Ni simulizi ya moja wa mahujaji wa mwaka jana 2014 aliyebahatika kutulia na kuiweka ziara yake katika maandishi. Ni ndefu lakini imejaa mafundisho.
Alhamdulillaah
nilibahatika kuwa miongoni mwa waliojaaliwa kuitekeleza Ibada ya Hajj mwaka
1435.(2014)
Nilikuwa
kwenye mafunzo ya kivitendo ya siku sita kuanzia tarehe 8 Dhulhijjah -mfunguo tatu mpaka tarehe 13
Dhulhijjah 1435.
Kwa
wale watakaombatana na safari yangu hii ni kwamba Hijja ni ibada ambayo
hufanyika katika mji wa Makkah, Saudi Arabia ni matendo maalum, yanayofanyika
katika wakati maalum, sehemu maalum na kwa ajili ya watu maalum. Ni nguzo ya
tano katika nguzo za kiislamu ambayo humuwajibikia kila Muislamu mwenye uwezo
mara moja katika maisha yake.
Naam
ni siku sita tu lakini nimeweza kujifahamu na kujitambua katika kipindi cha
siku sita ambazo zitabakia katika kumbukumbu ya maisha yangu. Kwani mafunzo
yake ya kinadharia, kivitendo na kiroho ni mafundisho nadra unayoweza kuweza
kuyapata kwa kipindi kifupi na yakaweza kuleta athari kubwa katika maisha ya
Muislamu.
Nikikumbuka
kwa mara ya pili nilipoivaa Ihraam siku ya Tarwiyah, tarehe 8 Dhulhijjah na
kutia nia ya Hajj na kuanza Talbiyah “Labbayka Allaahumma Labbayka Labbayka Laa
shariyka laka Labbayka Innal hamda Wanni’imata laka walmulk Laa shariyka laka”.
Sikujikuta peke yangu, kila ninaemkuta njiani anatamka Talbiyah kama mimi. Kila
ninaemkuta njiani amevaa Ihraam kama mimi shuka mbili tu nyeupe miongoni mwa
wanaume hana kitu chochote ndani kwani ni haramu kuvaa nguo yoyote iliyoshonwa
wakati upo katika Ihraamu. Sote tumevaa viatu vya kawaida tu mithili ya kanda
mbili au viatu visivyofunika mguu wote na hakuna hata mwanamme mmoja aliyevaa
kofia, ukishahirimia hutakiwi kuvaa kofia kichwani kwa mwanamme au kupaka
manukato ya aina yoyote.
Kila
ninamkuta njiani simjui jina lake wala wapi anapotoka, simjui kama ni Daktari
au ni Mwalimu, Mpagazi au Mchuuzi, ni mheshimiwa au mtu wa kawaida, mweupe,
mweusi mkubwa, mdogo lakini namjua kama
ni ndugu yangu Muislamu na sote
tumetamka Laa Ilaaha Illa Llaah Muhammadun Rasuulu Llaah. Kalima au neno
hili ndilo lilitukutanisha katika ardhi ya Haram, Kalima hili ndilo
litakalokutanisha peponi, Kalima hili ndilo litakalotuepusha na adhabu kali ya
moto wa Allaah ‘Azza wa Jall ikiwa tutakamilisha masharti yake saba.
Tulipofika
Mina huku tukiendeleza Talbiyah na kuomba dua kwa Allaah ‘Azza wa Jall, kila
nikiirudia Talbiyah basi nafsi yangu inanikumbusha ujumbe mzito uliopo kwenye
talbiyah nao ni wa Tauhiyd kumpwekesha Allaah ‘Azza wa Jall kwa ibada na kila
kwa kila kitu. Tunamhakikishia Allaah
‘Azza wa Jall kwamba hana mshirika huku tumemwitikia, tunamthibitishia Allaah
‘Azza wa Jall kwamba hakika himidi na shukrani, neema na ufalme vyote ni vyake
pekee na hana mshirika.
