Habari za Punde

Hutuba ya Rais wa Chama cha Mawakili Zanzibar (Zanzibar Law Society ) Katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria Zanzibar Tarehe 12 FEB, 2018

Rais wa Chama cha Mawakili Zanzibar Mhe. Omar Said Shaban akitowa Salamu za Chama cha Mawakili Zanzibar wakati wa hafla ya Maadhimisho ya Siku ya Sheria Zanzibar, ilioadhimishwa katika Ukumbi wa Zamani wa Baraza la Wawakilishi Kikwajuni Zanzibar. 


Mhe. Dr Ali Mohammed Shein – Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
Mh. Omar Othman Makungu – Jaji Mkuu wa Zanzibar
Mh Issa Haji Ussi Gavu, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
Dr Abdulhamid Yahya Mzee, Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi
Mh. Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania
Waheshimiwa Majaji wa Mahakama Kuu Zanzibar mliokuwepo pamoja na Naibu Kadhi Mkuu wa Zanzibar
Mh. Naibu Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar na Naibu Mkurugenzi wa Mashtaka
Mh. Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi
Waheshimiwa Mahakimu na Makadhi wa ngazi zote za Mahakama za Zanzibar
Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea na Wanasheria wote mliopo

Naomba nitambue pia uwepo wa Ma Naibu Katibu Wakuu wa Wizara ya Katiba Sheria Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Kaimu Mrajis wa Mahakama Kuu ya Tanzania pamoja Mtendaji Mkuu wa Mahakama Kuu ya Tanzania

Lakini pia nachukua fursa hii kuwapongeza wasanii wetu wa Utenzi na Igizo kwa kazi Yao yenye ujumbe maridhawa ambao bila ya Shaka unatupa nafasi ya kutafakari zaidi juu ya changamoto zilizopo kwenye jamii na namna ya kukabiliana nazo.                `

Mheshimiwa Mgeni

Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia kukutana tena Leo ikiwa ni muendelezo wa utaratibu uliowekwa na Mahakama wenye kuashiria kuanza kwa mwaka mpya wa Mahakama. Mkusanyiko kama huu unatupa fursa ya wadau wote katika Uga wa Sheria kukumbushana wajibu wetu katika maeneo mbali mbali kwa lengo moja tu: Kujenga Zanzibar yetu katika maendeleo iwe ya kiuchumi, kisheria na hata kisera.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Kauli mbiu ya Mwaka huu ni “ Imarisha Utawala wa Sheria kwa Kukuza Uchumi wa Nchi”.  Niwapongeze wote waliokuja na wazo la kauli mbiu hii maana imekuja katika wakati muafaka kwa mahitaji ya Wakati tulionao. Imekuja katika wakati ambao serikali yako inafanya kila aina ya jitihada katika kukuza uchumi wa Zanzibar na kuwakomboa wananchi kutoka kwenye dimbwi la umasikini. Imekuja katika wakati ambao Nchi yetu ipo kwenye utekelezaji wa mipango na mikakati mbali mbali ya utafutaji wa Rasilimali mafuta na Gesi ambazo kama itagundulika kuwepo katika Nchi yetu basi kutakuwa na transformation kubwa ya aina ya uchumi tulionao na kuiweka nchi yetu na watu wake katika kundi la Kati la kipato (Middle income state).

Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Mipango na mikakati yote hii haitaweza kuwa endelevu na yenye maslahi kwa Nchi yetu ikiwa hatutakuwa na Sheria Nzuri lakini pia hata Sheria Nzuri zikiwepo, hatutakuwa na watu au taasisi zinazoheshimu Sheria ziliopo. Hivyo Kauli mbiu yetu hii ya Leo inaweza kutafsiriwa na kujadiliwa katika muktadha wa aina mbili. Kuwepo kwa Sheria zenye kuchochea uchumi wa Nchi na Kuheshimu Utawala wa Sheria ili tukuze uchumi wa Nchi.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Wote tukubaliana kuwa kama Nchi tuna changamoto katika maeneo yote mawili. La Sheria ambazo utumikaji wake zinazorotesha ukuaji wa uchumi wa Nchi na watu ama Taasisi ambazo ni wagumu kufuata Sheria na hatimae kuzorotesha Uchumi wa Nchi. Lakini pia Kinyume chake ni Sahihi, yaani tunazo Sheria ambazo ni bora na nguzo muhimu katika ukuzaji wa Uchumi na wapo watu na taasisi ambazo siku zote wanajitolea katika kufata Sheria ili kulinda Uchumi na Maslahi ya Nchi. Hawa wanahitaji kupongezwa na kutiwa moyo.

