Habari za Punde

Washauri Wawekezaji Sekta ya Utalii Zanzibar Wapewe Ushirikiano

Na Salum Vuai, Maelezo.
Jamii visiwani Zanzibar imeombwa kutoa ushirikiano wa kutosha kwa wawekezaji wanaoonesha nia ya kuwekeza miradi ya maendeleo yenye mwelekeo wa kubadilisha maisha ya wananchi na kuwatoa kwenye umasikini.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa ziara ya kutembelea eneo la Matemwe ambako kampuni ya Penny Royal inajenga kijiji cha utalii, mwanaharakati Rashid Yussuf Mchenga, amesema Zanzibar haiwezi kujitenga na dunia, hivyo hapana budi kuwapokea kwa mikono miwili wawekezaji wenye nia njema.
Alitaka dhamira ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuwafungulia milango wawekezaji wa nje iungwe mkono na kila mpenda maendeleo, kwani uchumi wa visiwa hivi unahitaji ushirikiano wa kila hali na taasisi zenye mitaji mikubwa ya kuwekeza miradi yao hapa nchini zikiwemo za kigeni.
Mchenga ambae pia ni Katibu Mwenezi Taifa wa chama cha ADA-TADEA, amesema mradi huo utakaokuwa wa aina yake, ni neema ya kushukuriwa na wananchi wa Matemwe, mkoa wote wa Kaskazini na Wazanzibari kwa jumla.
“Kama tunavyosikia kwamba mradi huu utaajiri zaidi ya wananchi 1,500 katika hatua za awali, hii ni fursa muhimu ya kuwasaidia vijana wetu kuondokana na tatizo la ajira,” alifahamisha.
Hata hivyo, alisema kustawi kwa miradi ya maendeleo katika nchi yoyote lazima kuende sambamba na kuimarika kwa hali ya amani na usalama, kwani bila vitu hivyo, hakuna jambo la maendeleo linaloweza kufanyika.
Meneja wa Penny Royal Brian Thompson, amesema miongoni mwa mipango yao katika kuufanikisha mradi huo, ni kushirikiana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, kuandaa utaratibu wa mafunzo ya lugha ya Kiingereza kwa vijana, pamoja na elimu ya kazi zinazohusiana na utalii ili kuwaandaa kwa ajili ya ajira zitakazopatikana.
Alisema ujenzi wa kijiji hicho utakaogharimu zaidi ya dola bilioni moja, unatarajiwa kukamilika kabisa baada ya miaka minane, ukifanyika kwa awamu mbili, ambapo kila moja itachukua miaka mine.
Mradi huo mkubwa na wa kwanza wa aina yake hapa nchini, utajumuisha ujenzi wa skuli, hospitali, kituo cha polisi, kituo cha jamii kwa  wajasiriamali, uwanja wa ndege, kiwanja cha Golf na ujenzi wa visiwa vidogo vidogo pamoja na mkahawa maalum utakaojengwa chini ya bahari.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.