STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 9.2.2017

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein leo amekabidhiwa ripoti ya Uchaguzi Mkuu wa tarehe 25 Oktoba
2015 pamoja na uchaguzi wa marudio wa terehe 20 Machi 2016 na kuipongeza Tume
ya Uchaguzi Zanzibar huku akieleza kuwa hiyo ndio ripoti sahihi na hakuna
ripoti nyengine.
Dk. Shein aliyasema
hayo mara baada ya kukabidhiwa Ripoti ya
Uchaguzi Mkuu wa tarehe 25 Oktoba 2015 pamoja na Uchaguzi wa Marudio wa
terehe 20 Machi mwaka jana, Ripoti ambayo ni kwa ajili ya Uchaguzi wa Rais wa
Zanzibar, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani.
Hafla hiyo, ilifanyika
Ikulu mjini Zanzibar na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa
Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar
Makungu, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Mwanasheria Mkuu wa
Zanzibar Said Hassan, Mawaziri, Washauri wa Rais na viongozi wengine wa
Serikali.
Katika maelezo yake
Dk. Shein alisema kuwa Ripoti hiyo ni muhimu sana katika utekelezaji wa kazi za
Serikali na kuipongeza Tume ya Uchaguzi pamoja na viongozi wake wote kwa kazi
nzuri ya kutayarisha Ripoti hiyo kwa umakini mkubwa na busara pamoja na hekima
kubwa.
Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kutoa pongezi kwa wananchi wa Zanzibar kwa kushiriki uchaguzi wa kwanza
wa Oktoba 25 mwaka 2015 pamoja na ule wa marudio wa Machi 20 mwaka jana na
kutumia haki yao ya kuwachagua viongozi wanaowataka.
Aidha, Dk. Shein alisema
kuwa Tume ya Uchaguzi inaongozwa na Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 pamoja na
Sheria ya Uchaguzi Namba 11 ya mwaka 1984, hivyo aliwapongeza kwa kuzitumia
nyenzo hizo kwa kutekeleza majukumu yao kutokana na changamoto zilizojitokeza
katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 25 mwaka 2015.
Dk. Shein alisema kuwa,
kama inavyofahamika kuwa Tume hiyo haiingiliwi na taasisi wala mtu yoyote hivyo Tume ndio inayojua ukweli na hatimae
ndio imetayarisha ripoti hiyo ambayo ina umuhimu mkubwa kwa Serikali pamoja na
wananchi wote.
Alisema kuwa kutokana
na tukio hilo kuwa muhimu ndio maana amewaalika Mawaziri wote wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kuja kushuhudia tukio hilo muhimu na kusisitiza kuwa
mapendekezo yote anayakubali.
Sambamba na hayo, Dk.
Shein alipongeza mashirikiano mazuri yaliopo kati ya Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar na Tume ya Uchaguzi ya Taifa na kutumia fursa hiyo kuwapongeza wale
wote waliosaidia uchaguzi huo.
Dk. Shein alimueleza
Mwenyekiti huyo wa Tume ya Uchaguzi kuwa, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
chini ya uongozi wake italisimamia kwa karibu suala la changamoto ya ofisi yao
kwa kujengwa ofisi nyengine mpya au kufanyiwa ukarabati iliyopo hivi sasa huku
akiahidi kufanya ziara siku ya Jumaatatu ili kujionea mwenyewe hali halisi ya
ofisi hiyo.
Mapema Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar
Jesha Salim Jecha alieleza kuwa Ripoti
hiyo inaeleza utaratibu wote wa Uchgauzi tangu uandikishaji wa wapiga kura
katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, mapitio ya uchaguzi wa idadi, majina
na mipaka ya majimbo ya uchaguzi, uteuzi wa wagombea.
Pia, Mwenyekiti Jecha alieleza kuwa Ripoti hiyo inaeleza
kuhusu kampeni, kupiga kura, kuhesabu kura hadi kutangazwa kwa matokeo na
uteuzi wa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Viti maalum.
Aidha, Mwenyekiti
Jecha alisema kuwa Ripoti hiyo imeeleza
kufutwa kwa uchaguzi na matokeo yake pamoja na usimamizi wa uendeshaji wa
uchaguzi wa marudio mwaka 2016.
Aliongeza kuwa Ripoti
ya Uchaguzi ni nyenzo muhimu sana itakayotumika kutoa maelezo ya mchakato wa
shughuli zote zilizofanywa katika kipindi chote cha uchaguzi na kusisitiza kuwa
uandishi wa Ripoti hiyo hauna tofauti na ripoti nyengine zinazohusiana na
Uchaguzi wa Rais, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani kwa chaguzi
zilizopita.
Ripoti hiyo yenye
lugha ya kiswahili ina Sura 15, kurasa 302, Majedwali 13 na Viambatisho 28
ambao kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo Ripoti hiyo itasambazwa sehemu mbali mbali
zikiwemo Ofisi na Taasisi za Serikali na
Mahkama.
Sehemu nyengine ni
Baraza la Wawakilishi, Vyama vya Siasa, Maktaba ya Taifa, Maktaba za Vyuo vya
Elimu ya Juu, Idara ya Nyaraka, Taasisi zisizo za Serikali pamoja na Wadau
mbali mbali ambapo pia, itawekwa kwenye tovuti ya Tume ya Uchaguzi.
Sambamba na hayo,
Mwenyekiti huyo alitumia fursa hiyo kueleza changamoto mbalimbali zinazoikabili
Tume hiyo na kueleza kuwa Serikali haina budi kusaidia ili kuzipatia ufumbuzi
ikiwemo nafasi finyu katika jengo la Ofisi za Tume hiyo.
Mwenyekiti Jecha
alieleza kuwa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar inatoa shukurani kwa wadau wote
walioshiriki kwa namna moja au nyengine na ambao kwa nafasi zao walisaidia
kufanikisha uchaguzi huo.
Akiwataja miongoni
mwao ni Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), Shirika la Umoja wa Mataifa la
Mipango ya Maendeleo (UNDP) na Washirika wengine wa Maendeleo.
Wadau wengine
aliowatajwa ni vyama vya siasa, asasi za kiraia, vyombo vya habari vya ndani na
nje ya nchi, waaangalizi wa uchaguzi wa ndani na nje na wanancho wote wa
Zanzibar.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address:
2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment