Habari za Punde

Jumuiya ya Wazee Zanzibar Imeitaka Serikali Kutunga Sheria Maalum ya Kuwalinda.

Na. Miza Othman Maelezo. 
Jumuia ya Wazee  Zanzibar  imeiomba Serikali   kutunga  sheria  maalum ya kuwalinda na  kupewa nafasi  katika chombo cha kutunga sheria ili waweze kuwakilisha  maoni  yao  na kutafutiwa ufumbuzi unaofaa.

Akizungumza na waandishi wa habari  katika Ukumbi wa Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC)  Rahaleo, Mwenyekiti wa Jumuia hiyo  Bi. Salma Saleh Ismail  amesema wazee wanakabili na changamoto nyingi  zinazohitaji  kuwa na  sheria maalum  na uwakilishi  ndani ya Baraza la kutunga sheria.  

Amesema vijana pamoja na watoto wametungiwa sheria zao hivyo na  wazee wanahaki ya  kuandaliwa sheria ili kuepukana na unyanyasaji  na udhalilishaji wanaofanyiwa wazee.

“Vijana na watoto wamepewa kipaumbele kwa kutungiwa sheria za kuwalinda  na sisi  wazee tunahitaji sheria kama hizo na kupatiwa  nafasi ili tuweze kuwakilishwa katika chombo cha kutunga Sheria,” amefahamisha Mwenyekiti huyo.


Aidha amesema lengo la Jumuiya  ya Wazee  Zanzibar ni kuboresha maisha ya wazee na kupambana na  unyanyasaji na  kudharauliwa na kuhakikisha wazee  wanaenziwa  na kupatiwa   huduma muhimu  katika meneo wanayoishi.

“Hakuna kitu muhimu  kama kumenzi mzee kwani unapata fadhila nyingi, na sisi tumeona kuwa wazee wamesahaulika na ndio sababu  tumeamua kuanzisha Jumuia hii  kwa kushirikana na Serikali tuweze kuwasaidia,” ameeleza Bi Salma

Amefahamisha kuwa Jumuiya imeanzisha utaratibu wa  kuwsajili wazee wote wenye umri kuanzia miaka 60  kupitia  kwa masheha  wao  na kwa kuanzia  tunawaombea pencheni ya kila mwezi ili waweza kujisaidia kimaisha.

Wazee wameishauri  Serikali kuwaandalia utaratibu maalum katika vituo vya afya kwa kuwawekea  sehemu yao ya matibabu  ili kuepukana na msongamano wa wagonjwa katika vituo  na hali zao za kiafya.

Nae Katibu wa Jumuiya hiyo Amani Suleiman Kombo amesema Jumuiya imetoa elimu  sehemu mbali mbali kupitia taasisi za dini kwa lengo la   kuhamasisha wananchi  umuhimu wa wazee ili kuepukana vitendo vya unyanyasaji na udhalishaji.

Siku ya wazee  Duniani huadhimishwa kila ifikapo tarehe 01Oktoba  ambapo  Zanzibar  mwaka huu itaadhimishwa kwa  shughuli mbali mbali ikiwemo kuwatembelea wagonjwa, kutembelea sehemu za kihistoria na kutafanyika Bonaza  la michezo.

                                 IMETOLEWA NA IDARA YA HABARI MAELEZO                                                                         ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.