Mheshimiwa Rais
Ni dhana inayokubalika duniani kote na hata Serikali yako kuwa pale fursa za kiuchumi na utulivu wa kisiasa unapokuwepo, na mfumo wa sharia unaoheshimu utawala wa Sheria basi huvuta wawekezaji wa Kigeni na Biashara za kimataifa. Utawala wa Sheria ni muhimu katika uchumi wa soko kwa sababu kigezo cha msingi ambacho wanaohusika katika uwekezaji wanaweza kufanya makubaliano ya kibiashara na kujenga imani kuwa pale panapokuwa na migongano basi wanaweza kutatua kwa njia ya ufanisi, uwazi na usawa. Pale tunapokuwa na Sheria ambazo zenye kueleweka na kutabirika, zenye kuainisha Haki na wajibu wa kila mtu katika shughuli za uwekezaji na uchumi, basi ni rahisi kuvutia wawekezaji na kuimarisha shughuli za kiuchumi nchi kwetu na kinyume chake ndio hivyo hivyo.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi,

Ni miaka nane sasa tangu report ya Bank ya Dunia kuhusu urahisi wa kufanya Biashara Zanzibar imetoka. Katika report hiyo, mamlaka 183 za kiuchumi (world economies) zililinganishwa na Zanzibar ambapo vigezo 9 viliangazwa na Zanzibar kushika nafasi ya jumla 155 kati ya chumi 183. Katika vigezo vilivyoangazwa, vipo ambavyo moja kwa moja vinahusu sheria na sera na vipo ambavyo vinahusu utendaji tu wa kila siku. Ni jambo la faghari kwetu kuwa Zanzibar tulifanya vizuri sana kwatika baadhi ya vigezo kama vile utiliaji nguvu wa utekelezaji wa mikataba ambapo tulishika nafasi ya 37 kati ya 183 huku tukiwa wa pili kati ya 35 kwa uchumi mdogo wa visiwa tukiwa nyuma ya Singapore.

Vipo vigezo vengine kama vile Vibali vya Ujenzi, ulipaji kodi, uanzishaji wa biashara, ulindaji wa wawekezaji, upatikanaji wa mikopo na ufungaji wa biashara.  Vyote hivyo, performance yetu imekuwa ikitofautiana kwa sababu mbali mbali.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Napenda kuchukua fursa kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa hatua madhubuti walizochukua katika kuboresha yale maeneo ambayo report imeonesha hatukufanya vizuri lakini pia kutobweteka katika maeneo ambayo report imeonesha Zanzibar inafanya vizuri. Hatua zenyewe ni kama vile kuanzisha Sheria mpya ya Makampuni na usajili wa Biashara, Kuanzisha kitengo cha Mahakama ya Biashara cha Mahakama Kuu, kuanzisha mamlaka ya usimamizi wa mamlaka za leseni na kadhalika. Jitihada zote hizi zipo zilizotoa matunda ya wazi wazi na zipo ambazo bado zinakubwa na changamoto katika utekelezaji wake.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Mathalan katika kigezo cha kuanzisha Biashara (registering business) ambacho report ilionesha kuwa Zanzibar inashika nafasi ya 162 kati ya 183 kwa kuanisha ugumu wakati wa kuanzisha biashara na baada ya uanzishaji wake, binafsi kama mtaalamu wa sharia za makampuni na Biashara (Corporate Lawyer), napenda kukuthibitisha kwa dhati Mheshimiwa Rais kuwa tumepiga hatua kubwa sana tangu kutungwa kwa sharia mpya ya Makampuni na ambayo nafahamu Kanuni zake zipo tayari. Ushuhuda wangu unakwenda katika zama ambazo kusajili kampuni kulikuwa kunachukua hadi wiki mbili na wakati mwengine inachelewa kwa sababu printer ya kutolea cheti cha usajili haina wino, lakini leo binafsi nimeshuhudia kampuni ikisajiliwa ndani ya masaa mawili kutoka muda ambao nyaraka zimewasilishwa. Ninaamini ikiwa leo Bank ya Dunia watatufanyia tena tathmini, basi Zanzibar itashika nambari moja.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Napenda kuchukua fursa hii kuipongeza kwa dhati kabisa Wakala wa Usajili wa Biashara na Mali (BPRA) hasa kitengo cha usajili wa makampuni kwa mabadiliko makubwa ya kiutendaji wanayoyafanya. Ni matumaini yangu vitengo vyengine hasa kile cha usajili wa asasi za kiraia kitabadilika katika utendaji wake wa kazi. Utendaji kazi wa namna ya Wakala wa Usajili wa Biashara na Mali Zanzibar ukiigwa na taasisi nyengine basi ni wazi kuwa ukuaji wa Uchumi wa Zanzibar utakuwa katika nafasi nzuri Zaidi.


Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Pamoja na Report ya Bank ya Dunia kutuweka katika nafasi za juu katika eneo la enforcement of legal contracts na serikali kuchukua hatua ya kuanzisha Mahakama ya Biashara, bado tuna changamoto ya utendaji katika Mahakama yetu hii. Mahakama ya namna hii duniani kote inahitaji vifaa vya kisasa katika uendeshaji wa mashauri yake ili kuitofautisha na Mahakama nyengine. Naomba nichukue fursa hii kuiomba serikali yako kuitupia jicho Mahakama hii na kuijengea uwezo na nyenzo ili ijitofautisha na kuvutia wawekezaji wengi Zaidi kuona ndio mahakama sahihi kwa utatuzi wa migogoro yao wakiwa na uhakika kuwa mashauri yataenda kwa kasi na uwazi ili mipango yao ya uwekezaji isikwame kwa kigezo cha kuwa na kesi mahakamani.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Kama nilivyosema awali, kuwa kauli mbiu yetu inaweza kutafsiriwa katika muktadha wa aina mbili, ule wa kuwa na sheria zenye kuchochea kukuza uchumi na muktadha wa pili ni ule wa kuwa na watu au taasisi ziwe za serikali au binafsi zenye utamaduni wa kufata sheria ili kukuza uchumi.

Zipo baadhi ya Taasisi au wakuu wa Taasisi ambao kwao wao kufuata Sheria zilizowekwa wamekuwa wagumu na matokeo yake wanazorotesha ukuaji wa uchumi. Kwa mfano, baadhi ya watendaji wa mamlaka ya serikali za mitaa na wakati mwengine hata serikali kuu wamekuwa na tabia ya kuwabughudhi wawekezaji kwa sababu ambazo nyengine hazipo kisheria au wangekuwa na njia bora ya kuzitatua kwa kutumia mamlaka waliyonayo kwa mujibu wa sheria lakini wao wamekuwa ama sehemu ya migogoro ama kichocheo cha migogoro na hatimae kupelekea kuibuka migogoro ya kisheria inayokwenda Mahakamani huku aidha ikisitisha shughuli za kiuchumi au kuzizorotesha.

Wapo wengine hawaoni tabu hata kuagiza kufutwa kwa vibali vya uwekezaji na kupendekeza Mwekezaji aondoshwe nchini bila ya kufata utaratibu uliowekwa na sheria au kufanya mashauriano na mamlaka nyengine zinahusika za kiuchumi kama vile za kodi au uwekezaji. Mara nyingi utasikia Muekezaji huyu hana maelewano na wananchi lakini ukichunguza pengine sintafahamu ipo baina ya kikundi kidogo kwenye jamii husika ambacho kinaushawishi katika mamlaka Fulani.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Hali hii isipodhibitiwa, itajenga hofu kwa watu wanaotaka kuekeza kwenye Nchi yetu maana hawatojua siku wala saa watakayoambiwa waondoke nchini kwa kigezo cha “kutotakiwa na wananchi wanaozunguka miradi” Zanzibar Law Society hatukusudii kusema kuwa wawekezaji waachiliwe hata pale wanapokuwa kero kwa wananchi wenzetu, HAPANA! Tunachokisisitiza ni umuhimu wa kufuata utaratibu wa Sheria katika kukabiliana na kero za namna hiyo. Nchi yetu inaongozwa na Katiba lakini pia kupitia Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeridhia mikataba mbali mbali ya Kimataifa yenye kulinda Wawekezaji na Uwekezaji. Si vyema jithada za Serikali katika kuwaalika wawekezaji kuja nchini zikatiwa doa na watu wachache ambao hawajui athari za matendo yao.

Mheshimiwa Mgeni Rasmi

Mifano ya changamoto za namna hii ipo mingi na sio rahisi kuieleza yote kwenye jukwaa hili, jambo la muhimu kwa wadau wote wa Sheria waliopo hapa na wanaofatilia kwenye vyombo vya habari kutafakari kwa kina maana ya Kauli mbiu yetu ya leo na kuitafsiri kwa muktadha wa maeneo yao ya kazi na shughuli zao za kiuchumi iwe serikalini ama sekta binafsi kwa lengo moja tu, nalo ni kuangalia maslahi mapana ya Nchi yetu.

Nimalizie kwa kunukuu maneno ya aliyekuwa waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Bi Hillary Clinton ya mwezi August 2009 wakati anazindua Makubaliano ya Uwekezaji baina ya nchi yake na Nchi ya Mauritius alipoimwagia sifa nchi hiyo kwa kusema

“Mauritius has taken steps in recent years to attract investment by enacting reforms that protect investors and promote business. They have made it easier to launch start-ups, to access credit and to register property. They have demonstrated a commitment to transparency. Accountability and good governance. Mauritius has attracted more investment in the last three years than it did in the preceding twenty years”

Mheshimiwa Mgeni Rasmi, Zanzibar haina tofauti sana na Mauritius, sifa wanazomwagiwa na Jumuiya ya kimataifa tunaweza kuzipata na sisi. Inawezekana ikiwa kila mtu atatimiza wajibu wake.

Ahsante kwa kunisikiliza

Omar Said Shaaban
Rais – Zanzibar Law Society


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.