Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Shein Ameondoka Leo Kulekea Nchini Indonesia Kuhudhuria Mkutano waKwanza wa Wakuu wa Nchi na Serikali za Jumuiya ya Nchi Zinazopakana na Bahari ya Hindi (IORA)

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                            04.03.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein anaondoka nchini leo kwenda nchini Indonesia kumuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli katika Mkutano wa Kwanza wa Wakuu wa nchi na Serikali wa Jumuiya ya nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi (IORA)

Mkutano huo wa siku tatu unatarajiwa kuanza Jumaapili ya tarehe 05 Machi na kumalizikia tarehe 07 Machi mwaka huu, mjini Jakarta Indonesia ambao utatanguliwa na vikao vya Mawaziri na wadau wengine kutoka nchi wanachama wa Jumuiya hiyo ya nchi zinazopakana na Bahari ya Hindi (IORA).

Malengo ya mkutano huo ni kuendeleza ushirikiano baina ya nchi wanachama kupitia maeneo ya vipaumbele ambavyo ni Biashara na Uwekezaji, Usafiri wa Bahari, Uvuvi, Menejimenti ya Udhibiti wa Majanga, Taaluma, Sayansi na Teknolojia, Utalii na Utamaduni ambapo mada mbali mbali zitajadiliwa.

Pamoja na vipaumbele hivyo, hivi karibuni Jumuiya imeongeza maeneo mawili mtambuka ambayo ni Uchumi wa Bahari na masuala ya Jinsia na Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi.
Mbali ya kuhudhuria mkutano huo, Dk. Shein atashiriki katika utiaji saini wa Mkataba unaoainisha mikakati, mipango na maazimio yanayolenga kuongeza kasi ya maendeleo ya Jumuiya hiyo kwa kuanisha mafanikio na changamoto zake.

Miongoni wa Wajumbe wanaofuatana na Rais Dk. Shein katika mkutano huo, ni Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein, Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko, Balozi Amina Salum Ali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa, Haji Ussi Gavu, Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Hamad Rashid Mohammed, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afika Mashariki, Dk. Susan Alphonce Kolimba.

Wengine ni  Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhani Muombwa Mwinyi na Mshauri wa Rais Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Uchumi na Uwekezaji Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa pamoja na watendaji wengine wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar. 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein anatarajiwa kurejea nchi tarehe 9 Machi, 2017.

Katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume Dk. Shein aliagwa na viongozi mbali mbali wa Serikali, Vikosi vya Ulinzi na Usalama pamoja na viongozi wa vyama vya siasa wakiongozwa na Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.