Nikaikumbuka
aya katika Qur’aan inayosema: “hakika Sala zangu, vichinjwa vyangu, uhai wangu
na mauti yangu vyote ni vya Allaah Mola wa viumbe vyote, hana mshirika na hivyo
nimeamrishwa kuwa Muislamu wa awali”. Naam Hijja ni darsa muhimu
inayotufundisha somo la Tawhiyd kwani Mtume Muhammad Swalla Allaahu ‘alayhi
wasallam alihama Makkah kwenda Madina (kwa sababu ya kuisimamisha Tawhiyd) na
aliporudi kuikomboa Makkah aliikomboa bila ya kumwaga damu na kuisimamisha
Tawhiyd.
Naam
Mina ni Masha’aril Haraam mojawapo katika sehemu takatifu kwa Waislamu ni
sehemu ambayo ukiomba kwa Allaah ‘Azza wa Jall hutakabaliwa du’aa yako.
Nilijitahidi kuomba na kila Muislamu ninaemuona yumo katika maombi, au dhikr au
anasoma Qur’aan mpaka nafsi inanisuta mbona siku zote ulikuwa hufanyi Ibada
kama hivi? Nikaijibu nipo katika sehemu takatifu na nimekuja kwenye mafunzo ya
vitendo nafsi we. Naam nikajaaliwa kuzisali sala za Adhuhuri, Alasiri,
Magharibi na Isha pamoja na Alfajiri Jamaa kwa kupunguza Sala zenye rakaa nne
kama alivyofanya Mtume Swalla Allaahu ‘Alayhi Wasallam alipohiji.
Tulipoamka
Alfajiri siku ya pili ya mafunzo, Siku ya Arafah siku adhimu katika masiku ya
dunia, siku muhimu kwa mwenye kuhiji kwani ndiyo nguzo kuu ya Hajj ambayo
ikikosekana basi aliyefanya safari hii hana Hajj, tulijiandaa kuelekea Arafah
asubuhi na mapema kutoka Mina.
Tulipowasili
viwanja vya ‘Arafah, nilihakikisha nipo katika mipaka yake ili Ibada yangu
ikamilike. Tulibahatika mwaka huu siku ya ‘Arafah kuangukia Ijumaa kama
ilivyokuwa kwa kipenzi chetu Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam miaka 1435
iliyopita hivyo tukapata fursa mbili za kuweza kukubaliwa duaa, maombi, shida
na matlaba yetu – fusa ya ‘Arafah na fursa ya Ijumaa.
Ilipofika
muda wa kuanza ‘Arafah (baada ya Zawaal yaani jua kutenguka) tulisali Adhuhuri
na Alasiri jamaa ya kutanguliza na kupunguza kwa kuzisali rakaa mbili mbili.
Kisha tukatangaziwa kwamba ule muda ambao shetani anaukasirikia kadri ya
kukasirika umefika wa kupeleka maombi yetu, shahada zetu, maelezo yetu, CV zetu
kwa Allaah ‘Azza wa Jall umeanza.
Siku
ambayo Mtume wetu Swalla Allaahu ‘Alayhi wasallam ambaye tayari ameshasamehewa
madhambi yake yaliotangulia na yatakayokuja alisimama kuanzia adhuhuri mpaka
kuzama kwa jua akiomba tu huku mikono yake akiwa ameinyanyua kwa masaa takriban
sita. Nikajiuliza wapi mimi na Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam? Nikajiambia kimoyomoyo nijaribu kuiga mwenendo
wake nikatoka nje ya hema nikaelekea qiblah na kuanza kuomba kila dua
ninayoijua au niliyobahatika kuisikia na kuihakikisha si miongoni mwa dua
zilizokuwa na walakini.
