Habari za Punde

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                 19.08.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechukua uwamuzi wa makusudi kukiunganisha Chuo cha Maendeleo ya Utalii Maruhubi kuwa ni Tawi la Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA), ili chuo hicho kizidi kupata hadhi na kutambulikana Kitaifa na Kimataifa.

Dk. Shein aliyasema hayo leo mara baada ya kuweka jiwe la msingi jengo la Chuo Cha Utalii, kilichopo Maruhubi mjini Unguja ambacho kwa hivi sasa chuo hicho ni Tawi la Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA).

Akiwahutubia wanafunzi wa Chuo nje ya jengo hilo jipya la Chuo cha Maendeleo ya Utalii, Dk. Shein alisema kuwa kwa vile jengo hilo tayari limeshafikia asilimia 50 ya ujenzi kunatoa matumaini makubwa katika kukamilisha mradi huo mkubwa ambao utazidisha azma ya Serikali anayoiongoza katika kuimarisha sekta ya utalii.

Aliongeza kuwa hatua hiyo unakipa hadhi na sifa kubwa chuo hicho ambacho kwa siku za mbele kitaweza kujiendesha wenyewe na kuwa Chuo Kikuu cha Utalii kwani vyuo vingi vilianza hivyio na kutolea mfano Chuo Kikuu cha Muhimbili na kile cha Sokoine Morogoro ambavyo vilikuwa ni Matawi la Chuo Kikuu cha Dar-es-Salaam.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa lengo kubwa la Serikali katika kuchukua juhudi hizo ni kutaka vijana wake wasome na kusisitiza kuwa kazi hiyo kubwa ilibuniwa na Chama Cha Mapinduzi CCM katika Ilani yake ya Uchaguzi.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza umuhimu wa sekta ya utalii hapa Zanzibar ambao umekuwa ukichangia kwa kiasi kikubwa uchumi wa Zanzibar kwa kuingiza fedha za kigeni kwa asilimia 80 na kuchangia pato la Taifa kwa asilimia 27.

Alieleza kuwa jina la Zanzibar linajiuza kutokana na utalii  na kuwaeleza wanafunzi hao kuwa hawajakosea kuingia katika kada hiyo ya elimu.

Akitoa maelezo kwa Rais wa Zanzibar Dk. Shein, Meneja Mkuu wa Mradi wa ujenzi huo Yusuph Msafiri Mlimakifi alieleza kuwa  ujenzi huo una eneo la mita 5000 na utakuwa wa ghorofa tatu na unatarajiwa kugharimu TZS Bilioni 5.2 ambao mradi ho ni mashirikiano kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB).

Mhandisi huyo alieleza kuwa tayari asilimia 50 za ujenzi huo zimeshafikiwa na matarajio kumalizika kwake ni Disemba mwaka huu huku akieleza kuwa mbali ya jingo hilo kusaidia katika kutoa mafunzo kwa chuo hicho pia litakuwa ni eneo la biashara kwa chuo hicho.

Alieleza kuwa jengo hilo litakuwa na ukumbi  wa mikutano ambao utakuwa na ukubwa wa kuingiza watu wapatao 400, mkahawa utakaochukua watu 400 ambao utakaokuwa wazi wakati wote, ukumbi wa kusomeshea utakaochukuwa wanafunzi 150, jiko la kisasa la kufundishia na kwa shughuli za biashara pamoja na vyumba 9 vya kulaa vyenye sifa ya Hoteli ya nyota 4.

Wabunifu na Wasimamizi wa ujenzi wa jengo hilo ni  Kampuni ya Onspace Consult kutoka Dar-es-Salaam na mjenzi ni Kampuni ya Humphrey kutoka Arusha.

Mapema Dk. Shein alifika eneo la Kilimani mjini Unguja kwa ajili ya kukagua mradi wa upandaji wa Mikoko pamoja na Ujenzi wa Matuta ya kuzuia Mmongonyoko wa fukwe na kupongeza kwa hatua zilizofikiwa katika kuendeleza miradi hiyo ya ujenzi.

Akipata maelezo kutoka kwa Katibu wa Taasisi ya ZACEDY Jamali Khamis alisema kuwa mradi wa upandaji wa mikoko ni mwa mwaka mmoja na mikoko inayopandwa ni ile ya aina ya mchu ambayo ndio inayokubali katika eneo hilo.

Alisema kuwa mradi huo utasaidia katika kupambana na mabadiliko ya tabia nchi katika eneo hilo la kilimani na tayari wameshapanda 35,000 ambapo changamoto kubwa wanayoipata ni kuwa bado jamii haijaona umhimu wa mradi huo hivyo kuna haja ya kuelemishwa kwani kuna baadhi ya watu hupita katika maeneeo hayo wanayopanda mikoko ambayo bado ni michanga licha ya kuwashirikisha wananchi katika mradi huo.

Nae Meneja Mkuu wa Mradi wa ujenzi wa Matuta ya kuzuia mmongonyoko wa fukwe Bernard Odhuno alieleza kuwa mradi huo unaendelea vizuri na wanatarajia kujenga matuta 5 katika eneo hilo kwa ajili ya kuzuia mmongonyoko huo na wanatarajia kumaliza mnamo mwezi wa Novemba mwaka huu.

Alisema kuwa tayari mradi kama huo wameshaukamilisha  huko Kisiwa Panza kisiwani Pemba ambapo alieleza kuwa mradi huo uko chini ya Ofisi ya Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Usaidizi wa Miradi (UNOPS).

Wakati huo huo, Dk. Shein alilifungua Tawi la CCM la Muembe Matarumbeta katika Jimbo la Jangombe na kupongeza ujenzi huo wa tawi la kisasa huku akisisitiza haja kwa wanaCCM kuendelea kukitumikia chama chao.

Dk. Shein ambaye pia ni Makamo Mwenyekiti wa CCM  Zanzibar alieleza kuwa tawi hilo litawasaidia kwa kiasi kikubwa wanaCCM katika kufanya shughuli zao  wkani Tawi ndio kiini cha siasa ya chama hicho kwani ni lazima litumike katika kufanya kazi za chama.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza matumaini yake kwa viongozi wa Jimbo hilo kuwa karibu na wanachama wa chama hicho kutokana na kuwemo kwa Ofisi zao ndani ya Tawi hilo.

Mapema Dk. Shein alipokea taarifa ya Mkoa huko ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani, Kikwajuni  mjini Unguja na baada ya kusomwa taarifa hiyo na Mkuu wa Mkoa Ayoub Mohammed, Dk. Shein alieleza umhimu wa kuhakikisha yale yote yalioahidiwa na CCM yanatekelezwa, hivyo ziara yake hiyo imekusudia kwenda kushuhudia azma hiyo.

Aliongeza kuwa matumaini yake makubwa kuwa utekelezaji wa Ilani ya Uchgauzi ya mwaka 2015-2020 itavuka asilimia 95 zilizofikiwa katika utekelezajiw a mwaka 2010-2015.

Dk. Shein, pia, alitumia fursa kurejea kauli yake ya kuwataka Mawaziri wote wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kushiriki ziara hiyo isipokuwa wale wenye shughuli maalum ambao wamemtaarifu kwani hiyo ni ziara ya kazi na si ya mchezo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.