Habari za Punde

Zanzibar yaadhimisha siku ya kifua kikuu duniani kwa kongamano la wanafunzi wa vyuo vikuu

 Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Riziki Pembe Juma akifungua Kongamano la maadhimisho ya siku ya Kifua kikuu Duniani katika ukumbi wa sanaa Rahaleo (kulia) mwakilishi wa WHO Zanzibar Dkt. Ghirman  na (kushoto) Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. Jamala Taib.
 Mratibu kitengo cha ufuatiliaji na tathmini mwenendo wa maradhi ya Ukimwi, Kifua Kikuu na Ukoma Zanzibar Asha Ussi Khamis akitoa mada yake ya matokeo ya utafiti juu ya uelewa, tabia na matendo juu ya kifua kikuu Zanzibar katika ukumbi wa sanaa Rahaleo Mjini Zanzibar.

 Baadhi ya wanafunzi wa vyuo vikuu walioshiriki Kongamano la maadhimisho ya siku ya Kifua kikuu Duniani katika Ukumbi wa sanaa Rahaleo wakimsikiliza Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali alipokuwa akifungua Kongamano hilo.

Mmoja wawashiriki wa kongamano la kuadhimisha siku ya Kifua kikuu Duniani kutoka Skuli ya Afya na Sayansi ya Tiba (SUZA) Mariam Ali Mansour  akichangia moja ya mada zilizowasilishwa.
Picha na Makame Mshenga-Maelezo.    

Na Ramadhani Ali/Maelezo Zanzibar    
                               
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma amewataka vijana wasomi kujikita katika kufanya tafiti mbali mbali ili kupata majibu sahihi ya matatizo yanyoikabili nchi ikiwemo maradhi.

Amesema yapo matatizo mengi yanayoikabili jamii ya Zanzibar na yanahitaji majibu ya kisayansi ili kusaidia kupiga hatua katika kufikia maendeleo.

Waziri Riziki alieleza hayo alipokuwa akifungua kongamano la maadhimisho ya siku ya Kifua Kikuu Duniani lililowashirikisha wanafunzi wa Vyuo vikuu Zanzibar katika Ukumbi wa Wasanii Rahaleo

Alisema maradhi ya kifua kikuu ni miongoni mwa maradhi hatari duniani na kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya (WHO) mwaka 2015 watu milioni 10.4 waliugua ambapo milioni 1.8 walifariki.

Aliitaja Tanzania kuwa ni miongoni mwa nchi 30 Duniani zinazoongoza kwa maradhi ya kifua kikuu hivyo juhudi zaidi zinahitajika katika kukabiliana na maradhi hayo.

Waziri Riziki ambae pia ni Kaimu Waziri wa Afya alisema hali sio nzuri pia kwa Zanzibar na watu 700 hadi 800 wanaugua kifua kikuu kila mwaka na baadhi yao hupoteza maisha.

Alizitaja dalili za maradhi ya Kifua kikuu kuwa ni kukohoa kwa kipindi kirefu, kutoa makohozi yenye damu, homa za mara kwa mara hasa wakati wa jioni, kutokwa na jasho jingi wakati wa usiku, kukosa hamu ya kula na hatimae kupungua uzito.

Aliwashauri wananchi wasisite kufika katika vituo vya afya wanapoona dalili hizo ili kupata matibabu katika hatua za awali kwani maradhi hayo yanatibika kwa urahisi na dawa zake zinapatikana bila malipo.

Alisema miongoni mwa sababu zinazopelekea kupata maradhi hayo ni msongamano wa watu hasa sehemu za mijini ujenzi holela wa nyumba za kuishi kwa vile maradhi hayo yanaambukizwa kwa njia ya hewa.

Akitoa salamu za Shirika la Afya Duniani (WHO), Mwakilishi wa Shirika hilo Zanzibar Dkt. Ghirman Andermichael alisema kifua kikuu ni janga la Dunia hivyo kila mmoja anawajibu wa kushiriki katika kuhakikisha  maradhi hayo yanapungua kwa asilimia 30 ifikapo mwaka 2025.

Baadhi ya wanafunzi walioshiriki Kongamano hilo waliishauri Wizara ya Afya kuandaa wataalamu na vifaa vya kutosha vya kuchunguza maradhi hayo katika Hospitali na vituo vikubwa vya Afya.

Dunia huadhimisha siku ya Kifua kikuu kila ifikapo Machi 24  na kaulimbiu ya maadhimisho hayo mwaka huu ni Kifua kikuu ni janga la Taifa. Tuungane kutokomeza Kifua kikuu. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.