Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                 20.08.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewataka viongozi wa Majimbo wakiwemo Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kuwaeleza wananchi juhudi zinazochukuliwa na Serikali yao katika kuwapelekea huduma za maendeleo ikiwemo huduma ya maji safi na salama.

Dk. Shein aliyasema hayo leo mara baada ya kukagua kisima cha maji ikiwa ni miongoni mwa visima 8 vilivyopo katika kijiji cha Bumbwisudi, Wilaya ya Magharibi, Mkoa wa Mjini Magharibi, kisima hicho ni kisima kikubwa kati ya visima vya hapa nchini ambacho kinatoa maji mengi lita zaidi ya laki2 kwa saa.

Dk. Shein alieleza kuwa ni vyema Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi nao wakatumia fursa ya kuweleza wananchi juhudi za Serikali kwani baadhi yao hawazijui juhudi hizo, kwani kazi kubwa inafanywa na Serikali yao katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma ya maji safi na salama Unguja na Pemba.

Alieleza kuwa mbali ya mradi huo ambao una visima tisa ambavyo 8 kati ya hivyo viko katika eneo hilo la Bumbwisudi pia, kuna miradi mingi ikiwemo ule wa JICA, ule ambao fedha kutoka Serikali ya India na mengineyo, juhudi zote hizo ni kuhakikisha changamoto ya huduma ya maji inapatiwa ufumbuzi katika kipindi kifupi kijacho.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), Dk. Mustafa Ali Garu alimueleza Dk. Shein kuwa kisima hicho ndicho kisima kikubwa kilicho na uwezo wa kutoa maji mengi kupeleka katika kituo cha Welezo na hatimae kupeleka katika mji wa Zanzibar ambapo kwa hivi sasa hatua inayoendelea ni kuweka pampu.

Alisema kuwa katika eneo hilo la Bumbwisudi pekee yake pamechimba visima vinane na cha tisa kimechimbwa huko Mwembemchomeke mbali na visima vyengine 4 vya zamani na kulifanya eneo hilo la Bumbwisudi peke yake kuwa na visima 12.

Meneja wa Mradi huo Aboozar Sadeghi alimueleza Dk. Shein kuwa Mradi huo unatarajiwa kukamilika Januari mwakani.

Wakati huo huo, Dk. Shein aliweka jiwe la msingi Tawi la CCM Bumbwisudi alipongeza juhudi za wanaCCM pamoja na viongozi wao wa Jimbo kwa kujenga jengo hilo jipya la Tawi na kueleza kuwa hatua hiyo ni miongoni mwa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 ambayo yeye chini ya chama hicho anaisimamia.

Dk. Shein ambaye pia, ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar aliwaeleza wanaCCM hao kuwa kazi iliyombele yao hivi sasa ni kutekeleza ahadi walizoziahidi katika  Ilani hiyo yab Uchaguzi huku wakihakikisha wanakilinda chama chao sambamba na kuyalinda Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964.

Makamo huyo wa CCM Zanzibar alitoa wito kwa wanaCCM kuwa wamoja na kushirikiana kwa pamoja ili kukiimarisha chama chao ambacho hakitakiwa kuwa na makundi kwani tokea zama za  cha ASP kulikuwa hakuna makundi.

Mapema Dk. Shein aliliwekea jiwe la msingi jengo jipya la skuli ya Msingi Kihinani katika  Jimbo la Mfenesini na baadae aliwahutubia wananchi wakiwemo wanafunzi wa skuli hiyo na kuwaeleza azma ya Serikali anayoiongoza katika kuendeleza ujenzi wa madarasa mapya ya skuli za Zanzibar pamoja na thamani yakiwemo madawati kwa mashirikiano ya wananchi na viongozi wao.

Alieleza kuwa katika kuhakikisha changamoto ya upungufu wa madawati inapatiwa ufumbuzi tayari TZS Bilioni 4 kwa awamu ya kwanza zimeshakusanywa kwa ajili ya ununuzi wa madawati na baadae awamu ya pili itafuata hiyo yote ni kwa kutambua kuwa elimu ndio ufunguo wa maisha na nyenzo kubwa katika maisha ya mwanaadamu.

Alitumia fursa hiyo kutoa pongezi maalum kwa wanafunzi wa kike ambao ni wengi katika skuli hiyo na kuwaeleza kuwa juhudi wanazozichukua ni muhimu katika kuwaletea maendeleo wao wenyewe na nchi yao kwani katika kipindi cha hivi karibuni wanafunzi wa kike wamekuwa wakifanya vizuri katika masomo yao hasa ya sayansi.

Pamoja na hayo, Dk. Shein aliwaeleza wananchi pamoja na wananfunzi waliohudhuria katika hafla hiyo kuwa mafanikio yote yaliopatikana katika sekta ya elimu yanatokana azma ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 chini ya jemedari Marehemu Mzee Abeid Amani karume ambae alitangaza elimu bure.

Akieleza historia ya elimu hapa nchini kabla ya Mapinduzi Dk. Shein alisema kuwa wanyonge katika kipindi hicho walikuwa hawapati elimu kwani haikuwa rahisi na walitakiwa kulipa fedha ambazo hawakuzimudu.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Khadija  Bakari alieleza kuwa jumla ya TZS milioni 24 zimetumika katika ujenzi wa madarasa hayo 4 ambazo ni michango ya wananchi na Serikali imetoa TZS milioni 45, huku akieleza azma ya Wizara yake kuzimaliza skuli 288 zilizoanza kujengwa na wananchi katika Bajeti yao ya mwaka huu.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.