Habari za Punde

Mwenyekiti wa CCM Dk Magufuli afungua mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC)

Dar-es-Salaam.   
              
MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa,na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli amefungua mkutano wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) na kuwapongeza wajumbe wa mkutano huo kwa kuchaguliwa na kushiriki kikamilifu katika mkutano huo.

Mwenyekiti huyo wa CCM aliyasema hayo leo wakati alipokuwa akifungua kikao cha kwanza cha Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano Ikulu Jijini Dar-es-Salaam.

Katika maelezo yake, Rais Magufuli aliwahakikishia Wajumbe hao kuwa ataendelea kushirikiana nao kwa maslahi ya CCM katika kuhakikisha chama hicho kinazidi kupata mafanikio na maendeleo zaidi.

Aidha, Rais Magufuli alitumia fursa hiyo kueleza mafaniko yaliopatikana katika utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara.

Katika kikao hicho, Rais Magufuli pamoja na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein waliwahakikishia viongozi hao wa NEC pamoja na wananchi wote wa Tanzania kuwa wataendelea kuusimia na kuuimarisha Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa nguvu zao zote.

Viongozi hao walitumia fursa hiyo kuwaeleza Wajumbe hao wa NEC kutumia muda wao kuwaelimisha viongozi wa CCM pamoja na wananchi wote wa Tanzania juu ya umuhimu, malengo na faida za Muungano huo wa Tanganyika na Zanzibar.

Katika Mkutano huo, Wajumbe wa NEC waliridhia majina ya Wajumbe wapya wawili aliowateuwa na Rais Magufuli hivi karibuni kutokana na nafasi zake katika wadhifu wake wa Mwenyekiti wa Taifa wa CCM ambao ni Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Peter Pinda na Charles Makongoro Nyerere.

Rais Magufuli alitumia fursa hiyo kueleza uzoefu wa Wajumbe hao wapya ndani ya chama hicho na kueleza jinsi walivyoweza kukitumia hadi hivi leo.

Pia, katika Mkuno huo wa NEC, Wajumbe walifanya uchaguzi wa kuwachagua wajumbe wa  Kamati Kuu ya CCM Taifa (CC) kwa upande wa Tanzania Bara na Zanzibar.

Wajumbe waliokuwemo katika kinyanganyiro hicho jumla yao walikuwa tisa kwa kila upande wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ambapo kwa upande wa Tanzania Bara aliekuwemo ni Burton Kihaka Lumuliko, Charles Makongoro Nyerere, Ernest Samson Sungura.

Wengine ni Jackson William Msome,Komanya Eric Kitwala, Mizengo Kayanza Peter Pinda, Richard Bundala Charles, Khadija Shabaan Taya (Keisha) na  Theresia Adriano Mtewele.

Kwa upande wa Zanzibar waliekuwemo katika kinyanganyiro hicho ni Afadhali Taibu Afadhali, Bakar Hamad Khamis, Cassin Galos Nyimbo, Kombo Hassan Juma, Ramadhan Abdalla Shaaban, Ramadhan Shaibu Juma, Kidawa Hamid Saleh na Lailah Burhan Ngozi.

Waliochaguliwa kwa upande wa Tanzania Bara kuwa Wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa  (CC) ni Mizengo Kayanza Peter Pinda, Charles Makongoro Nyerere na Khadija Shaban Taya (Keisha).

Kwa upande wa Zanzibar waliochaguliwa kuwa Wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa (CC) ni Kombo Hassan Juma, Afadhali Taibu Afadhali, Lailah Burhan Ngozi na Waride Bakari Jabu.

Mapema Mwenyekiti wa CCM Taifa Dk. John Pombe Magufuli alieleza kuwa CCM ni chama cha watu wote  wa rika zote, jinsia zote  wakiwemo wakulima na wafanyakazi.

Pia, Rais Magufuli alieleza kuwa Tanzania iko vizuri katika uchumi wake ambapo kwa mwaka 2018 hadi 2030 ni miongoni mwa nchi nne duniani ambazo uchumi wake unakua kwa kasi kuelekea uchumi wa kufikia asilimia 7.1 ambapo kwa hivi sasa tayari umeshafikia asilimia 7.

Nae Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliwahakikishia Wajumbe wao wa NEC kuwa ataendelea kushirikiana nao, kuwatumikia wao pamoja na kuwatumikia  wanaCCM na wananchi wote wa Tanzania.

Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kueleza mafanikio makubwa yaliopatikana katika kuimarisha uchumi wa Zanzibar na juhudi zinazoendelea katika kuhakikisha uchumi huo unaimarika zaidi.

Wakati huo huo, Wajumbe hao wa NEC waliridhia kustaafu wa Katibu Mkuu wa Chama hicho Abdulrahman Kinana ambaye amemuomba Mwenyekiti huyo wa CCM Taifa kustaafu.

Kwa mujibu wa barua iliyoandikwa na Katibu Mkuu huyo wa CCM na kusomwa na  Mwenyekiti wa CCM Taifa, Dk. Magufuli mbele ya Wajumbe hao wa NEC, Katibu Kinana alieleza sababu zilizompelekea kustaafu kwake ambazo zilikubaliwa na Mwenyekiti huyo, Makamu wake wote wawili pamoja na Wajumbe hao wa NEC.

Akimpongeza Katibu Mkuu huyo kwa ujasiri wake mkubwa wa kukipenda Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Magufuli alieleza kuwa Katibu Mkuu huyo aliyestaafu amejituma sana na ameonesha jinsi anavyokipenda chama hicho na katika maisha yake yote amekuwa akihakikisha CCM inashinda na inaendelea kubaki madarakani.

Mwenyekiti huyo wa CCM Taifa alieleza kuwa CCM haitamsahao Katibu huyo mstaafu na wala haitomtupa na itaendelea kushirikiana nae katika kuhakikisha chama hicho kinaimarika zaidi.

Nae Katibu Mkuu huyo Mstaafu akitoa neon la shukurani, alimpongeza Rais Magufuli, aliwapongeza Makamu Wenyeviti wote wa CCM wa Bara na Zanzibar, Wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa pamoja na wanachama wote wa CCM kwa kufanya kazi nao vizuri katika wakati wake wote wa kazi.

Alieleza jinsi alivyojitolea na kusafiri masafa marefu Bara na Zanzibar katika kukimarisha chama hicho na hatimae kuendelea kupata ushindi na kuwataka Wajumbe hao wa NEC kuisoma sana Katiba ya CCM, Kanuni na miongozo mbali mbali inayotolewa na Chama hicho.

Sambamba na hayo, alisisitiza kuwa nguvu ya CCM ipo kwenye umoja na kueleza haja ya kuimarisha umoja na kuwataka viongozi wa CCM kutambua kuwa ndani ya CCM kuna kundi moja tu ambalo ni CCM huku akitumia fursa hiyo kuwapongeza wanahabari kwa ushiriki wao mzuri katika kutoa habari juu ya chama hicho hasa pale alipozunguka nchi nzima katika kukiimarisha.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.