Mkurugenzi wa Shughuli za
Kitakwimu kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Irenius Ruyobya (kushoto)
akizungumza na waandishi wa habari leo katika ukumbi wa NBS kuhusu maadhimisho
ya Siku ya Takwimu Afrika yatakayofanyika
tarehe 20 Novemba, 2017 jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mtakwimu
Mwandamizi Philemon Mwenda.
Baadhi ya waandishi wa habari waliohudhuria
kwenye mkutano kuhusu maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika yatakayofanyika tarehe 20 Novemba, 2017 jijini Dar es Salaam.
Na: Veronica Kazimoto, Dar es Salaam,
16 Novemba, 2017.
Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania
anatarajia kuwa mgeni rasmi katika Maadhimisho ya Siku ya Takwimu Afrika yatakayofanyika tarehe 20 Novemba, 2017 katika Kituo cha
Mikutano cha Kimataifa cha Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
Akizungumza
na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, Mkurugenzi wa Shughuli za
Kitakwimu kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Irenius Ruyobya amesema
maadhimisho hayo yanayoratibiwa na ofisi hiyo kwa niaba ya Serikali, yana lengo
la kuongeza ufahamu kuhusu nafasi na mchango wa Tasnia ya Takwimu katika kuleta
maendeleo ya kiuchumi na kijamii Barani Afrika.
Ruyobya amesema kuwa kaulimbiu
ya Siku ya Takwimu Afrika kwa mwaka huu ni “Takwimu Bora za Uchumi kwa Maisha
Bora"
"Kaulimbiu hii inalenga
kuweka mkazo katika matumizi ya Takwimu za Uchumi kwa ajili ya kuboresha maisha
ya wananchi wote nchini na Afrika kwa
ujumla", amebainisha Ruyobya.
Ruyobya amefafanua kuwa
matumizi sahihi ya Takwimu za Uchumi yanaiwezesha Serikali kutunga sera na
kutathmini programu mbalimbali kama vile Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka
Mitano (FYDP-II), Agenda ya Dunia ya Mwaka 2030 ya Malengo ya Maendeleo
Endelevu (SDGs) na Agenda ya Afrika ya Mwaka 2063.
"Progaramu zote hizi, zina
lengo la kuboresha maisha ya wananchi kwa kuhakikisha kuwa, kuna upatikanaji wa
Huduma za afya, Elimu,
Miundombinu ya umeme na
barabara, Mawasiliano, Utunzaji wa mazingira pamoja na Utawala bora",
amesema Ruyobya.
Jumla ya washiriki 200 kutoka
katika Wizara, Idara na Taasisi za Serikali, Wadau wa Maendeleo, Vyuo vya Elimu
ya Juu, Wanafunzi wa Shule za Sekondari pamoja na Wadau mbalimbali wa takwimu
nchini wanatarajiwa kuhudhuria kwenye maadhimisho hayo.
Tarehe 18 Novemba ya kila
Mwaka, Tanzania huungana na nchi nyingine Barani Afrika kuadhimisha Siku ya
Takwimu Afrika, kutokana na siku hii kuwa
Jumamosi, maadhimisho haya yatafanyika Jumatatu tarehe 20 Novemba, 2017.
No comments:
Post a Comment