Habari za Punde

Wafanyakazi Jumia Wafanya Matembezi ya Hisani Kuchangia Fedha Kusaidia Jamii.

Na Jumia Travel Tanzania
Ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya miaka mitano tangu Jumia ianze kufanya shughuli zake barani Afrika, wafanyakazi wa kampuni wamefanya matembezi ya hisani ili kuchangisha fedha kusaidia jamii inayowazunguka.
Matembezi hayo ambayo yalifanyika mwishoni mwa wiki iliyopita yaliwahusisha wafanyakazi wote wa kampuni ya Jumia nchini Tanzania kama vile Jumia Travel, Jumia Market, Jumia Food, Jumia Deals, Jumia Cars na Jumia House.

Akizungumzia juu ya tukio hilo Meneja wa Rasilimali Watu wa Jumia Tanzania, Bi. Poonam Divecha amebainisha kuwa matembezi hayo ni sehemu ya kukamilisha shamrashamra za maadhimisho ya miaka mitano tangu kampuni hiyo ianze kuwahudumia watanzania katika Nyanja ya huduma mbalimbali kwa njia ya mtandao.

“Miaka mitano ni mingi katika utoaji wa huduma hususani kwenye sekta mpya ambayo ina changamoto kadhaa ndani yake. Lakini tusingefikia hapa bila ya uungwaji mkono kutoka kwa watanzania ambao ndio wateja wetu na pia kujitoa kwa wafanyakazi wa Jumia katika kuhakikisha inafanya mapinduzi ya utoaji wa huduma. Katika utoaji wa huduma hizo tunatambua kwamba tunaendesha shughuli zetu kwenye jamii ambayo imekuwa rafiki siku na kutupa moyo wa kusonga mbele zaidi,” alisema Bi. Divecha. 

“Katika kurudisha sehemu ya faida kwa jamii yetu tumeonelea ni vema tufanye matembezi ya hisani ambapo kampuni itachangia kiasi kadhaa cha fedha kwa kila umbali wa kilometa atakazozitembea mfanyakazi wa Jumia. Hivyo basi mbali na kuchangia mapato yatakayotokana na matembezi hayo lakini pia itawajenga wafanyakazi kiafya na kuwakutanisha pamoja kwani ni mara chache kukutana kwa pamoja. Tunaahidi kuendelea kutoa huduma bora na kuisaidia jamii inayotuzunguka kwani ndiyo sababu ya sisi kuendelea kuwepo,” alihitimisha Meneja Rasilimali Watu wa Jumia kwa nchini Tanzania.
Kwa upande wake mmoja wa wafanyakazi wa Jumia, Mustapha Ally amesema kuwa, “Nimefurahi kwa kushiriki matembezi sio tu kwa ajili ya kusaidia watu wenye mahitaji maalum lakini pia kwa ajili ya afya yetu na pia kutuunganisha pamoja. Ningependekeza tuwe tunafanya mara kwa mara na sio mpaka kuwepo na sababu maalum.”
Jumia mbali na kutimiza miaka mitano tangu kuanzishwa kwake pia kwa mwaka huu imefanikiwa kutajwa tena kwa mara ya pili mfululizo kwenye orodha ya makampuni bora 50 na Taasisi ya Kiteknolojia ya Massachusetts (MIT) ya nchini Marekani yanayotumia teknolojia katika biashara ili kurahisisha utoaji na upatikanaji wa huduma.
Ikiwa inajishughulisha na utoaji wa huduma mtandaoni kwenye maeneo kama vile manunuzi ya bidhaa, usafiri, chakula, makazi na magari ambazo zote zinatumia jina la Jumia, kampuni hiyo inapambana na changamoto za kufanya biashara kwa njia ya mtandao barani Afrika zikiwemo barabara zisizopitika kwa urahisi, wateja wasiotabirika, kukosekana kwa mtandao wa intaneti kwenye baadhi ya maeneo ambapo lengo kubwa ni kuwashawishi watu wa tabaka la kati kufanya matumizi.  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.