STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 1.1.2017
RAIS wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewataka
wananchi wasikae kusubiri hadi kuambiwa na madaktari kufanya mazoezi ndipo wakaanza kukurupuka kwani mara nyingi
mtu anapopewa ushauri wa kufanya mazoezi na daktari huwa athari fulani
zimeshaanza kujitokeza mwilini mwake.
Hivyo, Dk. Shein aliwasisitiza wananchi kuzingatia hekima ya wazee kwamba kinga ni
bora kuliko tiba na badala yake ni vyema kila mmoja akajiwekea muda maalum wa
kufanya mazoezi yanayolingana na afya na umri wake.
Dk. Shein aliyasema hayo leo mara baada ya
kushiriki kikamilifu katika maadhimisho ya Siku ya Mazoezi Kitaifa huko katika
uwanja wa Amaan, Mjini Zanzibar yalioanza uwanja wa Tumbaku hadi uwanja wa
Amaan mapema saa 12 za asubuhi,
Viongozi mbali mbali walishiriki mazoezi hayo akiwemo
Rais mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ali Hassan Mwinyi, Makamu wa
Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd,
viongozi wengine wa dini na serikali pamoja na vikundi vya mzoezi kutoka
Unguja, Pemba na Tanzania Bara.
Katika hotuba yake Dk. Shein alisema kuwa mazoezi
ni lazima hasa katika dahari hizi ambapo mfumo wa maisha umekuwa na changamoto
nyingi zitokanazo na kuongezeka kwa mahitaji na hamkani za maisha ya kisasa
hapa nchini na duniani kote.
Alisema kuwa hivi sasa jamii imeacha utamaduni wa kutembea
kwa miguu na kwa baskeli badala yake hupanda vyombo vya moto hata kwa masafa
mafupi huku akieleza athari za vyakula vya kisasa vikiwemo mahanjumati, michuzi
ya mafuta, mapochopocho yalionona ambayo hupikwa kwa samli za kisasa na kuacha
vyakula vya asili.
Dk. Shein aliwahakikishia wananchi kwamba Serikali
itaendelea na juhudi za kuimarisha michezo na kuviunga mkono vikundi mbali
mbali vya mazoezi ya viungo ikiwa ni pamoja na kuweka miundombinu bora ya
michezo.
Alisema kuwa Serikali imedhamiria kujenga viwanja
vya michezo katika kila wilaya Unguja na Pemba ambapo tayari imeanza mchakato
kwa viwanja vitatu kikiwemo kiwanja cha Kitogani Mkoa wa Kusini Unguja, Mkoa wa
Kaskazini Unguja na Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Dk. Shein aliwaahidi wana mazoezi na wana michezo
wote kwamba Serikali italifanyia kazi ombi lao la kuwapatia mafunzo walimu wa
vilabu vya mazoezi ili waendeshe michezo na mazoezi kwa njia na mbinu za
kitaalamu zaidi.
Aidha Dk. Shein alilitaja jambo linalodhorotesha
juhudi za kuimarisha michezo kuwa ni uchache wa wadhamini katika ngazi zote za
michezo ambapo kampuni nyingi zilizopo Zanzibar na Wafanyabiashara bado hawana
mwamko wa kutosha wa kutumia michezo kwa kujitangaza.
Hivyo Dk. Shein aliutaka uongozi wa Wizara ya
Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo kwa kushirikiana na Baraza la Michezo la
Zanzibar pamoja na vyama vya michezo kubuni mikakati mipya kwa kuzishawishi
Kampuni na Wafanyabiashara kutumia michezo kujitangaza.
Dk. Shein alisisitiza michezo kuzingatia nidhamu
na kuwataka wanamichezo wasisahau kuwa dhamira ya michezo ni kuburudisha na
kuunganisha na sio kugombanisha.
Kwa upande wa kombe la Mapinduzi , ambapo mara hii
michuano maalum ya vijana katika Wilaya zote za Unguja na Pemba imeanzishwa na kusisitiza kuwa timu za Zanzibar lazima
zifanye vizuri ili kombe la Mapinduzi mara hii libaki hapa hapa Zanzibar.
Dk. Shein alitoa shukurani kwa uongozi wa Wizara
ya Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo na uongozi wa Chama cha Mchezo wa
Mazoezi ya Viungo (ZABESA) kwa
maandalizi mazuri ya Bonanza hilo na hatimae kutoa vyeti maalum kwa wale wote
waliofanikisha Bonanza hilo.
Nae Waziri wa Habarim Utalii, Utamaduni na
Michezo, Rashid ... aliahidi kuwa Wizara yake itaendelea kushirikiana na
vikundi vya michezo na mazoezi huku akitumia fursa hiyo kumpngeza Dk. Shein kwa
kuanzisha siku maalum ya mazoezi Kitaifa.
Mwenyekiti wa Baraza la Taifa la Michezo Zanzibar,
Sharifa Khamis alimpongeza Dk. Shein kwa kuwathamini na kuwajali wanamichezo wa
Zanzibar na kueleza jinsi wanavyofarajika na juhudi zake katika kuinua sekta ya
michezo hapa nchini.
Mapema katika risala yao wafanyamazoezi ya viungo walieleza
kwamba kutofanya mazoezi kunaongeza hatari ya kupatwa kwa ugonjwa wa moyo na
kuzisha hatari ya shinikizo kubwa la damu na pia huongeza maradufu uwezekano wa
kufa kwa shinikizo la damu na kiharusi.
Walieleza kuwa mwamko wa kufanya mazoezi nchini
umeongezeka huku wakieleza umuhimu wa mazoezi kwa watoto na hatimae kueleza
changamoto yao ya kuhitaji kupatiwa walimu wa vilabu mafunzo ya kufanya mazoezi
kitaalamu zaidi kwa maslahi ya Taifa.
Bi Rukia Ramadhani nae hakua nyuma katika kutoa
burudani ambayo ilitumbuiza hadhara iliyokuwepo kwa nyimbo yake maalum ya
kumpongeza Dk. Shein ambaye ni muasisi
wa Bonanza hilo ambapo pia wanamazoezi hao nao walipata fursa ya kuonesha
mazoezi mepesi pamoja na vikundi vya sarakasi navyo vilionesha umahiri wao.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment