Na.Benjamin Sawe
Waziri
wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa amemtaka Mtendaji
Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) kuhakikisha wanakamilisha haraka
miradi ya ujenzi wa nyumba za watumishi wa umma zinazojengwa nchini kote.
Ameyasema
hayo mara baada ya kukagua mradi wa ujenzi wa nyumba za watumishi 851 zilizopo
eneo la Bunju "B" ambazo zipo katika mpango wa Wakala wa kujenga
nyumba 10,000 kwa ajili ya watumishi wa umma na kuona hatua zilizofikiwa.
Waziri
Mbarawa amesema kukamilika kwa ujenzi huo kutawawezesha watumishi wa umma
kupata makazi yaliyobora na ya uhakika na hivyo kuiwezesha tba kujipatia
marejesho ya fedha walizowekeza kwa wakati.
"Bora
mjenge nyumba kidogo lakini zinamalizika kuliko kujenga nyumba nyingi kwa
wakati mmoja lakini hazimaliziki", amesema Prof. Mbarawa.
Prof.
Mbarawa amewatala TBA kuhakikisha wanamaliza ujenzi wa miradi ya nyumba na
majengo kwa wakati na kuziuza ili kupata faida itayowawezesha kujenga nyumba
nyingine badala ya kuwa na miradi mingi ya ujenzi ambayo haijakamilika.
Ameitaka
TBA kubadilika kimtazamo na kiutaalamu kuanzia watendaji hadi wafanyakazi wake
na kuanza kufanya kazi kwa malengo ili kuwezesha kukabiliana na ushindani wa
kibiashara wa majengo hapa nchini.
Katika
hatua nyingine Waziri Prof. Mbarawa amekagua mradi wa ujenzi wa mabweni ya
wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam uliopo barabara ya Sam Nujoma ambapo
ameridhishwa na kasi ya maendeleo ya mradi huo.
Amewataka
wakala huo kuhakikisha wanakamilisha kwa wakati na kwa kuzingatia viwango na
ubora vilivyowekwa ili kuweza kuondoa changamoto ya makazi inayowakabili
wanafunzi hao.
Kwa
upande wake Meneja Miradi wa TBA Arch. Humphrey Killo amesema ujenzi wa mradi
wa mabweni ya wanafunzi utahusisha ujenzi wa vyumba 960 vyenye uwezo wa
kuchukua jumla ya wanafunzi 3,840 na ujenzi huo utakamilika ndani ya miezi
sita.
Naye
Mtendaji Mkuu wa TBA Arch. Elius Mwakalinga amemhakikishia waziri kuwa wakala
wake utafanya kazi usiku na mchana ili kukamilisha kwa wakati mradi huo kwa
kuwa inayo uwezo wa kiteknolojia wa ujenzi wa miradi ya majengo hapa nchini.
"Kuonyesha
kuwa uwezo wa kufanya miradi kama hiyo tunayo, tutaikamilisha kwa wakati na
viwango stahili ili wateja wapate thamani ya pesa watakayolipa", amesema
Arch. Mwakalinga.
Zaidi
ya nyumba 10,000 za makazi ya watumishi wa umma zinatarajiwa kujengwa na
kuuzwa katika mradi wa Bunju "B" ikiwa ni mkakaati wa Serikali
kuwawezesha watumishi wa umma kupata nyumba bora kwa bei nafuu.
Imetolewa
na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano.
No comments:
Post a Comment