Habari za Punde

Jamii yaaswa kusimamia kwa nguvu zote amani iliyopo



 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                   22.11.2016
---
MKE wa Rais wa  Zanzibar Mama Mwanamwema Shein amesema kuwa miongoni mwa mambo muhimu ambayo jamii inapaswa kuyatekeleza kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuyalinda Mapinduzi ya Januari 12, mwaka 1964 sambamba na kusimamia kwa nguvu zote amani iliyopo.

Mama Shein aliyasema hayo leo kwa nyakati tofauti wakati akizungumza na akinamama, viongozi na wanachama wa Jumuiya ya Wanawake Tanzania (UWT) wa Wilaya ya Kaskazini A na Wilaya ya Kaskazini B Unguja kwa lengo la kuwasalimia na kuwashukuru kwa kuendelea kuiunga mkono CCM, na kupelekea kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi uliopita.

Akiwa katika ukumbi wa Korea, huko Kibokwa Wilaya ya Kaskazini A, Mama Shein alieleza kuwa kila mtu kwa nafasi yake ailinde amani na kuinukuu kauli ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein anayoitoa mara kwa mara isemayo “hakuna mbadala wa amani”.

Alisema kuwa mara nyingi kinamama na watoto huwa ndiyo wanaoathirika zaidi wakati amani inapotoweka.

Mama Shein ambaye katika ziara yake hiyo amefuatana na viongozi mbali mbali wakiwemo wake wa Wabunge na Wawakilishi wa Zanzibar, alisema kuwa tayari Serikali iliyochaguliwa na wananchi yenye nia ya kweli ya kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar, imeshaundwa na inaendelea na kazi ya kuwatumikia wananchi kwa ufanisi mkubwa.

Alieleza kuwa Serikali chini ya uongozi wa Dk. Shein inafanyakazi kwa umakini mkubwa kwa lengo la kutimiza matumaini na matarajio waliyonayo wananchi wakati walipoichagua.

Hivyo, Mama Shein alisema kuwa ni wajibu wa viongozi na wananchi wote kutoa ushirikiano katika kuhakikisha kwamba malengo ya Serikali katika kuinua uchumi na kuimarisha huduma za jamii yanafanikiwa.

Mapema Mama Asha Balozi, Mke wa Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alieleza haja ya wanawake kuendelea kupendana huku akisisitiza suala zima la uadilifu katika mchakato mzima wa uchaguzi ujao wa Chama hicho hapo mwakani.

Aliwataka akinamama kujipunguzia majukumu na badala yake wawe na utaratibu wa kujua nyendo za watoto wao hasa kutokana na kukithuri vitendo vya ubakaji ambavyo vimeendelea kushika kasi katika Mkoa huo.

Nae Mama Fatma Karume kwa upande wake aliwataka akina mama kuwaelimisha na kuwafunza watoto wao pamoja na kuwasaidia waume zao katika harakati zote za kisiasa na kimaendeleo.

Alieleza furaha yake kwa kona wanawake waliowengi hivi sasa wamepata uongozi na wamo madarani jambo ambalo ilikuwa nadra kabla ya Mapnduzi ya Januari 12, 1964 na kuwataka waliopana fursa hiyo kuitumia vyema na kuishi na watu vizuri.

Katika risala yao wanachama wa Jumuiya ya UWT walieleza kufarajika kwao na ujio wa Mama Shein katika Wilaya yao ya Kaskazini A na kumuhakikishia kuwa wataendelea kuiunga mkono CCM ili iendelee kushika hatamu.

Akiwa katika ukumbi wa  Hoteli ya Sea Cliff huko Kama, Wilaya ya Kaskazini B, Unguja Mama Shein alitoa wito kwa jamii kuchukua juhudi za makusudi katika kuhifadhi mazingira na kuielimisha jamii juu ya utunzaji wa mazingira hayo.
Alisema kuwa maeneo ambayo kwa miaka mingi yamekuwa yakitegemewa kuwa na vianzio vikubwa vya maji, yameathiriwa kutokana na ukataji wa miti, na ujenzi wa nyumba bila ya kuzingatia mipango mizuri sambamba na shughuli za uchimbaji wa mchanga na udongo ambazo zimeathiri sana ndani ya Mikoa hapa nchini.

Pia, Mama Shein ambaye alipata mapokezi makubwa katika mkoa huo, alisisitiza suala zima la kushirikiana na Serikali katika kupambana na ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto kwani katika jamii kumeendelea kusikika vitendo vya aina hiyo ambavyo ni aibu, na ni kinyume cha maadili na mafundisho ya Dini.

Nae Mama Fatma Karume aliwataka akinamama wa Jumuiya hiyo kutojali maneno na kasumba mbali mbali zinazosambazwa na wapinzani ambazo hazina manufaa wala nafasi kwa CCM.

Nae Mama Asha Balozi aliendelea kutoa wito kwa wananchi wa Mkoa huo kupiga vita suala zima la udhalilishaji wa wanawake na kusisitisha mashirikiano ndani ya Jumuiya ya UWT.

Nao wanajumuiya ya UWT Wilaya ya Kaskazini B, walieleza kuwa haja ya kuongezewa mitaji na mikopo katika vikundi vyao ili kipato wanachokipata kiweze kukidhi haja ya malengo yao.

Wakieleza suala zima la udhalilishaji wa wanawake na watoto na kueleza kuwa suala zima la mashirikiano katika kesi za ubakaji sambamba na changamoto zilizopo katika mtiririko mzima wa hukumu za kesi za aina hiyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.