Habari za Punde

Balozi Seif Atembelea Uwanja wa Amani Kuangalia Matayarisho ya Maandalizi ya Kumuapisha Rais Mteule wa Zanzibar Dk Shein.

Mwenyekiti wa Kamati ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa Balozi Seif Ali Iddi akiongoza Kikao cha Kamati hiyo kwenye ukumbi wa Watu mashuhuri { VIP } uliopo Uwanja wa Amaan.
Wajumbe wa Kamati ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa wakitafakari  na kujaribu kujadili changamoto zilizojitokeza wakati wa matayarisho ya mwisho wa sherehe za kuapishwa kwa Rais Mteule wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohammed Shein.
Vikosi vya ulinzi na usalama vikimaliza matayarisho ya mwisho ya sherehe za kuapishwa  kwa Rais Mteule wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi hapo uwanjwa wa Michezo Amaan Mjini Zanzibar.
Jukwaa maalum  la kuapishwa kwa Rais Mteule wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohammed Shein limeshakamilika matayarisho yake kwa ajili ya kazi hiyo.
Vikosi vya Ulinzi vikiwa katika hatua za mwisho za matayarisho ya upambaji uwanja wa Amaan wakitandika Zulia jekundu litakalopamba sherehe  za kuapishwa kwa Rais Mteule wa Zanzibar. Mjumbe wa Kamati ya sherehe na maadhimisho ya Kitaifa Kanal Shaaban Lissu akiwa makini kusimamia na kuhakikisha kazi hiyo  inakwenda kwa mujibu ilivyopangwa.
Vikosi vya Ulinzi vikiwa katika hatua za mwisho za matayarisho ya upambaji uwanja wa Amaan wakitandika Zulia jekundu litakalopamba sherehe  za kuapishwa kwa Rais Mteule wa Zanzibar. Mjumbe wa Kamati ya sherehe na maadhimisho ya Kitaifa Kanal Shaaban Lissu akiwa makini kusimamia na kuhakikisha kazi hiyo  inakwenda kwa mujibu ilivyopangwa.


Na Othman Khamis OMPR.
Jaji Mkuu wa Zanzibar Mh. Omar Othman Makungu anatarajiwa kumuapisha  Rais Mteule wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohammed Shein  Alhamis ya Tarehe 24 mwezi huu baada ya kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa marejeo uliofanyika Jumapili iliyopita.

Dr. Ali Mohammed Shein  wa Chama cha Mapinduzi { CCM } alishinda uchaguzi baada ya kupata kura Laki 299,982 sawa na asilimia  91.4% ya kura zote zilizopigwa kwenye uchaguzi huo.

Matayarisho kwa ajili ya sherehe hizo za uapishwaji zitakazofanyika katika uwanja wa michezo wa Amani Mjini Zanzibar  yamekamilika rasmi ambapo Vikosi vya ulinza na usalama vya SMT na SMZ vimeshajiandaa  kwa kuzipamba sherehe hizo.

Mwenyekiti wa Kamati ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa ambae pia ni Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiwa pamoja na Makamanda wa Vikosi hivyo  na baadhi ya watendaji wakuu wa Serikali alipata wasaa wa kuangalia mazoezi ya mwisho ya wapiganaji hao.

Sherehe hizo zitapambwa na Vikosi vya Jeshi la Wananchi wa Tanzania {JWTZ }, Polisi, Kikosi cha Kuzuia Magendo {KMKM }, Mafunzo, Jeshi la Kujenga Uchumi { JKU , Valantia { KVZ }na Kikosi cha Zimamoto na Uokozi { KZU }.   

Viongozi wa Dini tofauti watakaoambatana na Jaji Mkuu wa Zanzibar  katika sherehe hizo za uapishwaji wanatarajiwa kutoa Dua kwa nia ya kumtakia Uongozi Mwema Rais atakaeapishwa pamoja na Zanzibar kwa ujumla.

Baadaye Wajumbe wa Kamati ya sherehe za Maadhimisho ya Kitaifa  walipata fursa ya kukutana ili kukamilisha changamoto zilizojitokeza kwenye matayarisho ya Sherehe hizo hapo katika Ukumbi wa Watu Mashuhuri {VIP } ya uwanja wa  Aman.

Asilimia kubwa ya Wajumbe hao wameonyesha kuridhika kwao  hatua iliyofikiwa ya  maandalizi hayo wakitarajia mafanikio makubwa ya sherehe hizo katika Historia za chaguzi za vyama vingi hapa Zanzibar.

Akizungumza na vyombo vya habari nje ya Uwanja wa michezo wa Amani   baada ya kukamilika kwa maandalizi ya Sherehe hizo Mwenyekiti wa Kamati ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa  Balozi Seif Ali Iddi aliwahimiza Wananchi kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye sherehe hizo.

Balozi Seif alisema utaratibu maalum umeandaliwa kupitia kwa Makatibu Tawala wa Mikoa na Wilaya zote wa jinsi wananchi watakavyoingia kwenye uwanja kushuhudia sherehe hizo.

Aliwaasa wananchi wote kuelewa kwamba uchaguzi umekwisha  na lililobakia kwa wakati huu ni kuhakikisha kila mwananchi anaelekeza nguvu zake katika ujenzi wa Taifa hata kwenye kazi za amali ambazo kwa namna moja au nyengine zinasaidia uchumi wa Nchi.

Katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984 Kifungu cha 31 {1} inaelewa wazi kwamba Mtu anayechukuwa madaraka ya Urais, kabla ya kuanza wadhifa huo,atakula kiapo cha uaminifu na kiapo cha kazi kama kitakavyowekwa na Baraza la Wawakilishi lakini kwa hali yoyote itabidi ashike madaraka hayo kabla ya kupita siku saba baada ya kuchaguliwa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.