HOTUBA
YA MAONI YA KAMATI YA SHERIA, UTAWALA BORA NA IDARA MAALUM KUHUSU MSWADA WA
SHERIA YA KUFUTA SHERIA YA MAHAKAMA YA KADHI NAM. 3 YA 1985 NA KUANZISHA
UPYA MAHAKAMA YA KADHI NA KUWEKA MASHARTI MENGINE YANAYOHUSIANA NA HAYO
Mheshimiwa
Spika, kama ilivyo ada naomba nianze kwa
kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu ambae ametutujaalia neema ya uhai na uzima
mpaka kuweza kutekeleza majukumu yetu ya kila siku, namuomba azidi kutukirimu
neema hizo ambazo kwa hakika sote ni wahitaji kwake.
Mheshimiwa Spika,
napenda pia kukushukuru na kukupongeza wewe pamoja na wasaidizi wako, Mhe.
Naibu Spika pamoja na Wenyeviti wa Baraza kwa namna mnavyoliendesha Baraza kwa
umahiri mkubwa, namuomba Mwenyezi Mungu awazidishie hekma na busara katika
jukumu lenu la uongozi ili tuweze kutekeleza vyema wajibu wa chombo hiki.
Mheshimiwa Spika; Aidha,
nitumie fursa hii kuishukuru Wizara ya Nchi OR – Katiba, Sheria, Utumishi wa
Umma na Utawala Bora kwa juhudi zao kubwa walizozifanya katika kuufanyia
marekebisho Mswada huu katika Nchi yetu ambayo asilimia kubwa ya wakaazi wake
ni Waislamu.
Vile
vile, pongezi za pekee ziende kwa Tume ya Kurekebisha Sheria Zanzibar pamoja Ofisi
ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuona umuhimu wa kufanya marekebisho ya
Sheria hii ambayo imekuwa ikileta utata mkubwa katika utekelezaji wake. Pia,
nimshukuru mheshimiwa Waziri kwa kuwaongoza vyema watendaji wake kwenye kikao
chetu cha kujadili Mswada huu kwa kujibu hoja zetu vizuri na kuweza kuzitolea
ufafanuzi zaidi, na hivyo tukaweza kupata uwelewa mkubwa juu ya dhamira ya
kuletwa kwa Mswada huu.
Mheshimiwa Spika; hatahivyo, siktokuwa mwingi wa fadhila ikiwa
sitowashukuru Wadau wote walioshiriki katika kuuchangia Mswada huu kwa juhudi
zao walizoonyesha katika kufanikisha Mswada huu wa Sheria ya Kufuta Sheria ya
Mahakama ya Kadhi Nam. 3 ya 1985 na Kuanzisha Upya Mahakama ya Kadhi na Kuweka
Masharti mengine yanayohusiana na hayo.. Kwani sote ni wajibu wetu kuweza
kuuchangia kwa maslahi ya watu wetu, lakini pia, kwa faida ya Waislamu wote
waishio Zanzibar.
Mheshimiwa
Spika; kwa dhati kabisa,
Kamati inawashukuru wadau hao kwa michango yao mizuri ambayo naamini itasaidia
sana katika kuufanya Mswada huu kuwa bora zaidi. Vilevile, napenda
kuwahakikishia kwamba maoni na ushauri wao umezingatiwa na Kamati wakati
ilipokaa na Wizara ili kupatiwa ufafanuzi kuhusu Mswada huu.
Mheshimiwa
Spika, nitakuwa mchoyo
wa fadhila iwapo sitotambua mchango wa Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Baraza,
ambapo Kamati yetu iliwaalika katika kikao kilichojadili Mswada huu na Wizara.
Mheshimiwa Spika; Kamati yetu inakubaliana moja kwa moja na kufutwa
kwa Sheria ya zamani na kuanzishwa upya Sheria ya Mahakama ya Kadhi kutokana na
changamoto mbali mbali ambazo zimekuwa zikijitokeza katika utekelezaji wa
Sheria hiyo. Vile vile, Sheria hii inaanzisha Fungu la Bajeti na Fedha za
Mahakama ya Kadhi (vote), jambo ambalo ni muhimu sana katika uendeshaji wa
Taasisi hii na pia, itaweza kupunguza changamoto nyingi ambazo zimewakabili
kutoka na uhaba wa fedha za uendeshaji.
Mheshimiwa
Spika; pia, niwashukuru sana Wajumbe wa
Kamati hii pamoja na Makatibu wangu kwa mashirikiano makubwa ambayo wanatupatia
katika kuendesha shughuli zote za Kamati yetu.
Mheshimiwa
Spika; sasa naomba uwatambue Wajumbe hao kama
ifuatavyo:-
1.
|
Mhe. Machano Othman
Said
|
Mwenyekiti
|
2.
|
Mhe. Mwantatu
Mbaraka Khamis
|
Makamu Mwenyekiti
|
3.
|
Mhe. Nadir Abdul –
latif Yussuf
|
Mjumbe
|
4.
|
Mhe. Wanu Hafidh
Ameir
|
Mjumbe
|
5.
|
Mhe. Saada Ramadhan
Mwenda
|
Mjumbe
|
6.
|
Mhe. Ali Khamis
Bakari
|
Mjumbe
|
7.
|
Mhe. Suleiman Makame
Ali
|
Mjumbe
|
8.
|
Nd. Ali Alawy Ali
|
Katibu, na
|
9.
|
Nd. Haji Jecha Salum
|
Katibu
|
Mheshimiwa Spika;
naomba sasa uniruhusu nieleze baadhi ya marekebisho na mapendekezo mbali mbali
ambayo Kamati yetu imeyafanya na pia, naomba kuwatanabahisha Waheshimiwa
Wajumbe wa Baraza lako tukufu ya kwamba, hotuba hii inatoa ufafanuzi wa baadhi
tu ya vifungu ambavyo vimependekezwa na kufanyiwa marekebisho na Kamati, hivyo
maelezo zaidi ya mapendekezo hayo yamo katika muhtasari wa marekebisho yetu
ambayo Waheshimiwa Wajumbe tayari mmeshapatiwa.
Mheshimiwa Spika, Kamati ya Sheria,
Utawala Bora na Idara Maalum ilikutana na Wizara ya Nchi OR - Katiba, Sheria,
Utumishi wa Umma na Utawala Bora siku ya Jumatano,
tarehe 20 Septemba, 2017 na kuupitia
Mswada huu kifungu kwa kifungu pamoja na kufanya marekebisho ya kimantiki na
kisarufi. Vile vile, Wizara iliwasilisha katika kikao hicho Mapendekezo ya
Marekebisho ya Mswada huu katika vifungu vifuatavyo: 2, 3, 5, 8, 10, 11, 20, 28 na 33.
Aidha, Kamati
iliyapokea na kuyajumuisha katika Marekebisho ya Kamati ambayo yamewasilishwa
ndani ya Baraza baada ya kuvifanyia marekebisho machache pamoja na kufuta
marekebisho ya kifungu cha 20.
Mheshimiwa Spika, naomba niende moja kwa moja katika baadhi ya vifungu
ambavyo Kamati imevifanyia marekebisho, kama ifuatavyo:-
Kifungu cha 2, tafsiri ya “Mahakama ya Kadhi”
imerekebishwa ili iende sambamba na tafsiri iliyopo katika Mswada wa Kiingereza
na baada ya marekebisho hayo itasomeka kama ifuatavyo:
“Mahakama
ya Kadhi inajumuisha Mahakama ya Kadhi wa Rufaa na Mahakama ya Kadhi wa Wilaya,
kama ilivyoelezwa katika kifungu cha 3 cha Sheria hii”.
Mheshimiwa Spika, aidha, tafsiri ya “Mdaawa”
imeongezwa kama ifuatavyo: “Wadaawa
maana yake ni mdai na mdaiwa katika shauri la Mahakama ya Kadhi”. Kuongezwa kwa tafsiri hii kumetokana na kwamba neno hili
limetumika sana katika Mswada huu, hivyo, italeta utekelezaji bora kwa
watumiaji.
Mheshimiwa
Spika; kifungu cha 5(1) aya (a), (b), (c), (d), (e) na (f) zimefutwa na kuandikwa upya
kwani maelezo yake yapo tofauti na Mswada wa Kiingereza na uhalisia wake. Baada
ya marekebisho hayo, aya hizo zitasomeka kama ifuatavyo:-
(a) ndoa,
talaka na mambo yote yanayohusiana na hayo;
(b) nafasi
ya wanandoa;
(c) matunzo
na malezi ya watoto;
(d) wakfu
au amana za kidini, hiba na msaada;
(e) wasia
na urithi;
(f) mgawanyo
wa mali ya wanandoa pale ambapo kuna uchangiaji halisi.
Mheshimiwa
Spika, aya (d) imeongezwa katika kifungu cha 8(5) ambacho kinaongeza sifa ya ziada na muhimu katika uteuzi wa
Kadhi Mkuu na Naibu Kadhi Mkuu kitakachosomeka kama ifuatavyo:-
“(d)
mwenye taaluma na uzoefu wa dini ya kiislamu unaolingana na sifa za kuteuliwa
kuwa Kadhi”.
Mheshimiwa
Spika, marekebisho mengine yaliyopendekezwa na
Kamati ni kukifuta na kukiandika upya kifungu cha 9(2) kwa ajili ya kuweka muda wa ukomo wa kuongezwa muda wa
utumishi kwa Kadhi Mkuu na Naibu Kadhi Mkuu.
Kamati inaona kuwa kuna umuhimu mkubwa wa kuwekwa kwa muda huo. Mapendekezo ya
Kamati ni:-
“Bila
ya kujali masharti ya kifungu kidogo cha (1) cha kifungu hiki, Rais anaweza
kuongeza muda wa Utumishi wa Kadhi Mkuu na Naibu Kadhi Mkuu kama atakavyoona
inafaa lakini muda huo hautazidi miaka mitano (5)”.
Mheshimiwa
Spika, Vile vile, Kamati ilifanya marekebisho
katika kifungu cha 13(3) kwa kufuta
maneno “Qur’an na Sunnah”
yaliyojitokeza mwishoni mwa kifungu hicho na badala yake kuweka maneno “Sheria ya Kiislam”. Kamati imeona ni
vyema kuyafuta maneno hayo kwasababu tayari yamejumuishwa katika tafsiri ya “Sheria ya Kiislam”.
Mheshimiwa Spika, nina
imani kuwa Wajumbe wa Baraza hili wamepata fursa ya kuupitia kwa kina Mswada
huu, na kubaini maeneo kadhaa ya kuishauri Serikali kuhusu utekelezaji bora wa
Sheria inayotarajiwa kutungwa.
Mheshimiwa Spika;
Hivyo ni matumaini ya Kamati kwamba, Wajumbe wa Baraza hili Tukufu,
watauchangia, wataujadili ipasavyo na hatimae kuupitisha Mswada huu ikiwa ni
sehemu ya jukumu la Baraza, na hatimae kuipa fursa Serikali kutekeleza sehemu
ya jukumu lake la utekelezaji wa Sheria itakayotungwa.
Mheshimiwa Spika,
Nachukuwa fursa hii kuwashukuru kwa dhati Wajumbe wote wa Baraza lako tukufu
kwa umakini wao na usikivu wa hali ya juu waliouonesha wakati wa uwasilishaji
wa hotuba hii. Kamati inawaomba waujadili kwa kina na hatimae kuupitisha kwa
lengo la kuuboresha kwa ajili ya kuweka misingi mizuri ya Mahakama ya Kadhi
katika kuendesha majukumu yao ya kuwahudumia Waislamu wa Nchi hii.
Mheshimiwa
Spika, NAOMBA KUWASILISHA.
Ahsante,
…………………………..
(Machano
Othman Said)
Mwenyekiti,
Kamati
ya Sheria, Utawala Bora na Idara Maalum,
Baraza
la Wawakilishi,
Zanzibar
No comments:
Post a Comment