HOTUBA YA MAONI YA KAMATI YA FEDHA, BIASHARA NA
KILIMO KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA YA KILIMO, MALIASILI, MIFUGO
NA UVUVI KWA MWAKA WA FEDHA 2018/2019
Mheshimiwa Spika,
Kwa heshima kubwa
natanguliza shukurani zangu za dhati kwa Mwenyezi Mungu Mtukufu ambae ametujaalia
kufika hapa kwa mara nyengine tukiwa wazima na wenye afya njema. Namuomba tena Mwenyezi
Mungu akuzidishie wewe Mheshimiwa Spika busara, hekma na uadilifu katika
kutuongoza na sisi pia atujaalie tuendelee kuwa
na nguvu na ari ya kuitekeleza vyema Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya
mwaka 2015 - 2020 pamoja na malengo tuliyojipangia ili tuweze kutoa huduma bora
kwa Wananchi wetu.
Mheshimiwa Spika,
Kwa namna ya
pekee nachukua fursa hii kumpongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein kwa ujasiri wake wa kutekeleza vyema
jukumu zima la uongozi wa nchi hii sambamba na jitihada anazochukua za
kuendeleza sekta ya kilimo na sekta nyengine hapa nchini. Aidha, tunatoa
shukurani za dhati kwa Makamo wa Pili wa Rais, Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi
kwa busara zake na ushauri anaompatia Mheshimiwa Rais katika utekelezaji wa mambo
mbali mbali kwa ustawi wa nchi na wananchi wetu. Kadhalika, tunamshukuru
Mheshimiwa Balozi kwa kusimamia vyema shughuli za Baraza hili akiwa ni kiongozi
wa shughuli za Serikali ndani ya Baraza la Wawakilishi.
Mheshimiwa Spika,
Nitakuwa mkosefu wa shukurani iwapo nitashindwa kuthamini
juhudi zinazochukuliwa na Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo
na Uvuvi hususan kwa kuvuka lengo la makusanyo ya mapato kwa kukusanya zaidi ya
asilimia 165 ukilinganisha na mwaka uliopita. Hili limechangiwa zaidi na
usimamizi mzuri wa kuhakikisha uvujaji wa mapato unadhibitiwa hususan mapato ya
uchimbaji mchanga. Kamati inaisisitiza Wizara isije ikalewa sifa wanazopewa na
badala yake kuongeza juhudi na maarifa ya kuibua mbinu mbadala
zitakazohakikisha zinawafikisha katika malengo yaliyopangwa kwa mwaka huu wa
fedha wa 2018/2019.
Mheshimiwa Spika,
Kwa huzuni kubwa
napenda kuwapa pole Wananchi wetu wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla kutokana
na maafa ya mvua za msimu huu wa Masika zilizoathiri mali, Makaazi ya Wananchi
wetu pamoja na kusababisha baadhi ya Watu kupoteza maisha. Kwa niaba ya Kamati
yetu ya Fedha, Biashara na Kilimo nasi hatuna budi kuwaomba Wananchi hao wawe
na moyo wa subira na uvumilivu hasa katika kipindi hiki kigumu. Aidha, naiomba
Serikali na Taasisi binafsi kuendelea kuchukua juhudi za kuwajali na
kuwathamini Wananchi hao kwa kuwapatia misaada ya hali na mali.
Mheshimiwa Spika,
Kwa heshima
na taadhima, kwa kutambuwa mchango na ushauri mkubwa katika kutekeleza kazi za Kamati
hii, naomba sasa niwatambue kwa kuwataja majina yao Waheshimiwa Wajumbe
wafuatao wa Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo:-
1.
|
Mheshimiwa
Yussuf Hassan Iddi
|
-
|
Mwenyekiti;
|
2.
|
Mheshimiwa
Hamida Abdalla Issa
|
-
|
Makamo
Mwenyekiti;
|
3.
|
Mheshimiwa
Hamad Abdalla Rashid
|
-
|
Mjumbe;
|
4.
|
Mheshimiwa
Moh’d Mgaza Jecha
|
-
|
Mjumbe;
|
5.
|
Mheshimiwa
Ali Salum Haji
|
-
|
Mjumbe;
|
6.
|
Mheshimiwa
Ussi Yahya Haji
|
-
|
Mjumbe; na
|
7.
|
Mheshimiwa
Bihindi Hamad Khamis
|
-
|
Mjumbe.
