Habari za Punde

THBUB Yalaani Watu Wenye Ulemavu Kupigwa na Kudhalilishwa.

-
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
Kitalu Na. 8, Mtaa wa Luthuli
S.L.P 2643, DAR ES SALAAM
Simu: +255 22 2135747/8; 2137125; 2135222
Faksi: +255 22 2111281
Tovuti: www.chragg.go.tz

Juni 19, 2017
                                                                                                       
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

THBUB yalaani watu wenye ulemavu kupigwa na kudhalilishwa

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imepokea taarifa zinazohusu askari polisi kuwapiga na kudhalilisha watu wenye ulemavu katika tukio lililotokea asubuhi ya Juni 16, 2017, Mtaa wa Sokoine jijini Dar es Salaam.
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora imefuatilia tukio hilo kwa kuzungumza na viongozi wa walemavu na mamlaka husika, hususani Mkurugenzi wa Manispaa ya Ilala, Dar es Salaam na kuelezwa kuwa mnamo tarehe 16 Juni 2017 watu wenye ulemavu wapatao 200 wakiwa na vyombo vya moto, vijulikanavyo kama “bajaji”, waliziba barabara ya Sokoine kwa madai ya kutaka Mkurugenzi asikilize madai yao yahusuyo wenzao kukamatwa kwa kuendesha vyombo vyao bila kufuata taratibu za sheria.

Taarifa za vyombo vya habari na mitandao ya kijamii zilionyesha askari wa Jeshi la Polisi wakiwapiga watu hao wenye ulemavu.

Pamoja na kwamba watu wenye ulemavu walikiuka taratibu za sheria,
ni wazi kwamba wakati wa kuzuia uvunjifu huo wa sheria, kulikuwa na vitendo vya ukatili na udhalilishaji dhidi ya watu hao wenye ulemavu wakati wakikamatwa na kuingizwa kwenye magari.

Haki ya usawa mbele ya sheria kama ilivyo kwa haki nyingine, inalindwa kisheria na hakuna mtu anayepaswa kuvunjiwa haki zake wakati wa kutekeleza sheria. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) Ibara ya 13 (6) (e) ni marufuku kwa mtu kuteswa, kuadhibiwa kinyama au kupewa adhabu zinazomtweza au kumdhalilisha. Haki hizi pia zimeainishwa ndani ya mikataba mbalimbali ya kimataifa na kikanda ambayo Tanzania imeridhia.

Tume inapenda kulikumbusha Jeshi la Polisi kwamba kukimbilia kuwapiga raia kila wanapoonekana kukinzana na sheria ni matumizi mabaya ya madaraka yao. Ni wajibu wa polisi kulinda usalama wa raia bila kuwadhalilisha, kuwatesa na kuwapiga. Matumizi ya nguvu kupita kiasi wakati wa kutekeleza sheria ni uvunjifu wa sheria.

Pamoja na uvunjifu wa sheria uliotendwa na watu wenye ulemavu siku ya tarehe 16 Juni, 2017, kitendo cha kuwapiga bila kuwapa muda wa kutawanyika, au kutoa hoja za malalamiko yao kupitia kwa wawakilishi wao ni kitendo cha kuwadhalilisha.

Hivyo basi, Tume inatoa wito kwa Jeshi la Polisi:
1.   Kuzingatia kanuni, sheria, haki za binadamu na misingi ya utawala bora katika utekelezaji wa majukumu yake ya kila siku.
2.   Kuwapatia mafunzo ya mara kwa mara askari polisi na maafisa wake kuhusu haki za binadamu na misingi ya utawala bora. Wakati wa kuratibu  na kushughulikia masuala ya maandamano na mikusanyiko ya raia.
 3.   Kuhakikisha kuwa maafisa na askari wake hawatumii nguvu kupita kiasi wawapo katika operesheni zinazohusu raia waliokusanyika kwa amani, na hususan watu wenye ulemavu, ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza.
 4.   Mwisho, Tume inatoa wito kwa raia kwa ujumla, wakiwemo watu wenye ulemavu, kwamba hamna mwananchi au mtu yeyote aliye juu ya sheria, na kwamba njia bora ya kutatua kero au matatizo yanayowakuta wananchi wakidai haki zao ni kwa kufuata taratibu za sheria. Kwa hivyo, viongozi wa watu wenye ulemavu wafuate taratibu hizo kufikisha hoja zao kwenye vyombo na mamlaka husika na siyo vinginevyo.
 Imetolewa na:
(SIGNED)

Bahame Tom Nyanduga
Mwenyekiti

TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA

Juni 19, 2017


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.