Habari za Punde

Hakuna Mkulima anayekopwa Karafuu na ZSTC.

Na Pili Khatib na Zuhura Omar, MUM
​Mkurugenzi Mwendeshaji wa ZSTC Mwanahija Almas Ali

Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Biashara la Taifa Zanzibar (ZSTC) Bi. Mwanahija Almas Ali amekanusha uzushi unaodai kuwa Shirika la ZSTC limeishiwa fedha za kununulia karafuu na kuwakopa Wakulima karafuu zao.
Akizungumza na Wandishi wa Habari Makao makuu ya Shirika Maisara Zanzibar, Bi. Mwanahija alisema pamoja na kuongezeka kwa manunuzi yanayotokana na kuongezeka kwa uzalishaji katika msimu wa 2015/2016 Shirika linapesa za kutosha za kununulia karafuu zote katika msimu mzima na hakuna Mkulima yoyote aliyekopwa.

Alisema Shirika tangu kuanzishwa kwake mwaka 1968 halijawahi kuwakopa Wakulima na amesema kuwa madai hayo ni uzushi usiokuwa na ukweli wowote.

Alisema ZSTC ni Shirika la Serikali hivyo kama likipungukiwa na fedha za manunuzi ya karafuu Serikali ina uwezo wa kulipa fedha za kutosha zinazihitajika na sio kuwakopa Wakulima.

Amesema hakuna Mkulima aliyekopwa na wala hakuna shida ya kukopa kutoka taasisi za kifedha kwa vile Shirika limeshajipanga vizuri kununua karafuu zote kutoka kwa Wakulima kwa fedha taslimu.

 Aliwataka Wakulima wa zao la karafuu kutokuwa na wasi wasi wowote juu ya manunuzi ya karafuu zao na amewataka kuendelea kushirikiana na Shirika katika kulihudumia zao vizuri.
Aidha Bi. Mwanahija alifahamisha kuwa manunuzi yameongezeka mwaka huu wa 2015/2016 kinyume na ilivyokadiriwa awali kutokana na hali ya hewa kubadilisha msimu wa mwaka kuwa msimu wa vuli ambao huwa ni msimu mkubwa.
Sababu nyengine aliitaja kuwa ni uzazi wa mikarafuu midogo iliyopandwa kati ya mwaka 2005 hadi 2013 ambapo mikarafuu hiyo tayari imeanza kuzaa vizuri na kuongeza uzalishaji.
Pia alisema kuanzishwa kwa Mfuko wa Maendeleo ya Karafuu imekuwa ni hatua nyengine muhimu ya kuongezeka kwa uzalishaji wa zao la karafuu kutokana na kazi nzuri zinazofanywa na mfuko huo za kushajihisha Wakulima kuimarisha zao hilo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.