PRESS RELEASE
Dodoma 09.12.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amewataka Watanzania kujitathmini uzalendo wao kutokana na
kushuka kwa kasi na ari ya uzalendo huku akisisitiza haja ya kumuunga mkono
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli kutokana na jinsi
anavyotekeleza uzalendo kwa vitendo.
Dk. Shein aliyasema
hayo katika hafla ya Kampeni ya “Uzalendo na Utaifa”, iliyofanyika katika
ukumbi wa Chimwaga mjini Dodoma ikiwa ni miongoni mwa shamra shamra za
kuadhimisha miaka 56 ya Uhuru wa Tanzania Bara ambapo kauli mbiu ya sherehe
hizo mwaka huu ni ‘Uhuru wetu ni tunu, tuudumishe, tulinde rasilimali zetu,
tuwe wazalendo, tukemee rushwa na uzembe”..
Katika hotuba yake Dk.
Shein alitumia fursa hiyo akieleza maana ya mzalendo na uzalendo na kueleza
kuwa mzalendo ni yule aliyezaliwa pahala fulani kwenye asili yake ambapo pia,
ni mtu mwenye mapenzi ya dhati sana ya kuitumikia nchi yake na kueleza maana ya
uzalendo kuwa ni hali ya mtu kuwa na nasaba ya asili ya nchi ambaye pia
hujitolea kwa hali na mali kwa ajili ya nchi yake.
Alieleza kuwa kasi na
ari na mwamko wa uzalendo imepungua kwani uzalendo ni vitendo na
unapovitekeleza ndipo unapokuwa Mtanzania halisi na mzalendo halisi.
Aliongeza kuwa tangu kufanyika
kwa uhuru wa Tanganyika na Mapinduzi ya Zanzibar waasisi wa pande mbili hizo
Marehemu Mzee Abeid Amani Karume na Marehemu Julius Kambarage Nyerere walifanya
kazi kubwa ya kuwaandaa Watanzania kuwa wazalendo.
Dk. Shein alieleza
kuwa uzalendo una muda mrefu na pia, ni jambo kogwe kwani uzalendo hutengenezwa
na huwekewa mazingira mazuri ili wananchi wawe wazalendo kazi ambayo waliifanya
waaasisi hao kwa kuiunganisha Zanzibar na Tanganyika na kuwa Jamhuri ya Mungano
wa Tanzania, kazi ambayo ilikuwa ni ya
kizalendo.
Alieleza kuwa viwango
vya uzalendo vimekuwa vikitofautiana kwani baadhi ya Watanzania wanatofautiana kwani
kuna baadhi yao wanapokwenda nchi za nje hujificha kutambuliwa kuwa wao ni
Watanzania na kuukana Utanzania wao jambo ambalo linaonesha wazi kuwa hao si
wazalendo.
Alieleza kuwa uzalendo
huendelezwa na hufanywa kwa vitendo, kwani kumbukumbu zinaonesha kuwa mara
baada ya uhuru Baba wa Taifa akisisistiza Uhuru na kazi ambapo hivi sasa kujitolea
kumepungua ambapo Tanzania kuna utaratibu wa kupeana bahasha ama posho kwa
kuwalipa watu hali ambayo haikuwepo kabla ya uhuru na hata Mapinduzi.
Rais Dk. Shein
alieleza kuwa Wazanzibari walijenga nyumba za Michezani kwa kujitolea kutokana
na uzalendo waliokuwa nao jambo ambalo limekuwa ni tofauti kwani hivi leo wapo
wananchi wanaoisema Serikali na viongozi wa Serikiali kwa lugha zisizo nzuri,
hivyo ni lazima Watanzania wajitathmini na kumuunga mkono Rais Magufuli ili
jamii iendelee kuwa na uzalendo kama ilivyokuwa hapo siku za nyuma.
Dk. Shein alisema kuwa
uzalendo ni kila kitu, hata utawala bora ni uzalendo kwani unapozungumza huwa
unazungumziwa utawala wa sheria na lazima kila mmoja akipende chake cha
Tanzania na kukumbusha msemo wa Marehemu mzee Karume kuwa “ Kithamini
kilichochako mpaka usahau cha mwenzako”, alisema Dk. Shein.
Aliongeza kuwa
uzalendo ni sehemu ya maisha hivyo ni lazima ufanywe kwa vitendo huku
akisisitiza kuwafundisha watoto mila, desturi, maadili na uadilifu kwani malezi
yamepungua kwa kiasi kikubwa hivi sasa.
Alieleza kuwa uzalendo
unaanza nyumbani kumfunza mtoto katika familia kwani hapo zamani mtoto hulelewa
na mtaa mzima na sio baba na mama peke yao jambo ambalo lilipelekea watoto kuwa
na malezi mazuri na kuwakuza wakiwa wazalendo.
Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kumpongeza Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na
kumpongeza Makamo wa Rais kwa niaba ya Rais Magufuli kwa kubuni jambo hilo ambalo ni muhimu sana na
ipo haja ya kuungana apamoja katika kuhakaikisha Kampeni hiyo inafanikiwa kwa
manufaa ya Tanzania.
Akizungumzia kuhusu
suala zima juu ya lugha ya Kiswahili, Dk. Shein alisisitiza haja ya
kukizungumza na kukithamini Kiswahii na kueleza namna Baba wa Taifa Mwalimu
Julius Nyerere na Marehemu Mzee Karume walipoamua kukifanya kiswahili kuwa ni
lugha ya taifa.
Aidha, Dk. Shein alimpongeza
Rais Magufuli kwa kuwahimiza Mawaziri wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
kukizungumza kiswahili katika shughuli zao zote hasa kwa kufahamu kwamba lugha
hiyo ina haiba kubwa, kwani ni lugha ya pwani iliyoanzia Zanzibar na kuenea
katika ukanda wa Afrika Mashariki na hatimae duniani kote.
Sambamba na hayo, Dk.
Shein alieleza haja kwa Watanzania kukiimarisha kiswahili kwani kuna baadhi ya
wananchi wahaitendei haki lugha hiyo kwa kuizungumza visivyo.
Aliongeza kuwa kuna
kila sababu ya kukizungumza Kiswahili na kukiendeleza ikiwa ni pamoja na
kuyasoma na kuyafuatilia makkamusi ya Bara na Zanzibar ambayo yanatoa muongozo mzuri
wa kiswahili huku akisisitiza kuwa hakuna mbadala wa uzalendo na wananchi wote
wana asili ya Tanzania.
Katika hafla hiyo
viongozi mbali mbali walihudhuria ambapo mgeni rasmi katika hafla hiyo alikuwa
Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan na
kuwashirikisha wasanii mbali mbali wakiwemo waimbaji wakongwe pamoja na wale wa
kizazi kipya.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment