Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Ali Mohamed Shein, Azungumza na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Teknolojia Cha India.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                                                             14.11.2017
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa utekelezaji wa hati ya makubaliano (MoU) kati ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) na Chuo Kikuu cha Teknolojia (VIT) cha nchini India ni muendelezo wa uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na India.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu Mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Teknolojia (VIT) cha nchini India  Dk. Govindasamy Viswanathan akiwa na  wenyeji wake uongozi wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), ukiongozwa na Makamu Mkuu wa chuo hicho Profesa Idris Ahmada Rai.

Katika maelezo yake Dk. Shein alitoa pongezi kwa uongozi wa Chuo Kikuu cha (VIT) kwa kufika Zanzibar kwa lengo la kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya chuo hicho na chuo Kikuu cha (SUZA), hatua ambayo inazidi kujenga udugu na uhisiano kati ya Zanzibar na India.

Dk. Shein alieleza kuwa Zanzibar ina mambo ya kujifunza kutoka India hasa katika  masuala ya Teknolojia ya kisasa ambayo nchi hiyo imeweza kupiga hatua na kupata mafanikio makubwa.

Aliongeza kuwa licha ya chuo Kikuu cha SUZA kuwa kichanga lakini kimeweza kupiga hatua kubwa na kupata mafanikio, hivyo kuendeleza uhisnao na vyuo vikuu ulimwenguni kikiwemo chuo Kikuu cha VIT kutakisaidia chuo hicho kupanua wigo wa maendeleo sambamba na kujenga uwezo wa wafanyakazi kitaaluma.

Aidha, Dk. Shein alisisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini ushirikiano wan chi rafiki hivyo hatua ya chuo hicho kusaini hati ya mashirikiano kati yake na chuo kikuu cha SUZA kinaipa Serikali kuendelea kutilia mkazo suala hilo pamoja na kuendelea kutekeleza azma yake ya kuimarisha sekta ya elimu hapa nchini.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alimueleza Mkuu huo wa Chuo Kikuu cha VIT alieongozana na Mkurugenzi wa Uhusiano wa Kimataifa wa chuo hicho Dk. C. VijayKumar kuwa azma na malengo ya nchi zote za Jumuiya ya Umoja wa Afrika (AU) ikiwemo Tanzania ni kuimarisha sekta ya viwanda.

Hivyo, alisisitiza kuwa hatua ya ushirikiano huo utaimarisha zaidi uanzishwaji wa vituo vya ubunifu na ujasiriamali kupitia Teknolojia ya kisasa na hatimae kuisaidia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutekeleza azma ya kuanzisha viwanda vikiwemo vidogo vidogo na vya kati kutokana na rasilimali zake zilizopo.

Alieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza soko la ajira kwa wananchi wa Zanzibar huku akisisitiza haja ya kutilia mkazo suala zima la utafiti kwa chuo kikuu cha (SUZA) jambo ambalo limo katika hati ya makubaliano (MoU) ya vyuo vikuu hivyo.

Kuhusu utafiti wa bahari Dk. Shein alieleza haja ya kuendeleza utafiti wa bahari ili Zanzibar iweze kufaidika na bahari hasa ikizingatiwa kuwa maeneo yake yote ya visiwa vya Zanzibar yamezungukwa na bahari.

Nae Mkuu wa chuo Kikuu cha (VIT), Dk. Govindasamy Viswanathan alimueleza Dk. Shein kuwa chuo chake kimekusudia kuimarisha uhusiano na mashirikiano zaidi na Chuo Kikuu cha (SUZA) kwa kwa manufaa ya pande zote mbili.

Alieleza kuwa Chuo chake kiko tayari kuyatekekeza yale yote yaliotiwa saini katika hati ya mashirikiano na kusisitiza kuwa tokea kuanzisha mashirikiano yao mwaka 2013 kumekuwa na mafanikio makubwa.

Alieleza kuwa Chuo cha (VIT) ni miongoni mwa vyuo maarufu sana nchini India na kwa upande wa vyuo binafsi ni chuo kinachoongoza nchini humo ambacho kimeweza kupata mafanikio makubwa ndani na nje ya nchi hiyo hasa katika masuala ya Teknolojia ya kisasa.

Mapema Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) Profesa Idris Rai alimueleza Dk. Shein kuwa mnamo mwaka 2013 vyuo hivyo vilisaini hati ya makubaliano (MoU) na kukubaliana kushirikiana katika maeneo ya kadhaa yakiwemo kubadilishajna wafanyakazi, kubadilishana wanafunzi na kufanya tafiti za pamoja.

Aidha, alieleza mashirikiano mazuri na mahusiano yaliopo kati ya Chuo Kikuu cha (SUZA) na chuo cha (VIT) huku akieleza matumaini makubwa wanayotarajia katika mahusiano hayo hasa ikizingatiwa kuwa chuo hicho kimepiga hatua kubwa katika masuala ya Teknolojia.

Aliongeza kuwa mpaka hivi sasa tayari (SUZA) imeshasomesha walimu wa TEHAMA wawili katika ngazi ya Shahada ya Uzamili na mmoja anaendelea na masomo na wamekwua wakipata mashirikiano mazuri na chuo cha (VIT) katika mafunzo hayo.

Alieleza kuwa moja ya dhamira za ziara ya Mkuu huyo wa Chuo Kikuu cha (VIT) ni kuweka saini nyongeza ya Hati ya Makubaliano (MoU), itayowezesha kuanza kwa masomo ya TEHAMA mwaka ujao pamoja na dhamira ya kufanya mazungumzo juu ya uanzishwaji wa kituo cha Ubunifu na Ujasiriamali kupitia (TEHAMA) zoezi ambalo lilifanyika hapo jana.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.