Kamishna wa Idara ya Fedha za Nje, Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango – Zanzibar Bw. Yussuf Ibrahimu Yussuf, akizungumza wakati akifungua Warsha ya kujenga uelewa wa Ushirikiano kati ya Tanzania na Washrika wa Maendeleo iliyofanyika katika ukumbi wa Hazina Ndogo, Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam.
Na. Eva Ngowi -Wizara ya Fedha, Dar es Salaam
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeendesha mafunzo ya siku moja kwa Washirika wapya wa Maendeleo na Wakurugenzi wa Sera na Mipango iliyojikita katika kuimarisha uelewa wa taratibu, sera, na mikakati ya maendeleo ya nchi pamoja na kushirikiana katika utekelezaji wa Mwongozo wa Ushirikiano wa Maendeleo (DCF) katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.
Akizungumza kwa niaba ya Wizara ya Fedha wakati akifungua warsha hiyo, iliyofanyika katika ukumbi wa Mikutano wa Hazina Ndogo jijini Dar es Salaam, Kamishina, Idara ya Fedha za Nje, Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango - Zanzibar Bw. Yussuf Ibrahim Yussuf alisema kuwa dhamira ya warsha hiyo ni kuhakikisha serikali inaweka ushirikiano madhubuti na Washirika wa Maendeleo.
“Serikali zote mbili – ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ya Mapinduzi ya Zanzibar – zinaendelea kuimarisha ushirikiano na Washirika wa Maendeleo wenye misingi ya uwazi, uwajibikaji na kulingana na vipaumbele vya taifa. Mafunzo haya ni hatua muhimu katika kuelekea utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Tanzania 2050 na Zanzibar 2050,” alisema Bw. Yussuf.
Alisema kuwa warsha hiyo ilikuwa ni pamoja na kutoa uelewa kwa Washirika wapya wa Maendeleo kuhusu mazingira ya kisera, taratibu, na mifumo ya kitaasisi inayosimamia misaada ya maendeleo nchini Tanzania.
Bw. Yussuf, alisema, Mada zilizowasilishwa na kujadiliwa katika Warsha hiyo ni pamoja na Mwongozo wa Ushirikiano wa Maendeleo (DCF), Mzunguko wa Bajeti ya Serikali, Dira za Maendeleo za 2050, na Mwongozo wa Uandaaji, Utekelezaji na Usimamizi wa Miradi na Majadaliano ya Mikopo, Dhamana na Misaada.
Aidha Bw. Yussuf alisema kuwa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuendena na kasi ya kukua kwa teknolojia kunahitaji ushirikiano wa karibu, upatikanaji na usimamizi wa fedha za mabadiliko ya tabianchi kupitia vitengo maalum vilivyoanzishwa, usimamizi bora wa fedha za umma, ikiwemo kuongeza uwazi na udhibiti wa matumizi ya bajeti.
“Maeneo mengine ya ushirikiano huo ni Maendeleo ya miundombinu, usafiri, nishati, maji na teknolojia za kidijitali. Msaada wa kiufundi katika maeneo ya kidijitali na akili mnemba (AI) kwa ajili ya kuboresha utoaji huduma na ushindani wa kiuchumi,” Alisema Bw. Yussuf
Alisema kuwa ufanisi wa ushirikiano wa maendeleo unategemea uwazi, mawasiliano, na uelewa wa pamoja juu ya sera, mipango na miongozo ya kitaifa na juhudi za kuhakikisha Washirika wa Maendeleo wanalinganisha misaada yao na mzunguko wa bajeti na vipaumbele vya taifa.
“Tunathamini kwa dhati uhusiano wetu na Washirika wa Maendeleo kwa Mchango wao wa kifedha, kitaalamu na kimawazo ni nguzo ya mafanikio yetu,” aliongeza Kamishina Yussuf.
Mafunzo hayo ya kujenga uelewa yaliwashirikisha Washirika wa Maendeleo (DPs), Wakurugenzi wa Sera na Mipango (DPPs) wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Wakurugenzi wa Sera, Mipango na Utafiti (DPPR) wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Warsha hiyo imeaandaliwa na Wizara ya Fedha kupitia Idara ya Fedha za Nje, kwa lengo la kuongeza ufanisi wa upatikanaji na usimamizi wa rasilimali za nje na kuhakikisha matokeo chanya katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
No comments:
Post a Comment