Habari za Punde

Tuhuma za Rushwa Kwa Vyombo Vya Sheria Isiwarejeshe Nyuma.

Na.Haji Nassor - Pemba.
WADAU wa haki za binadamu kisiwani Pemba, wamesema tuhuma za rushwa zinazoelekezwa kwenye vyombo vya kisheria kama vile Polisi na mahakama, isiwe sababu kwa jamii, wanapovunjiwa haki zao za binadamu, kutovitumia vyombo hivyo kudai haki zao.

Walisema sio kweli kuwa, vyombo hivyo vinanuka rushwa na havifai kufungua mashitaka, iwapo kuna mtu au kundi la watu limevunjiwa haki zao, na badala yake wasisite kuvitumia, maana wapo wanaoshinda na kupata haki zao.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti, wadau hao walisema jeshi la Polisi, Mahakama, Ofisi ya mkurugenzi wa mashitaka, taasisi kama ZAECA na ZLSC vipo kwa ajili yao.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa kusini Pemba, Shehah Mohamed Shehan, alisema hata iweje lazima wananchi walitumie jeshi la Polisi, pale wanapovunjiwa haki zao za binadamu, hata kama wafanyaji ni Polisi.

Alisema, kujitokeza kwa mtendaji mmoja wa jeshi hilo, kudaiwa kuchukua rushwa au kufanya jambo ovu, isiwe sababu kwa jamii kulikataa jeshi lote, wakati wanapovunjiwa haki zao kwenye shughuli zao za kila siku.

“Jamii isikae majumbani wanapobaini kuwa wamevunjiwa haki zao za binadamu, kwa dhana potofu walizonazo kuwa, hata ukipeleka kesi, basi itaambatanisha wa rushwa”,alisema.

Hata hivyo alisema, upo uhusiano wa karibu baina ya rushwa na utekelezaji wa sheria kwenye kesi za uvunjifu wa haki za binadamu, ambapo wakati mwengine, husababishwa na jamii husika.

Nae Mwanasheria dhamana wa Afisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka Pemba, Ali Rajab Ali alisema, uwepo wa rushwa kwenye vyombo vya kutoa uamuzi, unaathiri upatikanaji wa haki hasa kwa maskini.

Mwanasheria huyo, alisema uwepo wa tuhuma hizo, haina mantiki kwa jamii, kwamba wasivitumie vyombo hivyo, wakati wanapoona wamevunjiwa haki zao za binadamu.

“Kama kuna Mwendesha mashitaka, Polisi au hakimu mmoja anatuhumiwa kwa rushwa, haina maana kwamba, sasa jamii iache kuvitumia vyombo hivyo, maana wachukua rushwa sio wote”,alisema.

Katika hatua nyengine Mwanasheria huyo, alisema zipo ksei kadhaa ambazo mtu mmoja, amemshitaki mtendaji wa vyombo vya sheria, ishara inayonyesha hakuna alie juu ya sheria.
Kwa upande wake, Mdhamini wa Mamlaka ya Kuzuia rushwa na Uhujumu wa Uchumi Zanzibar ZAECA afisi ya Pemba, Suleiman Ame Juma, alisema jamii isiwe na wasiwasi wa kuviogopa vyomba vya kisheria, maana wamekuwa wakipokea malalamiko yao, pindi wakijihusisha na rushwa bila ya kujali vyeo vyao.

Alisema zipo kesi za viongozi wakuu, kwenye sekta na taasisi hizo za vyombo vya sheria, wakiwashikilia kutokana na tuhuma za rushwa, jambo ambalo kila kundi linaweza kutazamwa.

“Jamii iondoe shaka kuwa, hata Polisi, hakimu, mwanasheria mwengine akionekana na rushwa ataachiwa, hakuna bali nae sheria itamuandama kama walivyo wengine”,alisema.
Afisa Mipango wa Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar ZLSC tawi la Pemba, Mohamed Hassan Ali, amesema haki za bindamu, zimeshaundiwa taasisi kama wizara husika, ili wanaovunjiwa wawe na pahala pakukimbilia.

Alisema hata mfano wa Kituo chao, kimekuwa kikitumiwa na wananchi waliowengi, pale wanapohisi wamevunjiwa haki zao za binadamu, hata ikiwa wavunjaji wakuu ni wale wanaofanyaka kazi kwenye vyombo vya kisheria.

“Sisi ZLSC tumeshapokea hata malalamiko ya Polisi au mahakimu, wakituhumiwa kwa rushwa, na malalamiko hayo kuyafanyia kazi, hivyo jamiii isisite kututumia wakiona wanafanyiwa ndivyo sivyo”,alisema.

Mapema Meneja miradi kutoka Jumuia kwa ajili watu wenye ulemavu wa akili Zanzibar, ofisi ya Pemba, Ali Mwadini Haji, alisema, bado kundi analoliongoza limekuwa na hofu kubwa kushinda kesi zao, kwa hofu ya kuingiliwa na rushwa.

Alisema asili hasa ya wazazi, walezi na watu wenye ulemavu wa akili wenyewe, wamekuwa wogo kutetea haki zao, kutokana na utamadani mkubwa uliopo, wa rushwa kwenye kesi za uvunjifu wa haki za bindamu.

“Mtu mwenye ulemavu, bado anaona ni sawa anapovunjiwa haki zake kubaki nyumbani, maana anawasiwasi wa kuzingiliwa na rushwa, anapokwenda kwenye vyombo vya kisheria”,alisema.

Msaidizi wa sheria jimbo la Chakechake Riziki Hamad Faki, alisema yapo mahusinao ya karibu katika upatikanaji wa haki za mashauri ya uvunjifu wa haki za binadamu, na rushwa.
Baadhi ya wananchi kisiwani Pemba, walisema bado ipo haja kwa vyombo vya kisheria, kuendelea kujisafisha ili jamii iwatazame katika jicho la utawala bora.

Haji Makame Omar wa Wawi, alisema jamii haijaona kuwa ndani ya vyombo vya kutoa haki, kama Polisi na Mahakama, mtu anaweza kushinda kesi bila ya kutumia rushwa.

“Ndio maana wapo baadhi hata wanapovunjiwa haki zao za binadamu, hushindwa kuvifikia vyombo vya kisheria, na ndio maana hupenda kumaliziana kienyeji”,alisema.

Hidaya Said Omar wa Kengeja, alisema anachoamini yeye kuwa, vyombo vya kisheria, vitaendelea kuwa ni mali ya wakubwa, watu maarufu na wenye nacho, na sio vyombo vya kila mmoja kama sheria zinavyoelekeza.

Mrajisi jimbo mahakama kuu Pemba, Huseein Makame Hussein alisema, sio sahihi kuvitafsiri vyombo kama vya mahakama kuwa, vinachukua rushwa bali hizo ni dhana zilizopo zisizo na ushahidi.

Alisema mahakamani baada ya kupokea kesi, husikilizwa na lazima mwisho wake mmoja wapo ashindwe na mmoja ashinde, hivyo upande usioridhika, hushutuma uwepo wa rushwa mahakamani.

Hata hivyo wadau hao, wameiomba jamii kuendelea kuvitumia vyombo vya sheria, wanapokumbana na moja ya uvunjifu wa haki za binadamu, na kuacha tabia ya kujichukulia sheria mikononi.


Tayari tokea kuanza kwa mwaka huu wa 2017, watu watatu wameshauwawa na watu wanaodaiwa kuwa na hasira, ndani ya mkoa wa kusini Pemba pekee.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.