Mheshimiwa
Spika,
Awali ya yote nianze
kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa utukufu kwa kutujaalia uhai na afya
njema na kutuwezesha kufika hapa kujumuika kwa pamoja kwa lengo la kuendelea na
majukumu yetu, pili naomba kuchukua fursa hii adhimu kukushukuru wewe
mheshimiwa Spika kwa kunipa nafasi hii ya kusimama mbele ya Baraza lako tukufu
kwa lengo la kuwasilisha maoni ya Kamati ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu
wa kitaifa kuhusu mswada wa Sheria ya kufuta Sheria ya Tume ya Uchaguzi Nam.9
ya 1992 na kutunga Sheria ya kuanzisha Afisi ya Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar,
majukumu, uwezo na mambo mengine yanayohusiana na hayo.
Mheshimiwa
Spika,
Napenda kuwashukuru
watendaji wa Ofisi ya Makamo wa pili wa Rais pamoja na watendaji wa Tume ya
Uchaguzi kwa mashirikiano yao makubwa wanayoendelea kutupatia katika
utekelezaji wa majukumu yetu ya kila siku hususan katika kuupitia na kuuchambua
mswada huu adhimu. Sambamba na shukurani hizi napenda kutumia fursa hii nawapongeza
sana wadau mbali mbali waliojitokeza katika Kamati yetu na kuwasilisha maoni
yao kwa lengo la kuufanya mswada huu uwe bora zaidi, kwa kuthamini mchango wao ndio
maana kila tunapokuwa na miswada huwa tunawaalika wadau ili waweze kutusaidia
kuichambua miswada hiyo.
Mheshimiwa
Spika,
Mswada huu wa
kuanzisha Afisi ya Tume ya Uchaguzi ni muhimu sana kwani umekuja kuweka misingi
bora ambayo itakuwa inaenda sambamba na Katiba ya Zanzibar ambayo ndio
iliyoanzisha Tume hii. Hivyo mswada huu umekuja kuanzisha uwepo wa Afisi ya
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ambayo itaongozwa na Mkurugenzi na ambae atakuwa Katibu
wa Tume ya Uchaguzi. Pia Mswada huu wa Sheria umeanzisha Afisi za Tume za Wilaya ambazo
zitakuwa kwa kila Wilaya ambazo zitakuwa jukumu la kuhakikisha uchaguzi au kura
ya maoni zinaendeshwa katika misingi ya demokrasia na utawala bora.
Mheshimiwa
Spika
Kamati yangu baada ya kuupitia
mswada huu imependekeza baadhi ya marekebisho ambapo naamini waraka wa
marekebisho hayo kila mjumbe ameshapatiwa nakala yake, hivyo ni vyema
tukaupitia kwa makini ili tuweze kutoa mapendekezo zaidi kwa lengo la kuufanya
mswada huu muhimu kuwa bora zaidi. Baadhi ya marekebisho ambayo Kamati
imependekeza ni kuongezwa kwa kifungu kidogo cha (3) kitakachosomeka “Afisa Uchaguzi wa Wilaya atakuwa msimamizi
wa jimbo au majimbo katika Wilaya yake katika kipindi cha Uchaguzi”.
Sababu ya mapendekezo
haya ni kuhakikisha kunakuwa na usimamizi mzuri wa uchaguzi katika majimbo
ambao utafanywa na Afisa huyo wa Wilaya ambae atakua ni Afisa wa Tume, kinyume
na utaratibu uliopo sasa ambapo msimamizi wa uchaguzi katika majimbo anakua sio
mwajiriwa wa Tume hivyo anapotenda kosa lolote Tume haina mamlaka ya
kumuwajibisha.
Mheshimiwa
Spika
Katika kifungu cha
26(2) Kamati imependekeza kuingizwa neno “zitawasilishwa”
baina ya neno “fedha” na neno “kwa”. Sababu ya marekebisho hayo ni
Sheria hii kumtaka Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali baada ya
kumaliza ukaguzi wa Hesabu za Tume kuwasilisha Ripoti yake kwa Waziri.
Mheshimiwa
Spika,
Ni wazi kuwa utekelezaji
wa Sheria hii hautakamilika bila ya kutungwa Kanuni zake, kwahivyo, Mhe. Waziri
mara baada ya Baraza lako tukufu kupitisha Sheria hii na kusainiwa na Mhe. Rais,
Kanuni za Sheria hii zitungwe haraka iwezekanavyo kwa ajili ya utekelezaji
mzuri wa Sheria hii.
Mheshimiwa
Spika,
Kazi ya kuupitia
mswada huu tumeifanya kwa mashirikiano ya pamoja baina ya Wajumbe wa Kamati ya
kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa kitaifa ambao ni Wajumbe wenye kupenda
kujituma na kufanya kazi kwa bidii ya hali ya juu, Mheshimiwa Spika kwa ruhusa
yako naomba niwatambue kwa kuwataja majina Wajumbe hao kama hivi ifuatavyo:-
1.
Mheshimiwa Omar Seif Abeid
Mwenyekiti
2.
Mheshimiwa Panya Ali Abdalla M/Mwenyekiti
3.
Mheshimiwa Mtumwa Suleiman Makame Mjumbe
4.
Mheshimiwa Mussa Ali Mussa
Mjumbe
5.
Mheshimiwa Simai Mohammed Said Mjumbe
6.
Mheshimiwa Amina Iddi Mabrouk Mjumbe
7.
Mheshimiwa Hussein Ibrahim Makungu Mjumbe
8.
Ndg KassimTafana Kassim
Katibu
9.
Ndg Maryam Rashid Ali Katibu.
Mheshimiwa
Spika,
Mwisho kabisa nachukua
nafasi kukushukuru tena Mheshimiwa Spika kwa kuniruhusu kuwasilisha maoni ya Kamati
juu ya Mswada huu uliombele yetu lakini pia kuwashukuru Wajumbe wote wa Baraza
lako tukufu kwa kunisikiliza kwa makini, hivyo nawaomba waupitie, waujadili, wakosoe
na hatimae kuupitisha mswada huu muhimu kwa ajili ya kukuza Demokrasia na
maendeleo ya katika nchi yetu na hatimae kuwa Sheria itakayotumika katika
kuendesha shughuli za Tume ya Uchaguzi.
Mheshimiwa,
Kwa niaba yangu na kwa niaba ya Kamati ya Kusimamia
Ofisi za Viongozi Wakuu wa kitaifa naunga mkono hoja na naomba kuwasilisha.
Ahsante,
………
Omar
Seif Abeid,
Mwenyekiti,
Kamati ya kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa
Kitaifa,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment