Habari za Punde

Rais Dk Shein, Kuwazawadia Wachezaji wa Zanzibar Heroes.Fedha na Viwanja.

USIKU wa kuamkia leo ulikuwa ni wa kihistoria kwa timu ya mpira wa miguu ya Taifa ya Zanzibar,’Zanzibar Heroes’ baada ya Rais  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kuwazawadia viwanja vya kujenga nyumba pamoja na fedha taslim Shilingi milioni tatu kwa kila mchezaji na kiongozi wa timu hiyo.

Zawadi hizo alizitowa katika tafrija maalum iliyofanyika katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi la zamani Kikwajuni mjini Zanzibar sambamba na taarab maalum aliyowaandalia timu hiyo iliyotumbuizwa  na kikundi cha Taifa cha Taarab cha Zanzibar kufuatia kufanya vizuri katika mashindano ya mwaka huu ya Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati ‘CECAFA’ na kupata nafasi ya pili.

Viongozi mbali mbali wa Serikali, vyama vya siasa, ZFA, na waalikwa wengine wakiwemo veterani walihudhuria katika tafrija hiyo maalum ambayo Dk. Shein aliwaandaliwa wachezaji na viongozi wa timu hiyo baada ya hapo juzi kuwaandaliwa chakula cha mchana katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar.

Dk. Shein alitoa zawadi hiyo kwa kutimiza ahadi yake aliyoitoa hapo juzi huko katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar ambapo akitoa salamu zake na pongezi kwa wachezaji na viongozi wa timu hiyo alikataa kuzitaja zawadi hizo na ambazo jumla yake zilikuwa tatu na aliitaja ile ya taaraab tu na kusema mbili angezitaja hapo jana.

Vigeregere, hoihoi na nderemo zilisikika katika ukumbi huo kutoka kwa wachezaji na viongozi wa timu hiyo pamoja na hadhara iliyohudhuria tafrija hiyo mara baada ya Rais Dk. Shein kuzitangaza zawadi hizo ambazo kila mmoja alikuwa anasubiri kwa hamu kuzisikia.

Rais Dk. Shein aliwakabidhi hundi ya Shilingi za Kitanzania milioni tatu kwa kila mchezaji na viongozi ambao kwa ujumla wao ni 33 huku akiwaeleza kuwa kwa upande wa viwanja watakabidhiwa si muda mrefu baada ya kukamilika hati zao na nyaraka nyengine muhimu kutoka kwa Wizara husika ya Ardhi, Maji, Nishati na Mzingira.
Aidha, Dk. Shein aliwausia wachezaji na viongozi wa timu hiyo kuwa zawadi hiyo ya viwanja aliyowapa ni muhimu wakaitunza na kuienzi na kubaki nayo na hatofurahi iwapo atatokezea mmoja miongoni mwao na kuiuza kwani hilo sio lengo lake na yeye atajua kwa atakaefanya hivyo.

Dk. Shein alieleza kuwa hiyo walioipata wao ni bahati kubwa sana kwani wapo maveterani waliocheza mpira wakati huo na kushinda mashindano mbali mbali lakini hawakupata zawadi hizo ambazo zina umuhimu mkubwa katika maisha yao.

Mapema katika hutoba yake Dk. Shein alisema kuwa timu ya Taifa ya Zanzibar, Zanzibar Heroes ilibezwa sana  na kuitwa majina mbali mbali waliitwa wala urojo, wala ubuyu bila ya kuelewa kuwa hao waliowaita majina hayo hawajui kuwa vyakula hivyo vina nguvu.

Aliongeza kuwa kutokana na timu hiyo kuogopwa shutuma mbali mbali ilishutumiwa timu hiyo na kueleza kuwa si jambo la rahisi timu ya Kenya wakatamani tena kukutana na ‘Zanzibar Heroes’ katika fainali ya mashindano hayo yaliofanyika nchini Kenya.

Alisema kuwa kutokana na timu hiyo kuonesha soka safi hivi sasa inaheshimiwa na kusisitiza kuwa mchezo wa mpira hujenga udugu, maelewano na kuimarisha urafiki sambamba na kutoa ajira.

Dk. Shein alitoa historia ya mpira wa miguu hapa Zanzibar na kueleza kuwa ushindi huo haukuja kwa bahati mbaya kwani Zanzibar ina historia kubwa ya soka tokea mwaka 1919 kulipoanzishwa timu ya ‘Kiungani School Team’ pamoja na makocha wa mpira wa miguu na kusisitiza kuwa malengo ya Serikali ni kuimarisha michezo kwa vitendo na si kwa maneno.

Aidha, aliitaka Wizara ya Habari,Utalii, Utamaduni na Michezo kuongeza kasi ya kuongoza mpira na sio kugombana wenyewe kwa wenyewe hadi kufikishana mahakamani kwani Wazanzibari wanataka mpira na sio kwenda mahakamani

Pia, alikubali ombi lililotolewa na Kocha wa timu hiyo Hemed Suleiman Moroko hapo juzi katika viwanja vya Ikulu la kuomba kumualika nchini Rais wa Shirikisho la Soka Barani Afrika Ahmad Ahmad kuja Zanzibar ili kufanya mazungumzo nae kwa ajili ya kuzungumzia mustakbali wa Zanzibar katika soka kimataifa na kuahidi kufanya hivyo kwa kiongozi huyo na viongozi wengine wa soko ulimwenguni.

Dk. Shein alitoa agizo kwa Wizara ya Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo kuhakikisha ktimu hiyo inapelekwa kisiwani Pemba kwa kutumia meli mpya ya MV Mapinduzi II ili wananchi wa kisiwani humo wapate kuiona timu yao na kufurahi kwa pamoja.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itawekeza katika timu hiyo ili timu hiyo iwe bora na wachezaji waliopo wataongezwa ili kocha awe na uwezo wa kuchagua.

Nae Kocha Mkuu wa timu hiyo alitoa shukurani zake kubwa kwa Rais Dk. Shein kwa kuwazawadia zawadi hizo ambazo ni za pekee na kumpa ahsante huku akieleza kwa niaba ya wenziwe kuwa hawana cha kumlipa Rais Dk. Shein ila kumpa ahsante huku wakiahaidi kuwa watahakikisha wanalipa deni kubwa walilonalo katika kuieletea Zanzibar ushindi.

Kikundi hicho cha Taarab kilipiga nyimbo mbali mbali zikiqwemo za kuwasifu wachezaji hao pamoja na kumpongeza Rais Dk. Shein kwa juhudi zake katika kuimarisha sekta ya michezo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.