Habari za Punde

Benki Kuu Kudhibiti Ukwasi wa Mabenki na Wananchi Tanzania.


Serikali imesema kuwa Benki Kuu inatekeleza sera ya fedha inayolenga kudhibiti ukwasi ili uendane na mahitaji halisi ya uchumi kwa lengo la kuuimarisha na kudumisha utulivu wa mfumuko wa bei.

Kauli hiyo imetolewa Bungeni mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), alipokuwa akijibu swali la msingi la Mbunge wa Same Magharibi Mhe. Mathayo David Mathayo (CCM), aliyetaka kujua mikakati ya Serikali ya kuongeza ukwasi katika mabenki na wananchi ili washirikiane na Serikali katika kujenga uchumi wa mtu mmoja mmoja, kaya na Taifa kwa ujumla

Dkt. Kijaji alisema kuwa, hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Benki Kuu zimesababisha hali ya ukwasi katika Sekta ya Fedha hususan benki mzuri na hakuna vihatarishi vinavyoweza kusababisha madhara hasi katika uchumi.

Dkt. Kijaji alifafanua kuwa kati ya Julai 2016 na Julai 2017, kiwango cha ukwasi katika benki kwa ujumla wake kiliongezeka kutoka asilimia 35.53 hadi asilimia 38.41.

 “Kiwango cha ukwasi wa asilimia 38.41 ni mzuri zaidi katika uchumi, ikilinganishwa na kiwango cha chini cha asilimia 20 kinachotakiwa na Benki Kuu ya Tanzania”. Alisema Dkt. Kijaji.

Alisema kuwa kuimarika kwa ukwasi kunatokana na hatua mbalimbali za kisera zilizochukuliwa na Benki Kuu, miongoni mwa hatua hizo ni kutoa mikopo ya muda mfupi kwa benki, kununua fedha za kigeni katika soko la jumla la fedha za kigeni na kushusha riba inayotozwa kwa benki za biashara na Serikali wanapokopa Benki Kuu.

Dkt. Kijaji aliongeza kuwa Benki Kuu itaendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuimarisha masoko ya fedha kwa lengo la kuhakikisha kwamba yanaendeshwa kwa ufanisi na ushindani ili kusaidia kuongeza ukwasi miongoni mwa mabenki na Taasisi nyingine za kifedha.

 Imetolewa na:
Benny Mwaipaja
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini
Wizara ya Fedha na Mipango

11/9/2017

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.