STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 04.03.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein anaondoka nchini leo kwenda nchini Indonesia kumuwakilisha
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli katika Mkutano
wa Kwanza wa Wakuu wa nchi na Serikali wa Jumuiya ya nchi zinazopakana na
Bahari ya Hindi (IORA)
Mkutano huo wa siku tatu
unatarajiwa kuanza Jumaapili ya tarehe 05 Machi na kumalizikia tarehe 07 Machi
mwaka huu, mjini Jakarta Indonesia ambao utatanguliwa na vikao vya Mawaziri na
wadau wengine kutoka nchi wanachama wa Jumuiya hiyo ya nchi zinazopakana na Bahari
ya Hindi (IORA).
Malengo ya mkutano huo
ni kuendeleza ushirikiano baina ya nchi wanachama kupitia maeneo ya vipaumbele
ambavyo ni Biashara na Uwekezaji, Usafiri wa Bahari, Uvuvi, Menejimenti ya
Udhibiti wa Majanga, Taaluma, Sayansi na Teknolojia, Utalii na Utamaduni ambapo
mada mbali mbali zitajadiliwa.
Pamoja na vipaumbele
hivyo, hivi karibuni Jumuiya imeongeza maeneo mawili mtambuka ambayo ni Uchumi
wa Bahari na masuala ya Jinsia na Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi.
Mbali
ya kuhudhuria mkutano huo, Dk. Shein atashiriki katika utiaji saini wa Mkataba
unaoainisha mikakati, mipango na maazimio yanayolenga kuongeza kasi ya
maendeleo ya Jumuiya hiyo kwa kuanisha mafanikio na changamoto zake.
Miongoni
wa Wajumbe wanaofuatana na Rais Dk. Shein katika mkutano huo, ni Mke wa Rais wa
Zanzibar Mama Mwanamwema Shein, Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko, Balozi
Amina Salum Ali, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Issa, Haji Ussi Gavu, Waziri wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi,
Hamad Rashid Mohammed, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afika
Mashariki, Dk. Susan Alphonce Kolimba.
Wengine
ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Mambo ya
Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Ramadhani Muombwa Mwinyi na
Mshauri wa Rais Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Uchumi na Uwekezaji Balozi
Mohamed Ramia Abdiwawa pamoja na watendaji wengine wa Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein anatarajiwa
kurejea nchi tarehe 9 Machi, 2017.
Katika
uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume Dk. Shein aliagwa na viongozi
mbali mbali wa Serikali, Vikosi vya Ulinzi na Usalama pamoja na viongozi wa
vyama vya siasa wakiongozwa na Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment