Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                          18.10.2016
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza haja ya kujitegemea  kwa kuwatumia wataalamu waliopo nchini sambamba na kutumia nyenzo na rasilimali zilizopo ili kupunguza gharama zisizo za lazima na hatimae kuweza kuisaidia Serikali.

Dk. Shein aliyasema hayo leo,   Ikulu mjini Zanzibar katika kikao maalum kati yake na uongozi wa Wizara ya Elimu mara baada ya kuwasilishwa kwa Ripoti ya Utekelezaji wa Kazi za Wizara  hiyo kwa kipindi cha Julai hadi Septemba mwaka 2016.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa kuna faida kubwa iwapo wataalamu waliopo Mawizarani watatumiwa vizuri badala ya wataalamu kutoka nje ya nchi.

Alisema kuwa kwa upande wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, imejaaliwa kuwa na wataalamu wa fani mbali mbali ambao wanaweza kuisaidia Wizara hiyo katika kufanya mambo yake mbali mbali katika kuimarisha sekta ya elimu.

Aidha, Dk. Shein alieleza juhudi za makususdi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika ukusanyaji wa mapato huku akisisitiza azma ya Serikali ya kukata  maposho yasiyoyalazima ili fedha hizo ziweze kusaidia katika kuendeleza majukumu na mipango ya Serikali.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Wizara hiyo kwa kuwasilisha vyema Mpango wake wa kazi na kuwataka viongozi na watendaji wa Wizara hiyo kuendelea kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja ili waendelee kupata mafanikio.

Pamoja na hayo, Dk.  Shein alisisitiza umuhimu  wa uzalendo katika utekelezaji wa majukumu na kueleza kuwa suala zima la uzalendo litapewa kipaumbele mafanikio makubwa yanaweza kupatikana.

Nae Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliipongeza Wizara hiyo na kusisitiza haja ya kuendelezwa vuguvugu la mashindano katika skuli mbali mbali hapa nchini ili kuweza kupata wanamichezo wazuri sambamba na kuongeza vipaji vya vijana katika sekta ya michezo.

Balozi Idd nae alitumia fursa hiyo kuihakikishia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kuwa ataendelea kushirikiana na kuisaidia Wizara hiyo ili kuweza kupatikana elimu iliyo bora hapa nchini.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Abdulhamid Yahya Mzee  alisisitiza umuhimu wa usimamizi  katika skuli hapa nchini na kuwataka walimu wakuu na wasaidizi wao kushirikiana kwa pamoja katika kulifanyia kazi suala hilo ili elimu bora iliyokusudiwa iweze kupatikana.

Mapema Waziri wa  Elimu na Mafunzo ya Amali, Riziki Pembe Juma  alieleza kuwa  katika mwaka wa fedha wa 2016/2017, Wizara yake inaendelea na malengo ya kupanua upatikanaji wa huduma za elimu na kuimarisha ubora wa elimu inayotolewa.

Alisema kuwa Wizara imeweka vipaumbele katika kufikia dhamira ya utoaji wa elimu bora kwa wote na kuweza kupanga mipango mbali mbali ikiwemo kuimarisha elimu ya Maandalizi, kutayarisha na kuchapisha miongozo ya walimu, kuimarisha elimu na Msingi, kuimarisha Elimu ya Sekondari, Kuimarisha Elimu Mbadala na Watu wazima na kuimarisha elimu ya juu.

Aidha, Waziri Pembe alisema kuwa katika kipindi cha miezi mitatu Julai hadi Septemba 2016, Wizara hiyo imeweza kutekeleza malengo mabli mbali yakiwemo matayarisho ya Mpango Mkuu wa Maendeleo ya Elimu kwa kipindi cha miaka mitano (2016-2021) yameanza.

Pamoja na hayo, alieleza kuwa ujenzi wa vituo viwili vya Mafunzo ya Amali huko Makunduchi na Daya nao umeanza pamoja na ujenzi wa Kituo cha Utamaduni wa Kiislamu Mazizini umekamilika.

Alieleza kuwa Wizara hiyo imepokea jumla ya madawati 5,150, Viti 1630 na meza 600, samani ambazo zimepokelewa kutoka kwa Wabunge, Wawakilishi na Diaspora.

Vile vile alieleza kuwa ujenzi wa jengo jipya la Taasisi ya Utalii Maruhubi unaendelea na umefikia asilimia 20 na ujenzi wa jengo jipya la Taasisi ya Karume nao unaendelea na umefikia asilimia 30 ambapo pia, ujenzi wa Kituo cha Mafunzo ya Amali Wingwi Mtemani nao unaendelea na umefikia asilimia 90.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.