratun Nahl, Mwenyezi Mungu anatutanabahisha kwa kutupa mfano wa waliopewa
neema ya amani na utulivu wakashindwa kuitunza kwa kusema:
“Na Mwenyezi Mungu anakupeni mfano wa
mji uliokuwa na amani na utulivu, riziki yake ikiujia kwa wingi kutoka kila
mahali. Lakini ukazikufuru neema za
Mwenyezi Mungu, kwa hivyo Mwenyezi Mungu akauvika vazi la njaa na khofu kwa
sababu ya yale waliyokuwa wakiyafanya”.
Tumuombe
Mwenyezi Mungu atuepushe na mtihani huo.
Napenda nikuhakikishieni kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zitaendelea kukabiliana na wale wote watakaofanya vitendo
vinavyoashiria kutaka kuvunja amani ya nchi yetu wakati wote na katika kipindi
hiki cha Kampeni za Uchaguzi Mkuu, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi. Hakuna atakayeonewa au kudhulumiwa kwa njia
yoyote ile lakini Serikali ina wajibu wa kikatiba wa kuwalinda watu wote na
mali zao pamoja na wageni wanaoitembelea nchi yetu.
Ndugu Wananchi,
Hivi sasa tumo katika kusherehekea sikukuu,
lakini kama tunavyofahamu baada ya siku chache zijazo tunatarajia kuanza kupata
baraka za mvua za Vuli. Mvua ni neema
kubwa kwetu hasa kwa kuendeleza shughuli za kilimo na upatikanaji wa maji
nchini. Kwa hivyo, ni vyema tukaanza maandalizi ya kilimo cha mazao na matunda
mbali mbali yanayostawi na kunawiri katika msimu wa Vuli.
Kwa upande mwengine, ni muhimu tukazingatia
kwamba baadhi ya nyakati, Mwenyezi Mungu hutupa neema ya mvua ambayo vile vile
huwa na mitihani ili kuzipima nafsi zetu. Mwenyezi Mungu ametuambia katika
Surat Muhammad aya ya 31 kwamba:
“Nitakufanyieni mitihani mpaka
muwadhihirishe (wajulikane) wale wanaopigania dini miongoni mwenu, na
wanaosubiri nasi tutadhihirisha habari zenu”.
Sote tunakumbuka jinsi baadhi ya wananchi wenzetu
walivyopata mitihani ya mafuriko katika sehemu mbali mbali za Unguja na Pemba
katika msimu wa mvua za Masika uliopita. Tulishuhudia matukio mengi ya
kusikitisha katika maeneo ya Kwahani, Mwanakwerekwe, Tomondo na kadhalika, katika
mwezi Mei, 2015. Mimi na viongozi
wengine tulipata fursa ya kuwatembelea wananchi waliopata maafa kwa ajili ya
kuwafariji.
Napenda niwakumbushe wananchi kwamba katika
nyakati mbali mbali, Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini “Tanzania Meteorological
Agency (TMA)”, imetahadharisha kwamba katika msimu wa mvua za Vuli, upo
uwezekano mkubwa wa kutokea mvua kubwa za “El-Nino” kutokana na hali ya
sasa ya kuongezeka kwa joto katika Bahari ya Pasifiki. Ongezeko hilo la
joto katika bahari hiyo kama litaendelea kuwepo, linaweza kuenea hadi
katika Bahari ya Hindi na kusababisha mvua kubwa za “El-Nino” katika
ukanda wote unaopakana na bahari ya Hindi.
Kwa kawaida mvua kubwa za “El-Nino”
zinapolikumba eneo la nchi husababisha mafuriko na kuacha madhara makubwa
ya uharibifu wa miundombinu na mali za wananchi; hasa nyumba zilizojengwa
katika maeneo ya mabondeni. Wataalamu
wetu wanatufahamisha kwamba kuna viasharia vingi sana vya kuonesha uwezekano wa
mvua za “El Nino” kutokea mwaka huu katika Ukanda wa Afrika Mashariki.
Huu ni utabiri wa binaadamu lakini Mwenyezi
Mungu ana kudra na shani yake. Utabiri huu unatokana na elimu na maarifa
aliyotupa Subhana Wata’ala, ili kurahisisha maisha yetu. Ni vyema tukaitumia
elimu hii vizuri kwa kuanza kuchukua tahadhari zinazofaa. Nasaha zangu kwenu
wananchi ni kwamba tuzingatie hekima ya ule usemi maarufu kwamba, “Tahadhari kabla ya athari”. Kwa hivyo, taasisi zinazoshugulikia usafi wa
miji ziongeze kasi katika kusafisha misingi ya maji machafu na njia za maji,
usafi wa mazingira yetu ili kuepukana na maradhi. Ninawanasihi wananchi tuache ujenzi katika
sehemu za mabonde na sote tuwe na moyo wa kusaidiana wakati wote, hasa pale
Mwenyezi Mungu anapotupa mitihani mbali mbali.
Ndugu
Wananchi,
Kwa baraka ya siku hii, tuwaombee mafanikio
vijana wetu wa darasa la sita, la saba na Kidato cha Pili waliofanya mitihani
yao hivi karibuni na Mwenyezi Mungu awape matayarisho mema vijana wetu
wanaojiandaa na mitihani ya Taifa Kidatu cha Nne. Awajaalie wote wafaulu katika
mitihani yao. Awape wagonjwa wetu wote
shifaa ya maradhi yao na aijaalie nchi yetu amani, upendo na masikilizano na
mapenzi zaidi baina yetu.
Namalizia hotuba yangu kwa kukuombeeni nyote
kila la kheri katika kuisherehekea sikukuu hii ya Idd-el-Hajj. Tuisherehekee sikukuu hii kwa mambo ya kheri
na kujiepusha na yale yote yanayomchukiza Mwenyezi Mungu. Tumuombe Mwenyezi Mungu azikubali ibada za
mahujaji wetu wote. Tunapowasiliana nao
tuwaombe waiombee nchi yetu iendelee kuwa ya amani na utulivu. Mwenyezi Mungu
awape uwezo wale wote wenye azma ya kuitekeleza ibada ya Hijja waweze kufanya
hivyo kama walivyokusudia na kupata fursa ya kuishi japo kwa siku chache katika
miji mitukufu ya Makka na Madina Yarabbil Allamina
Mwenyezi Mungu awarehemu wazee wetu, ndugu,
jamaa na marafiki zetu wote waliotangulia mbele ya haki. Aijaze neema na baraka
nchi yetu. Atupe uwezo na wepesi wa kuitekeleza mipango yetu ya maendeleo kama
tulivyoipanga. Atujaalie afya njema na
riziki za halali. Mwenyezi Mungu atujaalie sote turudi nyumbani kwa salama na
amani.
Ahsanteni
kwa kunisikiliza.
IDD
MUBARAK
KULLU
AAM WAANTUM BIKHEIR
No comments:
Post a Comment