-
|
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
Kitalu Na. 8, Mtaa wa Luthuli
S.L.P 2643, DAR ES SALAAM
Simu: +255 22 2135747/8; 2137125; 2135222
Faksi: +255 22 2111281
Tovuti: www.chragg.go.tz
|
Septemba 8, 2017
TAARIFA KWA
VYOMBO VYA HABARI
Tamko
la THBUB kuhusu Mhe. Tundu Lissu (Mb) kupigwa risasi
Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora
(THBUB) imesitushwa na kusikitishwa na kitendo cha Mhe. Tundu Lissu, Mbunge wa
Singida Mashariki na Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika kupigwa risasi,
tukio lililotokea Septemba 7, 2017 mjini Dodoma.
Tume inalaani vikali kitendo hicho kwani
ni kitendo cha uvunjifu mkubwa wa sheria na haki za binadamu.
Tukio hili ambalo limekuja siku chache
tu baada ya tukio la ofisi za wanasheria wa IMMMA zilizoko jijini Dar es Salaam
kulipuliwa kwa bomu siyo la kawaida, na limeleta hofu siyo kwa familia ya Mhe.
Tundu Lissu pekee, bali kwa wananchi wengi nchini.
Isitoshe, matukio haya hayaleti picha
nzuri kwa nchi inayoheshimu demokrasia, haki za binadamu na utawala bora.
Hivyo, Tume ya Haki za Binadamu na
Utawala Bora:
1. Inalitaka
Jeshi la Polisi kuhakikisha linakamilisha haraka upelelezi wa tukio hilo na
kuwapeleka wahusika katika vyombo vya sheria.
Tume
inaamini kuwa iwapo wahusika wa tukio hili watachukuliwa hatua kali itasaidia
kukomesha vitendo vya aina hii vinavyofanywa na makundi ya watu wanaojichukulia
sheria mkononi ambayo yanaonekana kujitokeza hivi karibuni.
2. Aidha,
inapenda kukumbusha kuheshimu haki za binadamu na misingi ya utawala bora na
kuepuka ukiukwaji wa Katiba na sheria za nchi.
3. Mwisho,
inamtakia Mhe. Tundu Lissu kila la kheri katika matibabu yake ili apone haraka.
Imetolewa
na:
(SIGNED)
Mhe. Bahame Tom Nyanduga
Mwenyekiti
TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
Septemba 8, 2017
No comments:
Post a Comment