Habari za Punde

Dk Shein Azungumza na Viongozi wa Wizara ya Ardhi Maji Nisharti na Mazingira Ikulu.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                         6.09.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza haja kwa uongozi wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira kuwafuata wananchi katika maeneo yao wanayoishi ili kutambua mahitaji yao katika upatikanaji wa huduma muhimu zilizopo katika Wizara hiyo.

Dk. Shein alieleza kuwa iwapo viongozi wa Wizara hiyo watakwenda katika maeneo wanayoishi wananchi wataweza kufanya kazi zao kwa ufanisi zaidi na kuwataka kutokaa maofisini na badala yake wawafuate wananchi katika maeneo yao kwani Serikali imo katika kutekeleza jukumu lake la kuwahudumia wananchi wote wa Zanzibar popote pale walipo.

Dk. Shein aliyasema hayo wakati  alipokutana na uongozi wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira wakati ukitoa taarifa ya Utekelezaji wa Programu ya Utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi pamoja na ahadi za Rais kwa muda wa miaka mitano (2015-2020) huko Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisisitiza juu ya uwajibikaji kwa viongozi hao katika kutekeleza majukumu yao ili kuwahudumia wananchi ipasavyo sambamba na kutambua vyema majukumu yao katika maeneno yao ya kazi.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa viongozi na watendaji wa Wizara hiyo katika kutekeleza ipasavyo majukumu yao katika kutoa huduma kwa wananchi hali ambayo imepelekea huduma hizo kuimarika zaidi Unguja na Pemba.

Aidha, Dk. Shein aliwataka viongozi hao kutotumia muda wao mwingi kukaa maofisini na badala yake waende kwa wananchi ili kutafuta changamoto zinazowakabili katika kupata huduma zitokanazo na Wizara hiyo.

Nao uongozi huo kwa upande wake ulieleza juhudi inazozichukua katika kutekeleza majukumu yake ikiwa ni pamoja na mafanikio makubwa iliyoyapata katika kuwapelekea huduma bora na muhimu wananchi zikiwemo huduma za maji na umeme.

Katika maelezo yao viongozi hao walieleza kuwa tayari Shehia zote za Unguja na Pemba zimeshafikishiwa huduma za umeme na hivi sasa zimebaki Shehia mbili tu ambazo ni Fundo na Minazini zilizopo Kiswani Pemba ambazo nazo hivi sasa zimo katika mchakatoya kupelekewa huduma hiyo.

Aidha, uongozi huo ulieleza kuwa kwa upande wa visiwa vidogo vidogo tayari vyote vimeshapelekewa huduma ya umeme na kisiwa kilichobaki ni kiswa cha Fundo na visiwa vidogo vya Uvinje, Okota na Njao ambavyo navyo vitapata huduma hiyo katika kipindi kifupi kijacho.

Katika programu hiyo ya Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 uongozi huo ulieleza kuwa umo katika jitihasda za kupunguza migogogro ya ardhi kwa kuimarisha huduma za mahakama za ardhi katika mikoa yote ya Unguja na Pemba.

Pamoja na hayo, uongozi huo ulieleza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa katikan kuandaa Sera na Sheria ya Mafuta na Gesi Asilia ikiwa ni pamoja na jitihada za kuwajengea uwezo watendaji pamoja na kuhamasisha vijana kujiunga na masomo ya fani ya Mafuta na Gesi Asilia.

Kwa upande wa suala zima la mazingira uongozi huo ulieleza kuwa hatua inazozichukua katika kusimamia Sera na Sheria ya Mazingira pamoja na ushirikishwaji wa jamii katuika utunzaji wa Uhifadhi wa Mazingira kwenye maeneo yao ikiwa ni pamoja na kusimamia mabadiliko ya tabianchi na elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa utunzaji wa mazingira.

Wakati huo huo, Dk. Shein alikutana na uongozi wa Wizara ya Biashara, Wiwanda na Masoko hapo Ikulu mjini Zanzibar kwa lengo hilo hilo la kutoa taarifa ya Utekelezaji wa Programu ya Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 iliyotolewa na Wizara hiyo.

Katika taarifa yake Wizara hiyo ilieleza kuwa majukumu yake makubwa ni kusimamia na kuendeleza sekta ya biashara na sekta ya viwanda hapa Zanzibar.

Aidha, uongozi huo ulieleza kuwa Wizara hiyo inatekeleza malengo hayo ambayo kwa ujumla yanajielekeza katika malengo makuu ya Mkakati wa Kukuza Uchumi Zanzibar pamoja na kuweza Mazingira ya Ukuaji Uchumi, Kujenga Uchumi Endelevu na mpana ili kuondoa umasikini pamoja na kujenga sekta binafsi iliyo imara kwa lengo hilo la kukuza uchumi.

Nae Dk. Shein kwa upande wake aliwataka viongozi na watendaji wa Wizara hiyo kufanya kazi kwa mashirikiano zaidi katika kuhakikisha malengo yaliokusudiwa yanafikiwa huku akipongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Wizara hiyo katika kuimarisha sekta zake.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliendelea kusisitiza suala zima la uwajibikaji kwa viongozi na watendaji wa Wizara hiyo sambamba na kuzitafutia ufunmbuzi changamoto zilizopo kwa lengo la kuendelea kupata mafanikio zaidi katika sekta za biashara, viwanda na masoko ili kuendelea kukuza na kuimarisha uchumi wa Zanzibar.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.