|
Aidha, Kamati yetu pia inafanyakazi kwa kusaidiana na
makatibu ambao kwa kiasi kikubwa wamekuwa wakitusaidia kutekeleza majukumu
yetu, kwa heshima naomba niwatambue makatibu hao ni:
1.
|
Ndugu Asma Ali
Kassim
|
-
|
Katibu
|
2.
|
Ndugu Said
Khamis Ramadhan
|
-
|
Katibu
|
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu ilipitia,
kujadili na hatimae kupitisha Makadirio ya Fungu L01 la Wizara ya Kilimo, Maliasili,
Mifugo na Uvuvi tarehe 04/05/2018 baada ya kuelekeza kufanyiwa marekebisho kutokana
na kuwepo utofauti katika jumla ya Makadirio ya Matumizi ya shilingi 2.54 bilioni ambapo jumla ya shilingi 65.16 bilioni yaliainishwa katika
Makadirio ya Matumizi ya Kitabu cha Mswaada wa Makadirio ya Mapato na Matumizi
ya Bajeti ya mwaka 2018/2019 ambacho Kamati ilikabidhiwa na Ofisi katika ngazi
ya Kamati na jumla ya shilingi 62.62
bilioni iliyoainishwa ndani ya kitabu cha Hotuba ya Waziri, Tofauti hiyo
imesababishwa zaidi na fedha hizo kuhamishiwa Serikali za Mitaa kwa ajili ya
ulipaji wa maslahi ya wafanyakazi waliogatuliwa kutoka Wizara hii ya Kilimo. Kwa
ruhusa yako na kwa niaba ya Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo naomba
niwasilishe mbele ya Baraza Lako Tukufu maoni ya Kamati yetu kuhusiana na
Programu Kuu na Programu ndogo za Wizara hii kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Spika,
Kiujumla, bajeti
ya makusanyo ya mwaka huu ya Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi imeongezeka
maradufu ukilinganisha na bajeti ya mwaka jana. Kwa mwaka 2017/2018, Wizara hii
ilipangiwa kukusanya jumla ya shilingi 4.93
bilioni ukilinganisha na makadirio ya mapato ya shilingi 12.50 bilioni ya mwaka ujao 2018/2019 sawa
na ongezeko la shilingi 7.57 bilioni
ya makadirio ya mapato. Hii inaonesha wazi kwamba kiwango cha makadirio ya
makusanyo waliyopangiwa Wizara hii ni kikubwa sana kwani ni zaidi ya mara mbili
ya kile kiwango walichopangiwa mwaka jana ukiachia mbali kuvuka lengo la
mkusanyo kwa kukusanya shilingi 7.7
bilioni. Kamati inaishauri Serikali iangalie vizuri makadirio ya makusanyo
waliyoipangia Wizara hii kwani inaonekana wazi sio rahisi kufikia lengo hilo
kwa asilimia mia moja hasa ukizingatia hakuna vyanzo vipya vya mapato ilivyoongezeka.
Mheshimiwa Spika,
Lakushangaza,
pamoja na kuongezewa kiwango cha mapato yanayohitajika kukusanywa na Wizara hii
lakini wamepunguziwa matumizi. Mwaka huu Wizara hii imepangiwa kutumia jumla ya
shilingi 62.62 bilioni ukilinganisha
na shilingi 70.61 bilioni za mwaka jana. Hii ni sawa
na punguzo la shilingi bilioni 8. Kwa vile Wizara ya Kilimo ndio
uti wa mgongo unaotegemewa na wananchi wetu katika sekta husika za kilimo,
Maliasili, Mifugo na Uvuvi, punguzo hilo litakuwa na athari kwa kipato cha
wananchi wetu na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika,
Sambamba na
hilo, Kamati yetu ilipata mashaka kidogo ilipokuwa ikipitia kwa undani
makadirio ya mapato ya Mauzaji ya Mazao na Miche kinachokusanywa na Taasisi ya
Utafiti wa Kilimo - Kizimbani (kifungu
1423002). Chanzo hiki kilipangiwa shilingi 20,000,000 milioni kwa mwaka jana ambapo mwaka huu kimepangiwa kukusanya
shilingi 70,000,000 milioni sawa na
ongezeko la shilingi 50,000,000 milioni,
baada ya kukitathmini chanzo hiki cha mapato, Kamati iliona Wizara imepangiwa
fedha nyingi kuliko uhalisia wake. Kamati inaishauri Serikali kuyaangalia upya
makadirio ya makusanyo ya chanzo hicho cha mapato kwa kupanga kiwango
kinacholingana na uhalisia wa upatikanaji wa mapato kupitia chanzo hicho.
