Habari za Punde

Rais Dk Shein azungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya NMB Tanzania




 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                    17.2.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa azma ya Benki ya NMB ya kuendelea kuziunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo katika jamii zitasaidia kuimarisha uchumi na kuleta tija kwa wananchi

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Mkurugenzi Mkuu wa  Benki ya NMB nchini Tanzania Bi Ineke Bussemaker alipofika Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa Benki ya NMB imekuwa na mchango mkubwa katika kuzisaidia sekta za maendeleo hapa nchini zikiwemo sekta ya afya, elimu na nyenginezo hatua ambayo ni muhimu katika kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikitekeleza miradi mbali mbali ya maendeleo ambayo lengo ni kuwanufaisha wananchi pamoja na kukuza uchumi na kueleza mikakati ya kuanzisha Mradi wa huduma ya afya kwa njia ya kimtandao e-Health.

Aidha, Dk. Shein aliipongeza Benki hiyo kwa kuanzisha programu mbali mbali za kuwasaidia wakulima wakiwemo wa zao la karafuu  hapa nchini na kueleza lengo la Serikali ni kuona zao la karafuu linaimarika na ndio maana imekuwa ikichukua juhudi za makusudi ili kuhakikisha zao hilo linapata sifa kimataifa.

Dk. Shein alizitaja miongoni mwa hatua zilizochukuliwa ikiwa ni pamoja na kuwasaidia wakulima wa karafuu, kuongeza uzalishaji wa miche, kuongeza bei ya zao hilo kwa wakulima sambamba na kuanzishwa kwa mpango wa kuzipa utambulisho maalum (Branding), karafuu na bidhaa za viungo vinavyozalishwa hapa Zanzibar.

Aliongeza kuwa hizo ni hatua muhimu za kuliimarisha zao la karafuu na kuongeza usafirishaji wa bidhaa zinazotokana na viungo nje ya nchi kwa lengo la kuongeza kipato cha wakulima na wafanyabiashara pamoja na kuimarisha uchumi wa nchi.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumueleza Mkurugenzi Mkuu huyo wa NMB juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kupambana na changamoto ya ajira kwa vijana ikiwa ni pamoja na lengo la Serikali la kuanzisha uvuvi wa bahari kuu.

Alisema kuwa miongoni mwa maeneo ya kuanzia katika changamoto hiyo ni katika sekta ya uvuvi hasa ikizingatiwa kuwa visiwa vya Zanzibar vimezungukwa na bahari, hivyo alimueleza Mkurugenzi huyo umuhimu kwa Benki yake kuisaidia sekta hiyo ili wavuvi waweze kuvua katika bahari kuu pamoja na kutumia vifaa vya kisasa.

Pia, Dk. Shein alimueleza Mkurugenzi huyo juhudi zinazochukuliwa na akina mama katika kilimo cha mwani ambacho kimekuwa ni maarufu katika maeneo ya ukanda wa pwani Unguja na Pemba licha ya wakulima hao kuuza kwa  bei ndogo bidhaa hiyo.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alimuhakikishia Mkurugenzi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Benki hiyo katika kuimarisha sekta za maendeleo na kukuza uchumi wa nchi na wananchi wake.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa NMB, nchini Tanzania Bi Ineke Bussemaker alipongeza juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo katika jamii na kuahidi kuendelea kuunga mkono.

Bi Bussemaker alisema kuwa Benki yake imekuwa ikisaidia katika kuimarisha miradi mbali mbalio katika jamii ikiwemo miradi ya elimu, kilimo, afya na mengineyo na kuahidi kuiendeleza kwa lengo la kuinua kipato cha mwananchi hapa Zanzibar.

Aidha, Bi Bussemaker alisema kuwa Benki ya NMB imeweza kusaidia miradi kadhaa ikiwemo miradi ya elimu kwa kusaidia madawati, na kueleza azma ya benki hiyo kusaidia kompyuta 50 kwa skuli za Zanzibar.

Pia, Mkurugenzi huyo alieleza hatua zinazoendelea kuchukuliwa na Benki yake katika mradi wa kuwasaidia wakulima katika kuimarisha na kusafirisha bidhaa zao zikiwemo bidhaa za viungo na kusisitiza umuhimu wa kukusanya mapato kwa kutumia mfumo wa kisasa wa “e-tax” ambapo benki yake tayari imeshaanza mchakato huo kwa upande wa Tanzania Bara.

Pamoja na hayo, Mkurugenzi huyo aliahidi kuwa NMB itaendelea kusaidia miradi mbali mbali  katika jamii  kwa lengo la kuwaunga mkono  wananchi katika kujiletea maendeleo  yao ya kiuchumi na kijamii.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.