Ni
siku ambayo niliingiwa na simanzi, mwili nikausikia una joto na huku chozi
likinitoka ninamuomba Allaah ’Azza wa Jall kwani niliwahi kuisikia hadithi ya
Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam inayosema jicho litalotoa machozi kwa
ajili ya Allaah halitogusa moto siku ya kiama! Naam licha ya jitihada zangu sikumfikia
au kuifikia rekodi ya Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi Wasallam.
Kulikuwa
na joto lakini sikujali, kwani sikuwa pekee yangu kwenye jua, mamilioni ya
waislamu tulikuwepo ‘Arafah sote tukifanya jambo moja tu; Kuomba. Joto ni kitu
gani mbele ya joto la moto wa Jahannam!
Naam
‘Arafah ni siku adhimu, ‘Arafah ni siku pekee ambayo haina mfano wake kwani
hakuna siku katika masiku ya dunia ambayo Allaah ‘Azza wa Jall huwaachia huru waja
wake na moto kwa wingi kama siku ya ‘Arafah. Ndio maana shetani huichukia.
Allaah
‘Azza wa Jall katika siku hii huwa karibu na Malaika na kuwauliza: “Wanataka
kitu gani waja wangu hawa?” Allaahu Akbar.
Naam
ikiwa ‘Allah ‘Azza wa Jall amewasamehe waja wake siku hii hata na mimi
nilipokuwa nimesimama ‘Arafah nilimhakikishia Allaah ‘Azza wa Jall kwamba
nimewasamehe wote walionikosea. Kwanini nisiwasamehe wakati nimehakikishiwa
ikiwa Hijja yangu itakubaliwa basi nitarudi kama ndio kwanza nazaliwa?
Nilipozaliwa sikuwa na niliemkosea wala alienikosea.
Kwanini
nisiwasamehe wakati Mtume Swalla Allaahu ‘alayahi wasallam alipofika Makkah na
kuikomboa aliwasamehe Maquraysh wote licha ya madhila, mateso na kila baya
walilowatendea waislamu na aliwauliza: “Mnadhani nitakufanyeni nini leo?”
Wakamjibu ‘Ndugu yetu uliye karimu , mtoto wa ndugu yetu aliye karimu’. Mtume
Swalla Allaahu ‘Alayhi wasallam akawaambia: “Nendeni nyote mko huru” Hili ni
darsa muhimu la kujifunza ndugu yangu tuwe ni wenye kusameheana kwa ajili ya
kupata radhi zake Allaah ‘Azza wa Jalla. Kama angelikuwa Allaah ‘Azza wa Jall
si mwenye kusamehe basi dunia hii isingelikalika ndio maana amejinasibu kuwa Yeye
ni Ghaafir – mwingi wa kusamehe na pia Ghaffaar -anaendelea kusamehe (kila
tukifanya makosa basi turudi kwake tuombe msamaha)
Ndugu
yangu katika imani unaeusoma waraka huu, ukitaka upate mafunzo
yatakayobadilisha mwenendo mzima wa maisha yako, jihimu uende Hijja na
ukasimame ‘Arafah. Ukitaka ujihisi upo karibu na Allaah ‘Azza wa Jall na huku
akisikia maombi na duaa zako, jihimu uende Hijja na umuombe Allaah ‘Azza wa
Jall siku ya ‘Arafah. Ukitaka kuachiwa huru na moto, jihimu uende Hijja na
uwepo katika viwanja vya ‘Arafah ukimuomba Allaah ‘Azza wa Jall maombi
yanayotoka ndani ya moyo wako, yaliyojaa Ikhlaas na kumthibitishia Allaah ‘Azza
wa Jall kwamba ni yeye pekee ndiye mwenye kupokea na kuyakubali maombi yote
yawe makubwa au madogo.
Ilipofika
magharibi mafunzo yetu yakaendelea kwa kwenda viwanja vya Muzdalifah kutekeleza
moja katika mambo yaliyo wajibu katika Hijja.
Muzdalifah
nimekutana na mafundisho kadhaa kama la kutakiwa kulala nje tena chini kwenye
jangwa lisilo na kitu chochote. Ni fundisho kubwa sana kwani hapo kila
aliyekuja Hijja bila ya kujali uwezo wake, ulwa wake, cheo chake anatakiwa
kulala chini kama alivyolala Mtume wetu Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam na
akatukumbusha kwamba: “chukueni kutoka kwangu matendo yenu ya Hajj”. Ndiyo nina
kitanda cha sita kwa sita nyumbani lakini Muzdalifah nimelala chini kwa ajili
ya kutekeleza Manaasik ya Hijja.
Muzdalifah
hukutanika Mahujjaaj wote wakiwa dhalili wakiwa na shuka mbili tu licha ya
utajiri waliojaaliwa nao, wakilala sehemu ya ardhi isiyokuwa na tandiko zaidi
ya zulia au busati kwa atakayejaaliwa licha ya neema ambazo Allaah ‘Azza wa
Jall amewajaalia baadhi ya waja wake. Yote ni kwa ajili ya kutufundisha
fundisho muhimu katika maisha kwamba tuondokane na kiburi na majivuni kwani
licha ya kujaaliwa kila tulichojaaliwa lakini utukufu ni wa Allaah ‘Azza wa
Jall pekee - Mwenye nguvu na mshindi na kuwepo kwetu Muzdalifah tunauthibitisha
utukufu huu kwa vitendo. Allaahu Akbar
Naam
tulipofika Muzdalifah tukasali Magharibi na Isha kwa kuzichanganya na kupunguza
Isha kwa kuisali rakaa mbili.
Kisha
tukatakiwa kuokota vijiwe vidogo tu saizi ya kokwa ya ubuyu kwa ajili ya kupiga
Minara ya Jamaraat. Nikaokota vijiwe sabini na kuongeza vichache. Kwa
nini sabini? Kwa sababu nitatakiwa kuvitumia kwa muda wa masiku matatu kama
sina haraka na kama nina haraka ningetumia kwa masiku mawili. Ndivyo alivyotupa
rukhsa Allaah ‘Azza wa jall katika Qur’aan.
Lakini
nilipovipitia vitabu vikanikumbusha kwamba kama nikitaka hasa kumfuata Mtume
Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam yeye aliokota
vijiwe saba tu Muzdalifah kwa ajili ya kupiga Jamaratul Kubra pekee ama vijiwe
vyengine aliviokota Mina. Mina pia kumeruhusiwa kuokota vijiwe.
Nikapanda
basi kurudi Mina nikitokea Muzdalifah huku nikiwapita maelfu na maelfu ya
Mahujjaaj waliokuwa wakielekea Mina kwa miguu.! Namshukuru Subhaana kwa
kujaaliwa usafiri lakini hapo nikajiuliza hivi Hijja yangu ni bora zaidi au
Hijja ya waendao kwa miguu?
Nikamkumbuka
Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam yeye alipohiji, alihiji akiwa juu ya
Ngamia. Kwa hivyo nikajikinaisha kwamba ninaetekeleza Sunnah ya Mtume wetu
Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam.
Tulipofika
Mina nikaendelea na siku yangu ya tatu ya mafunzo, siku hii huitwa siku ya
kuchinja – Yawmun Nahr. Ndio siku yenye mafundisho mengi kuliko siku nyengine
za Hijja. Tuendelee
Nikaianza
safari yangu kuelekea Jamaraat (kupiga mawe) nikitokea Mina kwa miguu ni mwendo
wa nusu saa tu, lakini kutokana na msongamano wa watu jinsi walivyokuwa wengi
ilinichukua saa 1.30 kufika Jamaraat.
Siku
kila aliyekuja kuhiji hutakiwa kupiga mawe Jamaratul ‘Aqabah au kubra. Mnara
mkubwa katika minara mitatu iliyopo eneo la Jamaraat.
