Habari za Punde

TBA Watakiwa Kukamilisha Miradi ya Ujenzi kwa Wakati

Na.Benjamin Sawe   
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amemtaka Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kuhakikisha wanakamilisha haraka miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi wa umma zinazojengwa nchini kote.

Ameyasema hayo mara baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa nyumba za watumishi 851 zilizopo eneo la Bunju "B" ambazo zipo katika mpango wa Wakala wa kujenga nyumba 10,000 kwa ajili ya watumishi wa umma na kuona hatua zilizofikiwa.

Waziri Mbarawa amesema kukamilika kwa ujenzi huo kutawawezesha watumishi wa umma kupata makazi yaliyobora na ya uhakika na hivyo kuiwezesha tba kujipatia marejesho ya fedha walizowekeza kwa wakati.

"Bora mjenge nyumba kidogo lakini zinamalizika kuliko kujenga nyumba nyingi kwa wakati mmoja lakini hazimaliziki", amesema  Prof. Mbarawa.

Prof. Mbarawa amewatala TBA kuhakikisha wanamaliza ujenzi wa miradi ya nyumba na majengo kwa wakati na kuziuza ili kupata faida itayowawezesha kujenga nyumba nyingine badala ya kuwa na miradi mingi ya ujenzi ambayo haijakamilika.

Ameitaka TBA kubadilika kimtazamo na kiutaalamu kuanzia watendaji hadi wafanyakazi wake na kuanza kufanya kazi kwa malengo ili kuwezesha kukabiliana na ushindani wa kibiashara wa majengo hapa nchini.

Katika hatua nyingine Waziri Prof. Mbarawa amekagua mradi wa ujenzi wa mabweni ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam uliopo barabara ya Sam Nujoma ambapo ameridhishwa na kasi ya maendeleo ya mradi huo.

Amewataka wakala huo kuhakikisha wanakamilisha kwa wakati na kwa kuzingatia viwango na ubora vilivyowekwa ili kuweza kuondoa changamoto ya makazi inayowakabili wanafunzi hao.

Kwa upande wake Meneja Miradi wa TBA Arch. Humphrey Killo amesema ujenzi wa mradi wa mabweni ya wanafunzi utahusisha ujenzi wa vyumba 960 vyenye uwezo wa kuchukua jumla ya wanafunzi 3,840 na ujenzi huo utakamilika ndani ya miezi sita.

Naye Mtendaji Mkuu wa TBA Arch. Elius Mwakalinga amemhakikishia waziri kuwa wakala wake utafanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha kwa wakati mradi huo kwa kuwa inayo uwezo wa kiteknolojia wa ujenzi wa miradi ya majengo hapa nchini.

"Kuonyesha kuwa uwezo wa kufanya miradi kama hiyo tunayo, tutaikamilisha kwa wakati na viwango stahili ili wateja wapate thamani ya pesa watakayolipa", amesema Arch. Mwakalinga.

Zaidi ya nyumba 10,000  za makazi ya watumishi wa umma zinatarajiwa kujengwa na kuuzwa katika mradi wa Bunju "B" ikiwa ni mkakaati wa Serikali kuwawezesha watumishi wa umma kupata nyumba bora kwa bei nafuu.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.