Habari za Punde

Waziri Aboud Azungumza na Kamati ya Uongozi.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Mohamed Aboud Mohamed akizungumza na Kamati ya Uongozi ya  Ofisi yake alipokutana nayo kujadili utekelezaji wa Maagizo ya Baraza la Mapinduzi Zanzibar.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar akisisitiza jambo wakati akikiendesha Kikao cha Kamati ya Uongozi wa Ofisi yake  kwenye Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi hiyo uliopo Vuga Mjini Zanzibar.
Baadhi ya Viongozi na Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar wakiwa katika kikao cha kujadili maagizo ya Baraza la Mapinduzi.
Baadhi ya Viongozi na Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar wakiwa katika kikao cha kujadili maagizo ya Baraza la Mapinduzi.
(Picha na OMPR)
Na Othman Khamis OMPR. 
Viongozi wa Taasisi za Umma wametahadharisha kujiepusha na taratibu  zinazopelekea kulipwa mishahara Watumishi hewa, wale waliostaafu pamoja na watumishi wanaokwenda masomoni nje ya Nchi na kutorejea Nchini, kwani kufanya hivyo ni kwenda kinyume na kanuzi na taratibu za Utumishi Serikalini.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Mohamed  Aboud Mohamed alitoa tahadhari hiyo wakati akizungumza na Kamati ya Uongozi ya Ofisi yake kwenye Ukumbi wa Ofisi hiyo Vuga Mjini Zanzibar.

Waziri Mohamed Aboud alionya kwamba Kiongozi wa Taasisi ya Umma atakayebainika kuendelea kusimamia udhaifu huo unaocheche ya kuitia hasara Serikali Kuu ataanza kuwajibika yeye kwanza.

Alisema Kiongozi ndie dhamama  kwa watumishi anaowaongoza na kuwakumbusha Watumishi wote lazima wazingatie kujenga misingi ya nidhamu na uadilifu katika utumishi wao wa kuhudumia Jamii inayowazunguuka.

Aliwataka Viongozi wa Kamati hiyo wa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar pamoja na Taasisi nyengine kuhakikisha kwamba zinaepuka kuwa na Wafanyakazi Hewa licha ya kwamba zipo baadhi ya Taasisi zimeonyesha dalili ya kuwa na watendaji hewa.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwapongeza Viongozi hao wa Kamati ya Uongozi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  kwa usimamizi wao mzuri uliopelekea  kuepuka kuwa na taratibu za kulea watendaji hewa.

Alisema  Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar inatakiwa kuwa kioo na mfano kwa Wizara na Taasisi nyengine za Umma katika kuratibu masuala ya utendaji wa uratibu wa shughuli za Serikali za kila siku.

Akizungumzia suala la  Dawa za kulevya ambazo Serikali zote mbili zimeamua kupambana nalo kwa nguvu zote Waziri Aboud alisema Serikali imeridhia kuanzishwa kwa nyumba za kurekebishia tabia  kwa Vijana waliotumbikia katika matumizi ya dawa hizo.

Hata hivyo Waziri Aboud  alisema lengo la nyumba hizo ni kuunda tabia nzuri kwa Vijana waliopotea licha ya baadhi ya nyumba hizo kukiuka taratibu zilizowekwa na kupelekea SerikalI Kuu kuchukuwa hatua za kuzifungia baadhi yake.

Kuhusu  mvua za masika zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbali mmbali Nchini Mheshimwa Mohamed Aboud Mohamed  alisema athari za mvua hizo tayari zimeanza kujitokeza katika baadhi ya maeneo yenye kiwango kikubwa cha mvua hizo.

Waziri Aboud  aliiagiza Mamlaka ya Kukabiliana na Maafa Zanzibar kuratibu matukio yote yanayosababishwa na athari za Mvua hizo ili baadae Serikali Kuu iweze kutoa Taarifa rasmi kwa Umma juu ya matukio yote yanayoripotiwa yakitokana na kusababishwa na Mvua hizo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.