Habari za Punde

Rais Dk Shein awataka vijana kuonesha nidhamu na maadili ya hali ya juu alipozindua mashindano ya Majimbo


 
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                         24.03.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amezindua mashindano ya Mpira wa miguu ‘Majimbo Cup’ na kuwataka vijana wanaoshiriki mashindano hayo kucheza kwa maadili na nidhamu kama kilivyo chama chao cha CCM.

Uzinduzi huo umefanyika katika uwanja wa Amaan mjini Zanzibar ikiwa ni maadhimisho ya mwaka mmoja tokea kuapishwa kwa Dk. Shein kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kufuatia ushindi wa kishindo alioupata katika uchaguzi mkuu uliopita na kuweza kuendelea katika kipindi cha pili cha uongozi wake ambapo timu zilizofungua dimba ya mashindano hayo ni Mfenesini na Mpendae

Akitoa salamu zake katika uzinduzi huo, Dk. Shein alitoa pongezi kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa mchango wao mkubwa waliotoa kwa Majimbo yao kwa lengo la kuendeleza mashindano hayo.

Dk. Shein alitoa pongezi zake kwa wale wote waliochangia na kusimamia mashindano hayo ikiwemo Kamati maalum iliyoundwa kuendesha mashindano hayo, viongozi, Mwenyekiti wa Kamati pamoja na Mwakilishi wa Uzini Mohammed Raza kwa kuyafadhili mashindano hayo.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Wawakilishi wa Majimbo yote ya Pemba na wale wa viti maalum kwa mchango wao wa Tsh. Milioni 12 kwa ajili ya mashindano kama hayo yatakayofanyika katika majimbo kisiwani humo.

Dk. Shein ambaye pia, ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar alisisitiza kuwa mashindano hayo pia ni mwendelezo wa maadhimisho ya miaka 40 tokea kuzaliwa kwa CCM.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza imani yake kubwa kuwa mashindano hayo yataenda vizuri kutokana na mazingira mazuri ya uwanja wa Amaan unaochezewa mashindano hayo pamoja na kukamilika vyema kwa maandalizi yake.

Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi alitoa pongezi kwa niaba ya wanaCCM na wale wote wapenda amani kwa Rais Dk. Shein kwa kutimiza mwaka mmoja tokea kuchaguliwa tena na wananchi kuiongoza Zanzibar katika uchaguzi uliopita.

Mabodi alisisitiza kuwa michezo ni afya, amani, upendo na kustahamiliana hivyo, alieleza haja kwa timu zote kucheza vyema mashindano hayo ili kufikia lengo lililokusudiwa.

Mapema Mwenyekiti wa mashindano hayo ambaye pia, ni Waziri wa Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo Rashid Ali Khamis alitoa pongezi kwa Kamati ya mashindano hayo ambayo itasimamia mashindano hayo hadi tamati ya mashindano.

Hadi mwisho wa mtanange huo wa uzinduzi wa mashindano hayo kati ya Mfenesini na Mpendae, timu ya Mfenesini ilitoka kidedea kwa kushinda magoli mawili katika kipindi cha pili cha mchezo huo magoli ambayo yote yalifungwa na mshambuliaji machachari Ali Seif Bausi na Mpendae haikupata kitu.

Viongozi mbali mbali, wa chama na Serikali, wanaCCM na wananchi kutoka maeneo mbali mbali ya Zanzibar walihudhuria katika mashindano hayo ambapo mapema Wanamichezo wakiongozwa na Brass Band waliingia uwanjani hapo na kupita mbele ya Mgeni Rasmin Dk. Ali Mohamed Shein.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.