Habari za Punde

Wakulima wa Miwa Kagare Waaswa Kuchangamkia Soko la Miwa Kiwanda Cha Sukari Kagera.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (kushoto) akizungumza na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Sukari cha Kagera Bw. Ashwin Rana alipotembelea kiwanda hicho kwa ziara ya kikazi ambapo alimpongeza kwa kuongeza uzalishaji wa Sukari na kutoa ajira kwa wakulima wanaozunguka eneo hilo.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (kulia) akiongozwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Sukari cha Kagera Bw. Ashwin Rana alipotembelea kiwanda hicho kwa ziara ya kikazi.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (wa pili kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Mhandisi wa masuala ya Kielektroniki wa Kiwanda cha Sukari cha Kagera, Bw. Obed Kiswaga (kushoto) kuhusu utendaji kazi wa kiwanda hicho baada ya kutembelewa na Naibu Waziri huyo.
Msimamizi wa Mitambo ya Kiwanda cha Sukari cha Kagera, Bw. Eliasa Kilemile  (kushoto) akitoa ufafanuzi wa usimamizi wa mitambo ya kiwanda hicho kwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (kulia) baada ya Naibu Waziri huyo kufanya zaiara kiwandani hapo.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) akiwa ameshika mfuko wa sukari wenye ujazo wa kilo moja inayozalishwa katika Kiwanda cha Sukari cha Kagera, alipokuwa akipata maelezo kuhusu ubora wa sukari inayozalishwa kiwandani hapo kwa kutumia teknolojia ya kisasa.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (kushoto) akiangalia mitambo ya kutengeneza Sukari inavyofanyakazi, alipotembelea katika kiwanda cha Sukari cha Kagera.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (wa pili kushoto) akitembelea maeneo ya kiwanda cha Sukari cha Kagera kujionea namna kiwanda hicho kinavyozalisha sukari.
Mtaalam Mwandamizi wa masuala ya Kilimo katika kiwanda cha Sukari cha Kagera, Bw. Nassoro Abubakari, (wa pili kulia) akimuelezea Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (kushoto) kuhusu mbegu tano za miwa ambazo zinatumika katika shamba la miwa la kiwanda hicho.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (kushoto) akisikiliza maelezo ya Mtaalam Mwandamizi wa masuala ya Kilimo katika kiwanda cha Sukari cha Kagera, Bw. Nassoro Abubakari, kuhusu ramani ya shamba la kiwanda hicho na namna linavyotumika katika uzalishaji wa miwa.
Mtaalam wa masuala ya Kilimo katika kiwanda cha Sukari cha Kagera, Bi. Salma Msonga, (kulia) akimueleza  Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe Dkt. Ashatu Kijaji (Mb) (kushoto) hatua za kuzalisha miwa kuanzia mbegu hadi uvunaji baada ya Naibu Waziri huyo kutembelea shamba la kiwanda hicho Mkoani Kagera kujionea uzalishaji wa sukari kiwandani hapo.

(Picha na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini-Wizara ya Fedha na Mipango)

Na.Benny Mwaipaja, Karagwe
NAIBU Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, amewataka wakulima wa miwa wanaozunguka Kiwanda cha Sukari cha Kagera (Kagera Sugar) kuchangamkia soko la uhakika la zao hilo kwa  kuongeza uzalishaji wa miwa kutokana na uhitaji mkubwa wa miwa kwa ajili ya uzalishaji wa miwa katika kiwanda hicho

Dkt. Kijaji alitoa wito huo baada ya kutembelea kiwanda hicho na kuelezwa kuwa katika msimu wa kilimo cha miwa uliopita wakulima wa miwa wanaozunguka kiwanda hicho walilipwa Shilingi bilioni 4 baada ya kukiuzia kiwanda hicho zaidi ya tani 56,000 za miwa.

Alisema kuwa bado mahitaji ya miwa kwa ajili ya kuzalisha sukari kiwandani hapo ni makubwa na kuwataka wakulima hao kupitia umoja wao wa wakulima wadogo wa miwa kuhamasishana kuongeza uzalishaji ili waweze kujikwamua kiuchumi.

Kiwanda cha Sukari cha Kagera kimeendelea kuongeza uzalishaji tangu kipate wawekezaji ambapo uzalishaji huo umeongezeka kutoka tani 25,000 mwaka 2011/2012 hadi kufikia tani 75,000 na katika kipindi cha miaka mitano ijayo uzalishaji utafikia tani 170,000.

Afisa Mwendeshaji Mkuu wa Kiwanda hicho Bw. Ashwin Rana alisema wameanzisha Kitengo maalumu cha kuwaendeleza wakulima wadogo wa miwa wanaozunguka mashamba yao kwa kuendelea kuwapatia vitendeakazi ikiwemo matrekta, utaalamu pamoja na mbegu bora za miwa ili waweze kuchangia kuzalisha miwa yatakayosaidia waweze kufikia malengo yao ya kuongeza uzalishaji wa sukari.

Bw. Rana alisema kuwa tangu walipoanza kuunda umoja wa wakulima wadogo wa miwa wanaozunguka mashamba yao mwaka 2006, uzalishaji wao umeongezeka kutoka tani 0 hadi tani 56,000 ambazo kiwanda hicho kilinunua msimu uliopita na kwamba wanatarajia uzalishaji wao utaongezeka zaidi.

“Mahitaji ya sukari nchini kwa mwaka ni tani 450,000 lakini uzalishaji uliopo hivi sasa ni tani 320,000 na kwa mikakati ya Kiwanda cha Sukari Kagera ya kuongeza mashamba na teknolojia ya uzalishaji wa bidhaa hiyo utapunguza kwa kiasi kikubwa upungufu huo” aliongeza Bw. Rana.

Kaimu Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania TRA Bw. Beatus Nchota, alieleza kuwa Mamlaka hiyo inapongeza jitihada kubwa ya kiwanda hicho kuongeza uzalishaji hatua ambayo itaongeza mauzo, ajira na hatimaye kuongeza kiwango cha kodi ambayo Kiwanda hicho kimekuwa kikilipa kwa kiwango kikubwa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.