Habari za Punde

Dk Shein, akisoma Risala ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein akitoa Risala ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhan kwa Wananchi na Waislamu wote nchini katika Risala hiyo amewataka Wananchi kuwa Amani na Utulivu na kuwaombea kwa Mola wetu kuwajaalia Rehma na baraka za Mwezi Mtukufu wa Ramadhan pia amewataka kufanya ibada kwa wingi katika kipindi chote cha mwezi huu,(Picha na Ikulu.)06/06/2016



STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                          6.6.2016
---
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar itaongeza juhudi za kuwafuatilia wafanyabiashara wenye tabia ya kupandisha bei za bidhaa bila ya sababu za msingi, jambo ambalo linaathiri hatua ya Serikali kutoa unafuu wa ushuru wa bidhaa muhimu kwa wafanyabiashara hao hapa nchini.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo, Ikulu mjini Zanzibar katika risala aliyoitoa kwa wananchi kupitia vyombo vya habari katika kuukaribisha Mwezi mtukufu wa Ramadhani mwaka huu.

Katika risala hiyo, Alhaj Dk. Shein alisema kuwa inasikitisha kuona kuwa, licha ya kuwa Uislamu unahimiza kuoneana huruma, lakini wapo wafanyabiashara ambao huchukua fursa ya kupandisha bei bidhaa zao katika mwezi wa Ramadhani, hasa zile bidhaa za chakula muhimu ambazo Serikali hupunguza ushuru ili kuwapa nafuu wananchi.

“Nafahamu malalamiko yaliopo hivi sasa, ambapo wafanyabiashara walipandisha bei za bidhaa kwa kisingizo cha uchaguzi na hadi hii leo bei za bidhaa hizo bado ziko juu”,alisema Alhaj Dk. Shein.

Aidha, Alhaj Dk. Shein alisema kuwa upandishaji wa bei usio na msingi unakwenda kinyume na malengo ya Serikali ya kuanzishwa kwa biashara huru yenye ushindani.

Hata hiyo, Alhaj Dk. Shein alisisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na wafanyabiashara na itahakikisha kuwa bidhaa zote muhimu zinazohitajika na kutumika zaidi katika mwezi wa Ramadhani zinapatikana wakati wote na bila ya usumbufu wowote.

Kwa vile mwezi wa Ramadhani ndio Qur-ani iliteremshwa kwa Mtume Muhammad (SAW), Alhaj Dk. Shein alieleza kuwa bidii inahitajika katika kuisoma na kuifahamu Qur-an sambamba na kuhimizana katika kuzitekeleza Sala za Fardhi na Sala za Sunna mbali mbali hasa nyakati za usiku.

Alhaj Dk. Shein alisisitiza wajibu wa kuishi kwa kumfanya Mtume Muhammad (S.A.W) kuwa mfano katika kutekeleza ibada mbali mbali katika mwezi wa Ramadhani ikiwemo kutoa sadaka, bidii ya kumtaja Allah, kufanya istighfari, kukaa Itikafu, kuharakisha kufungua wakati unapofika pamoja na kutekeleza sunna ya kula daku.

Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein alieleza kuwa ni muhimu ikafahamika kwamba hivi sasa teknolojia imevisogeza vishawishi vingi vinavyoweza kuibatilisha saumu karibu na nafsi ambapo miongoni mwa vishawishi hivyo ni pamoja na mitandao ya simu na intaneti.

Alisema kuwa bila ya kujijua, mtu anaweza kujikuta anafanya makosa pale anapoangalia mitandao yenye mambo yasiopendeza, hasa katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Hivyo, Alhaj Dk. Shein alitoa wito kwa Mashekhe kuendelea kutoa taaluma juu ya umuhimu wa matumizi bora ya mitandao na kwa pamoja kuhimizana juu ya umuhimu wa kuunga mkono juhudi za Serikali za kushajihisha matumizi bora ya mitandao ya simu na kompyuta kwa matumizi ya mitandao ya intaneti.

Alisema Serikali itaendelea kuchukua tahadhari na hatua mbali mbali kama ilivyotangazwa na Wizara ya Afya  katika kujikinga na maradhi ya miripiko licha ya kuwa uamuzi huo unaweza kuathiri utamaduni wa kufutarishana unaoandaliwa na wananchi, taasisi za Serikali na binafsi katika kipindi cha Ramadhani.

Katika risala hiyo, Alhaj Dk. Shein aliiagiza Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira pamoja na Mamlaka ya Maji ya Zanzibar (ZAWA) zifanye kila jitihada ili iwapatie wananchi maji safi na salama, kwa kutumia magari katika sehemu zote ambazo zina upungufu  wa maji safi na salama.

Alhaj Dk. Shein alimtaka Mkurugenzi Mkuu wa ZAWA kuhakikisha kwamba kazi hiyo ya kuwapatia wananchi maji inafanyika kwa mafanikio makubwa na kutoa wito kwa wananchi kushirikiana na Mamlaka hiyo ili kufanikisha shughuli hiyo.

Sambamba na hayo, Alhaj Dk. Shein  aliwataka wananchi kufuata mafundisho ya Qur-an na Hadithi za Mtume Muhammad (S.A.W) katika kuhakikisha kuwa wanafanya vitendo vyema, wanaimarisha mapenzi na wanaepuka chuki na hasama miongoni mwao.

“Ni wajibu wetu kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza kwa kuiweka nchi yetu katika hali ya amani na salama na sote tunafahamu kuwa sisi ni wamoja na kwa hivyo, chuki na husda hazina tija wala hazina nafasi katika kuijenga Zanzibar ya leo”,alisisitiza Alhaj Dk. Shein.

Alhaj Dk. Shein aliwahakikishia wananchi kuwa Serikali zote mbili Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, zitaendelea kuhakikisha kuwa nchi inaendelea kuwa ya amani na salama.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.