Habari za Punde

Kumbukumbu ya Hijja na athari zake -1

Alhamdulillaah, nilibahatika kuwa miongoni mwa waliojaaliwa kuitekeleza Ibada ya Hajj mwaka 1435 - 2014

Nilikuwa kwenye mafunzo ya kivitendo ya siku sita kuanzia tarehe 8  Dhulhijjah - mfunguo tatu mpaka tarehe 13 Dhulhijjah 1435.

Kwa wale watakaombatana na safari yangu hii ni kwamba Hijja ni ibada ambayo hufanyika katika mji wa Makkah, Saudi Arabia ni matendo maalum, yanayofanyika katika wakati maalum, sehemu maalum na kwa ajili ya watu maalum. Ni nguzo ya tano katika nguzo za kiislamu ambayo humuwajibikia kila Muislamu mwenye uwezo mara moja katika maisha yake.

Naam ni siku sita tu lakini nimeweza kujifahamu na kujitambua katika kipindi cha siku sita ambazo zitabakia katika kumbukumbu ya maisha yangu. Kwani mafunzo yake ya kinadharia, kivitendo na kiroho ni mafundisho nadra unayoweza kuweza kuyapata kwa kipindi kifupi na yakaweza kuleta athari kubwa katika maisha ya Muislamu.

Nikikumbuka kwa mara ya pili nilipoivaa Ihraam siku ya Tarwiyah, tarehe 8 Dhulhijjah na kutia nia ya Hajj na kuanza Talbiyah “Labbayka Allaahumma Labbayka Labbayka Laa shariyka laka Labbayka Innal hamda Wanni’imata laka walmulk Laa shariyka laka”. Sikujikuta peke yangu, kila ninaemkuta njiani anatamka Talbiyah kama mimi. Kila ninaemkuta njiani amevaa Ihraam kama mimi shuka mbili tu nyeupe miongoni mwa wanaume hana kitu chochote ndani kwani ni haramu kuvaa nguo yoyote iliyoshonwa wakati upo katika Ihraamu. Sote tumevaa viatu vya kawaida tu mithili ya kanda mbili au viatu visivyofunika mguu wote na hakuna hata mwanamme mmoja aliyevaa kofia, ukishahirimia hutakiwi kuvaa kofia kichwani kwa mwanamme au kupaka manukato ya aina yoyote.

Kila ninamkuta njiani simjui jina lake wala wapi anapotoka, simjui kama ni Daktari au ni Mwalimu, Mpagazi au Mchuuzi, ni mheshimiwa au mtu wa kawaida, mweupe, mweusi mkubwa, mdogo  lakini namjua kama ni ndugu yangu Muislamu  na sote tumetamka Laa Ilaaha Illa Llaah Muhammadun Rasuulu Llaah. Kalima au neno hili ndilo lilitukutanisha katika ardhi ya Haram, Kalima hili ndilo litakalokutanisha peponi, Kalima hili ndilo litakalotuepusha na adhabu kali ya moto wa Allaah ‘Azza wa Jall ikiwa tutakamilisha masharti yake saba.

Tulipofika Mina huku tukiendeleza Talbiyah na kuomba dua kwa Allaah ‘Azza wa Jall, kila nikiirudia Talbiyah basi nafsi yangu inanikumbusha ujumbe mzito uliopo kwenye talbiyah nao ni wa Tauhiyd kumpwekesha Allaah ‘Azza wa Jall kwa ibada na kila kwa kila kitu.  Tunamhakikishia Allaah ‘Azza wa Jall kwamba hana mshirika huku tumemwitikia, tunamthibitishia Allaah ‘Azza wa Jall kwamba hakika himidi na shukrani, neema na ufalme vyote ni vyake pekee na hana mshirika.


Nikaikumbuka aya katika Qur’aan inayosema: “hakika Sala zangu, vichinjwa vyangu, uhai wangu na mauti yangu vyote ni vya Allaah Mola wa viumbe vyote, hana mshirika na hivyo nimeamrishwa kuwa Muislamu wa awali”. Naam Hijja ni darsa muhimu inayotufundisha somo la Tawhiyd kwani Mtume Muhammad Swalla Allaahu ‘alayhi wasallam alihama Makkah kwenda Madina (kwa sababu ya kuisimamisha Tawhiyd) na aliporudi kuikomboa Makkah aliikomboa bila ya kumwaga damu na kuisimamisha Tawhiyd.

Itaendelea...

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.