Habari za Punde

Dk Shein Azindua Kamati ya Kuchangia Madawati Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                          18.07.2016

---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameizindua rasmin Kamati ya Rais ya Kukusanya fedha kwa ajili ya ununuzi wa madawati kwa skuli za Msingi na Sekondari za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar huku akiahidi kuwa Serikali itakuwa bega kwa bega na Kamati hiyo katika kuhakikisha lengo hilo linafikiwa.

Dk. Shein aliyasema hayo leo huko Ikulu ndogo Kibweni katika hafla fupi ya kuizindua Kamati hiyo ambayo itafanya kazi kwa lengo la kulitafutia ufumbuzi tatizo la uhaba wa madawati katika skuli za Sekondari na Msingi za Unguja na Pemba.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa anamatumaini makubwa kuwa Kamati hiyo chini ya Mwenyekiti wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora Haroun Ali Suleiman itapata mafanikio na kufikia lengo lililokusudiwa kutokana na uzoefu na uhodari wa wajumbe wake.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itakuwa bega kwa bega katika kushirikiana na Kamati hiyo ili lengo lililokusudiwa liweze kufikiwa kwani tatizo hilo ni la Jamii nzima ya Zanzibar.

Kutokana na hali hiyo, Dk. Shein alisisitiza kuwa Serikali itachukua juhudi za makusudi kwa mashirikiano na Kamati hiyo katika kuhakikisha lengo hilo linafikiwa kama ilivyofanya katika kulitafutia ufumbuzi suala la usafiri wa baharini na hatimae Serikali ikanunua meli yake mpya ya MV Mapinduzi II.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa anaelewa kuwa kazi hiyo ni ngumu lakini anaamini kutokana na uzoefu, weledi na uhodari wa Wajumbe wa Kamati hiyo kwa mashirikiano ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mafanikio yatapatikana kwani tayari Serikali imeshawasilisha rasimu ya uchangiaji na upatikanaji wa madawati katika skuli za  Serikali za Unguja na Pemba.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi  ambapo mara tu baada ya uwasilishaji wa rasimu hiyo Katika Kikao cha Baraza la Wawakilishi baadhi ya wajumbe walianza kutoa michango yao kwa ajili ya ununuzi wa madawati hayo.

Nae Mwakilishi wa Jimbo la Uzini Mohammed Raza ambaye pia ni  Mjumbe wa Kamati hiyo kwa niaba ya Wanakamati wenziwe alieleza azma na nia sambamba na lengo la Kamati hiyo ni kuhakikikisha tatizo la uhaba wa madawati katika skuli za Zanzibar linapatiwa ufumbuzi.

Katika maelezo yake Raza alitoa shukurani za dhati kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa juhudi zake na maarifa katika kuwatumikia wananchi wa Zanzibar wakiwemo wanafunzi katika kuhakikisha wanapatiwa madawati ili sekta ya elimu izidi kuimarika hapa nchini.

Raza alisema kuwa nia na malengo ya Kamati hiyo ni kulitafutia ufumbuzi tatizo hilo kwa mashirikiano ya pamoja ikiwa pia ni miongoni mwa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM katika kuimarisha sekta ya elimu hapa nchini.

Pamoja na hayo,  Raza alisisitiza suala la uangalifu katika manunuzi sambamba na umazubuti wa madawati hayo ili yaweze kudumu kwa muda mrefu na kujenga heshima kwa kufahamika kwa matumizi ya fedha zote zilizochangwa.

Nae Mwenyekiti wa Kamati hiyo ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Makunduzi Haroun Ali Suleiman alimueleza Rais Dk. Shein hatua za awali zilizoanza kuchukuliwa na Kamati hiyo ikiwa ni pamoja na kukutana na uongozi wa Wizara husika ya Elimu katika kulipangia mikakati suala hilo.

Aidha, Waziri Haroun aliahidi kuwa nia na malengo ya Kamati hiyo itafikiwa katika kulitafutia ufumbuzi suala hilo kwa mashirikiano ya pamoja.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.