Nilifika
salama usalimini eneo la kupiga mawe (hii ni sehemu ya hatari katika sehemu
zote za hijja kwa kuwepo msongamano mkubwa kila mwaka ambao mara nyingi hupelekea
vifo vya mahujjaaj). Nikakoma kusema Talbiyah kwani kisheria nikifika sehemu ya
Jamaratul ‘Aqabah ndiyo sehemu ya mwisho ya kusema Talbiyah ambayo niliikuwa
nikiisoma tokea nilipovaa Ihraam siku ya tarehe 8 dhulhijjah.
Nikatafuta
sehemu muwafaka ya kurusha mawe kutokana na wingi wa watu na nilipoipata
nikaanza kurusha kijiwe cha kwanza huku nikisema: Bismillaah Allaahu Akbar. Nikafuatanisha
na chengine kwa kusema Allaahu Akbar pekee bila ya
bismillaah hadi nikamaliza vijiwe saba. Jamaratul kubra ukimaliza kupiga mawe
hutakiwi kusimama baada yake na kuomba du’aa kama ilivyo kwa minara mengine na
pia ni Jamarah pekee ambalo limeruhusiwa kupigwa kabla ya Zawaal siku ya iyd (kuchinja).
Nilipomaliza
nikaendelea na safari yangu kwa miguu kutoka Jamaraat hadi ‘Aziziyah kitongoji
kimojawapo kaskazini mwa Makkah tulipofikia. Kutokana na msongamano safari hii
pia ilinichukua takriban saa nzima.
Alhamdulillah
nikatumiwa ujumbe mfupi kwenye simu yangu (kutoka kwa kiongozi wa kundi letu)
kwamba kichinjwa changu tayari kimeshachinjwa kwani hii pia ni mojawapo ya
Ibada inayotakiwa kufanyika katika siku hii au ziku za Tashriyq (yaani tarehe
11,12 na 13 Dhulhijjah). Nikaulizia nini maana ya Tashriyq? Nikajuulishwa na
wenye weledi na Hijja ni ile nyama inayochinjwa siku ya Eid huanikwa juani hadi
kukauka na kuhifadhiwa ndiyo maana yake. (kumbuka miaka hiyo hawakuwa na
majokofu ya kuhifadhi nyama kama tulivyo siku hizi)
Baada
ya kupumzika kidogo, nilikoga na kuvua Ihraam zangu kwani hapa tayari nimekuwa
nimetahallal (kutoka ihram) kidogo kwani nimeruhusiwa kufanya mambo yote
isipokuwa kustarehe na mke nikatakiwa kuendelea na mafunzo yangu kwa siku kwa
kuelekea Al Ka’abah kwa ajili ye kutekeleza nguzo mbili kuu za Hijja, kufanya
tawaaf kufanya Sa’iy.
Safari
yangu kutoka Aziziyah hadi Al Ka’abah ilinichukua saa 1.15 naam kwa miguu.
Nilipofika Al Ka’abah ambapo umati uliokuwepo hapo siku hii ukiteleza nguzo za
Hijja na umati mwengine ambao niliuacha Mina nikajisemea moyoni Alhamdulillaah,
haya ndio matunda ya kazi aliyoifanya Mtume Muhammad Swalla ‘Allaahu ‘alayhi
Wasallam. Ninayoshuhudia kwa macho yangu ni ushuhuda kwamba Mtume Muhammad
Swalla ‘Allaahu ‘alayhi Wasallam amefikisha ujumbe na kutimiza amana aliyopewa
na Allaah ‘Azz wa Jall. Nina imani Allaah ‘Azza wa Jall anashuhudia kwamba
Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam amefikisha ujumbe kama alivyoagizwa.
Nikaingia
msikitini kwa kuomba du’aa ya kuingia msikitini na kuelekea sehemu ya kuanzia
Tawaaf.
Tawaaf
ni ibada unayotakiwa uizunguke Al Ka’abah mara saba ukianzia sehemu lilipo jiwe
jeusi (Hajarul aswad). Unatakiwa kuzunguka ilhali Al Ka’abah ipo upande wako
kushoto ( anti clockwise). Ni mojawapo katika nguzo za Hijja na lazima ifanyike
veynginevyo Hijja haitosihi.
