Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Azungumza na Balozi wa Iran Ikulu Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                               12.05.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amepongeza azma ya Serikali ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ya kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta za maendeleo kwa lengo la kukuza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya pande mbili hizo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika mazungumzo kati yake na Balozi mpya wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Moussa Ahmed Farhang, mazungumzo yaliofanyika Ikulu mjini Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alipongeza juhudi za nchi hiyo za kuendeleza ushirikiano na uhusiano mwema uliopo ambao una historia na kuihakikishi nchi hiyo kuwa Zanzibar utaudumisha.

Dk. Shein alisema kuwa kuna haja ya kuendelea kuitunza na kuiimarisha historia iliyopo kati ya Iran na Zanzibar kwani watu wa Zanzibar wanafahamu fika uhusiano huo ambao Mabalozi wote waliofanya kazi kabla ya Balozi Farhang waliuendeleza.

Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza miongoni mwa mambo muhimu ikiwemo miradi ya maendeleo ambayo Iran imeisaidia Zanzibar ikiwemo kuendeleza elimu ya amali kwa kusaidia vifaa, fedha taslim, nafasi za masomo ya elimu ya juu, nafasi za mafunzo ya utaalamu ya muda mfupi kwa ajili ya walimu wa elimu ya vyuo vya amali.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar bado ina matumaini makubwa ya azma na ahadi ya  Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kukiimarisha kituo cha Afya cha Mbuzini, kilichopo Wilaya ya Mgharibi A.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa bado Zanzibar ina kumbuka ahadi ya Serikali ya Iran ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika ujenzi wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), ambapo tayari Serikali imeshakijenga na kukiendeleza chuo hicho.

Dk. Shein Shein pia, alimueleza Balozi   Farhang haja ya kushirikiana katika suala zima la utafiti pamoja na masuala mengine ya kisayansi.

“Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ikiwemo Zanzibar iko tayari kufanya kazi na kuendeleza uhusiano na ushirikiano wake na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa maslahi ya nchi zetu na watu wake”,alisema Dk. Shein.

Aidha, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano kati yake na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ikiwa ni pamoja na kulifanyia kazi wazo la kuunda timu ya watendaji ambayo itaweza kubadilishana uzoefu, utaalamu pamoja na kuyafanyia kazi mambo yatakayokubaliwa kimashirikiano kati ya pande mbili hizo.

Nae Balozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Moussa Ahmad  Farhang alimuhakikishia Dk. Shein kuwa nchi yake itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuendeleza na kuimarisha sekta za maendeleo, uchumi na za kijamii.

Balozi Farhang alimueleza Dk. Shein kuwa Iran inaithamini sana Zanzibar pamoja na watu wake kwani nchi hiyo ina kumbukumbu nyingi za Zanzibar na jinsi watu wake walivyokuwa wakishirikiana pamoja na Serikali zao miaka mingi iliyopita.

Alieleza kuwa Serikali ya Iran iko tayari kuendeleza ujenzi wa Hospitali ya Mbuzini na hivi sasa imo katika kusubiri taratibu za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia wizara husika zikamilike ili ujenzi huo uanze kwani tayari fedha zake zipo kiasi cha Dola laki 5.

Aliongeza kuwa Serikali ya Iran inakumbuka jinsi Zanzibar ilivyoiunga mkono na kuisaida nchi hiyo wakati ilipowekewa vikwazo, na hivyo haina malipo ya kuilipa Zanzibar bali ni kuendeleza na kuimarisha ushrikiano na uhusiano wake kwa Zanzibar.

Balozi Farhang aliieleza matumaini makubwa ya Iran kuwa Zanzibar itaendelea kupata mafanikio zaidi ya kiuchumi, kijamii na kiutamaduni huku akiahidi Iran kuleta walimu kwa ajili ya kutoa mafunzo ya walimu wa vyuo vya amali vya Zanzibar.

Hata hivyo, kiongozi huyo alipongeza hatua za kuimarisha ushirikiano kwa kutembeleana kati ya viongozi wa pande mbili hizo na kutoa wazo la viongozi kuunda timu kwa ajili ya mashirikiano ya pamoja kati ya Iran na Zanzibar huku akihadi nchi yake kuunga mkono na kutekeleza vipaumbe vya Zanzibar.

Sambamba na hayo, Balozi huyo alimueleza Dk. Shein kuwa umbali uliopo kati ya Iran na Zanzibar sio sababu ya nchi yake kutoshirikiana na Zanzibar na kumuahidi kuwa ushirikiano uliopo utadumishwa huku akitumia fursa hiyo kupongeza amani na utulivu iliyopo Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein ambayo ndio chachu ya maendeleo yaliopo.

Balozi Farhang pia, alitumia fursa hiyo kumpa Dk. Shein salamu za Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Rais Hassan Rouhani za kumtakia uongozi mwema ambapo Dk. Shein nae alipokea salamu hizo kwa furaha na kwa upande wake alimpa Balozi huyo salamu zake kwa kiongozi huyo wa Iran.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.