Habari za Punde

CCM yatoa mkono wa Pole na kuifariji familia iliyopata ajali ya moto


 Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Mabodi akiwafariji ndugu na jamaa wa marehemu wa familia iliyopata msiba huo katika kijiji cha Fumba Wilaya ya Magharibi “B” Unguja.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Mabodi  Akisalimiana na baadhi ya wananchi na viongozi mbali mbali waliohudhuria katika msiba huo.


 Na Is-haka Omar, Zanzibar.

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kimetoa mkono wa pole kwa familia iliyopata ajali ya kuungua moto nyumba na kusababisha vifo vya watu wanne huko katika kijiji cha Fumba Wilaya ya Magharibi “B” Unguja.

Akizungumza Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dk. Abdalla Juma Mabodi wakati wa kuifariji familia hiyo amesema CCM Zanzibar imesikitishwa sana na tukio hilo kwani limegharimu maisha ya wananchi wasiokuwa na hatia.

 Dk. Mabodi alisema kwa niaba ya Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  anatoa pole kwa ndugu, jamaa na marafiki wa familia hiyo na kuwasihi waendelee kuwa  na moyo wa subra katika kipindi hichi kigumu cha msiba huo.
“Kupoteza watu  Wanne katika familia moja  ni jambo zito linalotia huzuni lakini tuendelee kuwa wavumilivu kwani Allah amewapenda zaidi na sisi tuliobaki tuendelee kuwaombea  dua ili wapate makaazi mema na kusamehewa madhambi yao”, alitoa nasaha hizo kwa masikitiko makubwa Dk. Mabodi.”
Mapema Sheha wa Shehia ya Fumba, Mohamed Suleiman alifafanua kuwa nyumba hiyo ilianza kuwaka moto majira ya saa 6:15 usiku Oktoba 21 mwaka huu, ambapo wananchi mbali mbali walianza juhudi za kuzima moto huo na kushindwa kuokoa watu waliokuwa ndani kwani uliku ni mkubwa.
Suleiman alisema wakati juhudi za kuzima moto huo zikiendelea waliwasiliana na Kikosi cha Zimamoto na Uokozi Zanzibar ambacho kilifika na kusaidiana na wananchi hao ambapo walizima moto huo na kukuta watu wanne tayari wamefariki dunia.
Akidhibitisha tukio tukio hiloalisema chanzo cha moto huo ni hitilafu za umeme zilizoanzia katika waya wa jokofu (Friji) lililokuwa likifanya kazi wakati wa usiku.
Kamanda Nassir aliwataja watu waliofariki katika tukio hilo kuwa ni Bahati Ali Ameir (40), Sinawema Abdalla Ali, Hashim Abdalla Ali (6) na Latifa Mohamed Ali (8).
Alitoa wito kwa wananchi kujenga utamaduni wa kuzima vifaa vya umeme wakati wa usiku ambavyo havina umuhimu wa kutumiwa wakati huo ili kuepuka majanga yanayoweza kuhatarisha maisha ya watu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.