Tawaaf
ya nguzo huitwa Tawaaful Ifaadhah au Tawaafu Ziyaarah. Lazima uwe katika hali
ya tohara kabla ya kufanya tawaaf (uwe na udhu).
Sehemu
ya kuanzia imewekewa ishara ya taa rangi ya kijani pamoja na maelezo kwa
kiarabu kwamba hapa ndipo sehemu ya kuanzia na kumalizia Tawaaf. Nikaelekea
kona lilipo Hajarul Aswad (jiwe jeusi) na kuliashiria na kusema Allaahu ‘Akbar
na kuanza Tawaaf huku Al Kaabah ikiwa kushoto kwangu.
Siku
hii na umri huu na umati uliokuwepo sikuwa na ubavu wa kulifikia Hajarul aswad
na kulibusu kama alivyofanya Mtume Muhammad Swalla ‘Allaahu ‘alayhi wasallam
nikabaki kuliashiria tu ambayo pia inakubalika kisheria. Kila nikifika Ruknil
Yamani (kona ya Yemen kona ya tatu kabla ya kona ya hajarul aswad) nilitakiwa
kuomba dua’a aliyotufundisha Mtume Muhammad Swalla ‘Allaahu ‘alayhi Wasallam na
kusema: ` Rabbanaa aatinaa fiddunyaa hasanatan wafil akhirati hasanatan waqinaa
‘adhaaba Nnaar. (Mola wetu tupe katika dunia yaliyo mazuri na katika akhera
yaliyo mazuri na utuepushe na adhabu ya moto)
Umati
uliokuwepo ukifanya Tawaaf ukanikumbusha kwamba kwenye Baytul Ma’amuur,
mbinguni kuna umati kama huu wa Malaika nao ukifanya Tawaaf. Tofauti na umati
uliokuwepo baytul haraam na baytul ma’amuur ni kwamba umati wa baytul maa’muur
hufanya tawaaf mara moja katika uhai wao na hawarudi tena! Allaahu Akbar
Nikiendelea
kufanya Tawaaf kwa kuizunguka Al Ka’abah mara saba na kila nikifika eneo la
Hajarul aswad niliashiria na kusema Allaahu Akbar. Ilikuwa ni wakati wa
adhuhuri jua likiwa kali na tayari nimeshapata kufanya mwendo tokea Mina hadi
Jamaraat, Jamaraat hadi Aziziyah, Aziziyah hadi Al Ka’abah na sasa nikiendelea
na mwendo wenye kheri na Baraka wa Tawaaf, sikuhisi machofu ya aina yoyote.
Nilipofanya
Tawaaf na nikabahtika kuifanya kwenye Mataaf (sehemu ya chini ya kutufu karibu
na ‘Al Ka’abah) nilikuwa nnajiuliza inawezekana katika mojawapo ya sehemu
nimepita ni sehemu alipopita Mtume Swalla ‘Allaahu ‘alayhi wasallam alipofanya
Hijja yake kwa hivyo nimeweza kupata angalau Sunnah. Ila nitajuaje kama
nimeipatia?
Naam
kwenye Mataaf kuna msongamano, kuna mchanganyiko wa wanawake na wanaume lakini
yote haya hayakunijia katika mawazo yangu. Kilichokuwepo katika mawazo yangu ni
kupata fursa nadra ya kuwa karibu sana na Al ka’abah – nyumba ya kwanza
iliyoasisiwa kwa ajili ya Ibada. Allaahu Akbar! Kama ni unyenyekevu basi ukiwa
karibu na Al Ka’abah utaupata wa hali ya juu. Kama ni udhalili basi ukiwa
karibu na Al Ka’abah utaupata wa hali ya juu. Ni hisia ambazo haziwezi
kuelezeka mpaka uwepo mwenyewe karibu na nyumba ya Allaah ‘Azza wa Jall ndipo
utakapozifahamu hisia hizi. Kama bado hujafanya ibada ya Hijja ndugu yangu
katika Imani, jihimu na fanya haraka.
