Habari za Punde

Dk Shein Ziarani Kisiwani Pemba

 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba                                                     
                                                                              6.1.2016
---
RAIS wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amekagua maendeleo ya mradi wa huduma za mazingira na usafi wa miji Zanzibar (ZUSP) iliyopo Pemba na kueleza kuwa hatua hizo ni miongoni mwa utekelezaji wa ahadi alizowaahidi wananchi mwaka 2010 za kuimarisha miji mikuu ya Unguja na Pemba.

Dk. Shein alisema kuwa hatua za utekelezaji wa mradi huo ni miongoni mwa juhudi za kuimarisha miji hiyo kwa lengo la kuifanya kuwa ya kisasa hasa ikizingatiwa kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekopa fedha nyingi kutoka Benki ya dunia kwa ajili ya mradi huo.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali ilikopa kutoka Benki ya Dunia jumla ya Dola milioni 38 sawa na Tsh. Bilioni 56 kwa hesabu za fedha za mwaka 2011 kutekeleza mradi huo ambapo kwa upande wa Pemba utafanyika katika miji ya Wete, Chake na Mkoani.

Akizungumza na wananchi kwa nyakati tofauti mara baada ya kutembelea maeneo ya miradi hiyo huko Mkoani na Chake Chake Pemba, Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar anayoiongoza yeye itaendelea kufanya kazi zake za kuwapelekea wananchi huduma muhimu za maendeleo.

Dk. Shein aliwaeleza wananchi kuwa mradi huo kwa upande wa Unguja unahusisha uimarishaji wa Mji Mkongwe pamoja na Ngambo kwa kuweka taa za jua za barabarani kuelekea uwanja wa ndege, Amani na sehemu nyengine za mji hatua ambayo itauweka mji katika mazingira mazuri pamoja na kuupamba.

Ujenzi huko pia, utahusisha ujenzi wa ukuta wa Forodhani pamoja na ujenzi wa barabara mbili katika eneo hilo ambapo tayari ukuta wa bahari umeanza kujengwa.

Katika maelezo yake, Dk. Shein aliwaeleza wananchi kuwa mkopo huo si ruzuku wala msaada na fedha hizo ni nyingi hivyo wananchi wanatakiwa kushirikiana na serikali yao kwa kuhakikisha kuwa inatunzwa na inaendelezwa huku wakitambua kuwa kila mmoja anachangia kwa njia tofauti katika mkopo huo.

Aidha, Dk. Shein alisema kuwa mradi huo pia, unahusisha kuyatoa maji ya mvua na bahari katika maeneo ya viwanja vya Mnazi Mmoja, ujenzi wa misingi mikubwa ya kutoa maji katika maeneo ya Mpendae kwa Biti Amrani na Sebleni.

Mapema Mkurugenzi wa Baraza la Mji wa Mkoani Issa Juma Othman alimueleza Dk. Shein kuwa kwa upande wa Mji wa Mkoani, mradi huo unahusisha maeneo makubwa matatu ambayo yanajumuisha ukarabati mkubwa wa Ofisi ya Baraza la Mji Mkoani, Ujenzi wa njia za vidaraja katika eneo la mji wa Mkoani pamoja na ujenzi wa mitaro ya maji katika maeneo ya Mji wa Mkoani.

Mkurugenzi huyo alisema kuwa miradi hiyo mitatu inatarajiwa kugharimu jumla ya Tshs. Milioni 755 huku akieleza kuwa miradi hiyo inatekelezwa kwa kipindi cha mwaka mmoja kutoka tarehe 01 April,2015 na kutarajiwa kukamilika mwezi April mwaka huu.

Alieleza kuwa  mradi wa ujenzi wa vidaraja katika Mji wa Mkoani unahusisha ujenzi na ukarabati wa njia za vidaraja 17 ambapo tano kati ya hizo ni ukababati na 12 ni ujenzi mpya.

Nae mwakilishi wa Kampuni ya ZECCON COMPANY LTD Ali Mbarouk alieleza kuwa gharama za miradi hiyo kwa upande wa mji wa Mkoani imeongezeka kutoka Tshs 755 hadi Tshs. Bilioni 1 kutokana na marekebisho mbalimbali ya lazima yaliyofanywa kqtika miradi hiyo..

Akiwa katika mji wa Chake Chake, Dk. Shein alitemebela ujenzi wa vidaraja huko Chachani-Minazini pamoja na kuangalia ujenzi wa jengo la Ofisi ya Baraza la Mji Chake ambalo ni la ghorofa mbili huku akisisitiza ujenzi wa ofisi hizo uzingatie watu wenye ulemavu wa miguu pamoja na wazee.

Wakati huo huo, mara baada ya kuzungumza na wananchi Dk. Shein alielekea huko Kisiwani Wesha kwa ajili ya kuangalia ujenzi wa chinjio jipya la Ng’ombe la Baraza la Mji Chake na kupata maelezo juu ya chinjio hilo ambalo hadi kumalizika ujenzi wake litagharimu Tshs milioni 166.

Chinjio hilo linalojengwa na Kampuni ya NOWE INVESTMENT LMT ya Dar-es-Salaam ambapo hadi sasa ujenzi wake umeshafikia asilimi 90 linatarajiwa kukamilika mwezi April mwaka huu.

Dk. Shein yuko kisiwani Pemba kwa ziara ya kiserikali ikiwemo kuangalia miradi ya maendeleo pamoja na kuzindua miradi mbali mbali iliyomo katika ratiba ya shamrashamra za sherehe za miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.