Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                          10.12.2016
---
RAIS wa  Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  amewataka viongozi wa Serikali kutoa taarifa kwa wananchi kwa mujibu wa sheria na miongozo iliyopo kwani suala hilo ni la kikatiba na msingi muhimu wa kuimarisha maadili na kukuza utawala bora.

Dk. Shein aliyasema hayo leo  huko katika viwanja vya Victoria Garden mjini Zanzibar, katika maadhimisho ya siku ya Maadili na Haki za Binaadamu, hafla ambayo ilihudhuria na viongozi mbali mbali wa Serikali na weatendaji wake, vyama vya siasa, wake na wananchi.

Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa  kuna baadhi ya viongozi wanadhani kwamba anapowahimiza kuwa watoe taarifa kwa wananchi wanadhani kwamba jukumu hilo si lao badala yake ni la vyombo vya habari au ni kazi ya watu maalum.

Alisema kuwa dhana hiyo si sahihi kwani kazi hiyo ni ya viongozi wote kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 18, kifungu cha (2) na kusisitiza kuwa licha ya Serikali kuweka utaratibu maalum unaowataka viongozi wa Serikali watoe taarifa kwa wananchi, bado wapo ambao hawatekelezi vyema agizo hilo.

“Katika kuimarisha utawala bora, tunapaswa tuhakikishe kuwa tunatoa taarifa sahihi na za kuaminika kwa wanaostahiki, wanawananchi na watu waliochuni ya dhamana zetu”,alisema Dk. Shein.

Akieleza kuhusiana na suala la rushwa Dk. Shein alisema kuwa serikali zote mbili hapa nchini zinaendelea kuchukua juhudi katika kupambana na rushwa, uhujumu wa mali za umma na kuimarisha uwajibikaji, imeanza kuza matunda.
Aidha Dk. Shein alisema kuwa, viongozi wamechaguliwa na wameteuliwa ili waongoze Wizara na Idara zao kwa mujibu wa taaluma, uzoefu na sifa maalum walizonazo, hivyo wawe mstari wa mbele kutoa rai mbali mbali za maendeleo na kusimamia utekelezaji wake badala ya kusubiri maagizo kutoka ngazi za juu.

Alisema kuwa kila kiongozi aliyepewa jukumu la kuongoza wananchi au kusimamia taasisi ya Serikali ni lazima atekeleze jukumu hilo kama inavyostahiki kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo hasa kwa wale viongozi waliokula viapo.

Dk. Shein alisema kuwa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma tayari imeshaanza kutoa elimu juu ya umuhimu wa madili ambapo aliwahimiza  viongozi wote waliohusika wahakikishe wanarejesha fomu ya tamko la rasilimali na madeni zilizotolewa hivi karibuni kwa viongozi wote waliotajwa kwenye sheria Na.4 ya mwaka 2015 kwa wakati uliopangwa.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza kuwa kila mmoja ahakikishe anatoa taarifa kama ilivyoelezwa na taarifa zote zinazotolewa ziwe sahihi kwani utoaji wa taarifa za uongo ni kosa kwa mujibu wa sheria  hiyo ya maadili.

Dk. Shein alilitilia mkazo suala zima la kushikamana katika kupiga vita unyanyasaji wa watoto na akina mama huku akisisitiza matumizi mazuri ya mitandao sambamba na kupiga vita matumizi ya dawa za kulevya.

Mapema Waziri wa Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora alieleza kuwa juhudi zitaendelea kuchukuliwa katika suala zima la utawala bora, kusimamia maadili pamoja na rushwa ili kuhakikisha lengo lililokusudiwa linafikiwa.

Nae Mwenyekiti wa Tume ya Maadili, Asaa Ahmada Rashid alisema kuwa kauli mbiu ya siku hiyo inayosema ‘Imarisha utawala bora kwa kukuza uadilifu, uwajibikaji, haki za binaadamu na mapambano dhidi ya rushwa” imebeba ujumbe muwafaka kwa taasisi za utawala bora.

Aidha, Mwenyekiti huyo alitumia fursa hiyo kueleza juhudi za Serikali katika kuimarisha utawala bora ikiwa ni pamoja na kuunda taasisi mbali mbali ikiwemo Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma ambayo imepewa jukumu la kusimamia Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Sheria Na 4 ya mwaka 2015.

Mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania Bi Anna Liboro Senga kwa upande wake alisisitiza umuhimu wa utawala bora, maadili na wajibikaji ambapo pia alitoa ujumbe wa UN katika kuadhimisha siku ya Maadili duniani.

Bi Senga, alitumia fursa hiyo kueleza kuwa bila ya kuwepo kwa maadili amani na utulivu haitokuwepo huku akitoa pongezi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein kwa kusimamia amani na utawala bora.

Mapema Dk. Shein alipokea maandamano kutoka kwa Wafanyakazi wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee. Vijana, Wanawake na Watoto.

Sherehe hizo zilipambwa na vionjo mbali mbali vikiwemo ngoma ya kibati kutoka kikundi cha Vijana Ngoma Group, Mchezo wa Kuigiza kutoka kundi la Black Root Investment chini ya Makombara pamoja na utenzi mwanana.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.