Nilipomaliza
kufanya Tawaaf ambayo ilinichukua takriban saa 1.15 nikatafuta sehemu nyuma ya
Maqaamu Ibrahim kwa ajili kusali Sunnah rakaa mbili, sikuipata kutokana na
zahma na msongamano. Nikatafuta sehemu tu na nikaswali rakaa mbili , rakaa ya
kwanza nilisoma Alhamdu na Qul Yaa ayyuhal Kaafirun na rakaa ya pili nilisoma
alhamdu na Qul huwa Llaahu ahad. Ndivyo alivyotufundisha Mtume wetu Swala
Allaahu ‘alayhi wasallam.
Baada
ya hapo nikaelekea sehemu yalipo maji ya zamzam, nikanywa kadri ya kiu yangu
huku kila nikinywa huomba du’aa. Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam
alituagiza tunapokunywa maji ya zamzam ni dawa ya maradhi na pia kujipangusa
katika sehemu za mwili.
Nilipomaliza
nilitakiwa kurudi tena na kulibusu Hajarul aswad lakini haikuwezekana kutokana
na msongamano nikabakia kuliashiria tu.
Bado
niko katika siku yangu ya tatu ya mafunzo na nilipomaliza funzo la Tawaaf nikaanza
funzo la Sa’iy.
Sa’iy ni kwenda matiti kati ya Jabal Swafaa na
Jabal Marwah. Milima hii imo ndani ya Msikiti ambako kumetengenezwa eneo maalum
la kjufanya ibada hii. Fundisho hili ni muhimu kwa ni mojawapo katika mambo
ambayo lazima niyafanye ili Hijja yangu ikamilike ni mojawapo ya nguzo za
Hijja.
Fundisho
hili lina mazingatio makubwa kwani linatukumbusha kisa cha mke wa Nabii
Ibrahiym ‘alayhis salaam alipomwacha mkewe bi Hajrah na mtoto mchanga Nabii
Ismaail ‘alayhis salaam kwenye jangwa lisilokuwa na chochote wakati huo. Na Bi
Hajrah alimuuliza Nabii Ibrahiym ‘alayhis salaam: “kwanini unatuacha hapa?” Nabii
Ibrahiym ‘alayhis salaam hakumjibu kitu mpaka alipomuuliza: “hivi ndivyo
alivyokuamrisha Mola wako?” Akajibu: “naam” basi Bi Hajra akasema: “Mola wetu
hatotuacha mkono”.
Ni
kisa kirefu ila fundisho muhimu ni pale Bi Hajrah alipoishiwa na maji na akawa
anatafuta kila upande akihaha huku na kule akienda katika ya Jabal Swafaa na
Marwah. Na kila akipita sehemu alipomwacha Ismaaiyl na kumsikia akilia
alizidisha mwendo kutafuta maji.
Naam
tunafanya Sa’iy kwa kumkumbuka mke wa Nabii Ibrahiym ‘alayhis salaam alipokuwa
akihangaika kutafuta, maji kwa ajili ya mwanawe.
Nikafika
Jabal Swafaa ambapo hutakiwa kuanzia na kumalizia Marwah. Nilipoweka mguu wangu
kwenye mlima Swafaa nikasoma aya Inna Swafaa walmarwata min sha’aairi Llaah,
faman hajjal bayta awi’itamara falaa junaah ‘alayhi an yatawwafa bihimaa, wamna
tattawa’a khayran, Fainna Llaah Shaakirun ‘aliym. (Suuratul Baqarah 158)
Nilipomaliza
nikasema kama alivyosema Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam – abdau bimaa
bada-a Llaahu bihi ( Ninaanza kwa kile ambacho Allaah alianzia)
Kisha
nikapanda Jabal Swafaa (ukitaka kulipata Jabal Swafaa itakubidi ufanye Sa’iy
chini na si kwenye ghorofa ya kwanza au ya pili) mpaka kufikia sehemu ambayo
ninaweza kuliona Al Ka’abah, nikaelekea qiblah na kisha nikaomba dua’a
aliyotufundisha Mtume Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam
Kisha
nikaanza kutembea kutoka Jabal Swafaa nikielekea Marwah ili kukamilisha
mzunguko mmoja.
Nilipofika
kwenye alama za taa za kijani (karibu na Jabal Swafaah) nikaongeza mwendo na
kwenda mwendo wa haraka (ni Sunnah kwa wanaume tu jambao ambalo pia hushangaza
kwani alietuletea utaratibu huu ni mwanamke , mke wa nabi Ibarhiym ‘alayhis
salaam) na zilipomalizika alama nikaendelea na mwendo wa kawaida hadi
nilipopanda Jabal Marwah nikasoma kama nilivyosoma nilipanza Jabal Swafaa na
kuendelea na sa’iy.
Nilikithirisha
kuomba du’aa na kumkumbuka Allaah ‘Azza wa Jall muda wote wa Sa’iy mpaka
nnamaliza.
Kila
nikijaribu kupata mazingatio katika Sa’iy naona tuna mengi ya kujifunza kwani
chimbuko la maji ya zamzam ni kutokana na Sa’iy aliyoifanya Bi Hajrah. Tukio
hili ambalo mamilioni ya waislamu duniani hulifanya kila mwaka ni limeanzia na
Bi Hajrah wakati alipokuwa akihangaika kwa ajili ya mwanaye mchanga. Kwanini
Nabii Ibrahiym ‘alayhis Salaam amuwache mkewe kwenye jangwa ambalo halina kitu
wala watu wala maji? Majibu ya masuala haya ndiyo hii nyumba ya mwanzo
iliyoasisiwa kwa Ibada. Allaahu Akbar.
Alhamdulillaah
nimemaliza fundisho muhimu la Hijja ambalo limehitaji kutumia mwendo wa miguu
kama ilivyokuwa Tawaaful Ifaadhah, kama ilivyokuwa safari yangu kutoka Mina
hadi Jamaraat, Jamaraat hadi Aziziyah, Aziziyah hadi Haram.
Naam
mwili sasa niliusikia kama umechoka na kipande cha kurudi Aziziyah nilipofikia
kilikuwa si kidogo kutembea kwa miguu na bado nitatakiwa kutembea tena usiku
kurudi Mina.
Niliamua
kuchukua Taxi na kurudi Aziziyah ambapo nilipofika kabla ya kupumzika
nilitekeleza fundisho jengine la Hijja la kunyoa nywele zote. Naam mara nyingi huwa sinyoi kipara, hupunguza
tu nywele zangu lakini ili Hijja yangu iwe na ubora niliamua kunyoa kwani Mtume
Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam aliwaombea du’aa mara tatu walionyoa na mara
moja waliopunguza.
Baada
ya kumaliza kunyoa sasa nimetahallal kikamilifu yaani yale mambo yote
niliyokatazwa wakati nipo katika Ihraam sasa nimeruhusiwa mpaka kustarehe na
mke .
Natumai
uliebahatika kusoma waraka huu utaweza kufaidika japo kidogo hasa kwa
kuzingatia ibra – mazingatio yanayopatikana katika Ibada ya Hijja na Umrah na
Allaah atuwafikishe katika kila lililokuwa na kheri kwetu.
Aamiyn
Allah amlipe katika mizani ya kheri kwa simulizi hii ambayo ina manufaa si kwake tu, bali pia kwa wale wote wataojaaliwa kuusoma, kuuzingatia na kuchambua yale aliyoyaainisha kuwa ni mafundisho.
ReplyDelete