PROGRAMU KUU YA MAENDELEO YA KILIMO
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu
imegundua kwamba kuna wakulima wengi wameathiriwa na mvua za masika zilizokuwa
zikiendelea kwa kuharibu maeneo wanayatumia kwa kilimo pamoja na mazao yao
kutokana na kujaa kwa maji. Aidha, kuna miundombinu mingi ya barabara ambayo
nayo imeharibika inayowasaidia wakulima wetu kusafirishia mazao yao kutoka
maeneo wanayolima. Kamati yetu inaishauri Wizara hii ya Kilimo kukaa na Taasisi
zinazoshughulikia Maafa na utengenezaji wa miundombinu ya barabara ili kutatua
changamoto hizo ikiwa ni pamoja na kuwapatia wakulima wetu fedha kidogo kufidia
athari waliyoipata ili wakulima wetu waweze kupata faraja kutokana na hasara
waliyoipata.
Mheshimiwa Spika,
Suala la
uimarishaji wa kilimo cha umwagiliaji maji katika nchi yetu ni jambo la msingi
ambapo Wizara ya Kilimo imekuwa ikilifanyia kazi kwa juhudi kubwa hususan
katika kuimarisha kilimo shadidi. Kamati inaipongeza Wizara ya Kilimo kwa
kuongeza uzalishaji wa mpunga kutoka tani 2.5
kwa mwaka jana hadi tani 6.8 mwaka 2017/2018
kwa hekta kwa kutumia kilimo cha teknolojia ya Shadidi. Kamati inaishauri
Wizara hii kuendelea na juhudi hizo za kuwahamasisha wakulima wetu ili waweze
kuhamasika na kulima zaidi kilimo hicho cha kibiashara.
Mheshimiwa Spika,
Licha ya
juhudi kubwa zinazochukuliwa na Wizara hii ya Kilimo ya kununua matrekta mapya
20 na kupokea matrekta mengine 10 kutoka nchi ya Libya, bado wakulima wetu
wanakabiliwa na changamoto ya kutolimiwa eka zao za mpunga kwa wakati na
hatimae huambulia kupata mavuno machache. Kamati imeelezwa na wataalamu wa Kilimo
kwamba, ili sekta ya kilimo ipige hatua kwa kuwa na matrekta ya kutosha basi
kunahitajita yapatikane matrekta 80 ambapo Serikali yetu tayari imeshaingia
Mkataba na Kampuni ya kutengeneza Matrekta (Mahindra) iliyopo nchini India wa
kuipatia nchi yetu Matrekta 100. Hivyo, tunaiomba Serikali yetu sikivu
kuharakisha upatikanaji wa nyenzo hizo ili wakulima wetu waepukana na kilimo
cha jembe kongoroka mpini.
Mheshimiwa Spika,
Wakati Kamati
yetu ilipokuwa ikipitia Makadirio ya Matumizi ya Programu hii ya Maendeleo ya
Kilimo iligundua kwamba Wakala wa Huduma za Matrekta na Zana za Kilimo
haikupangiwa pesa, Kwa kuthamini na kutambua umuhimu wa Wakala huo hususan
katika kuwasaidia wakulima wetu kulimiwa na kuburugiwa mashamba na eka zao za
kilimo cha mpunga, Kamati iliishauri Wizara hiyo kuipangia pesa za kutosha
Wakala huo ili uweze kuleta faraja kwa wananchi wetu. Hatimae Wakala huo
ulipangiwa jumla ya shilingi 1.38
bilioni ambazo japo kwamba hazitoshi lakini angalau wataweza kuendelea kutekeleza
majukumu yao waliyojipangia.
Mheshimiwa Spika,
Katika
Programu Kuu ya Maendeleo ya Kilimo kuna Programu Ndogo ya Umwagiliaji Maji
ambayo imepangiwa kutumia fedha kidogo shilingi
10.11 bilioni kwa mwaka wa fedha 2018/2019 ukilinganisha na shilingi 27.15 bilioni za mwaka 2017/2018.
Kamati ilielezwa kwamba fedha hizo zitatumika katika ujenzi wa miundombinu ya
maji. Hata hivyo, Kamati yetu ilitaka kujua miundombinu hiyo itajengwa wapi na
kwanini kifungu hicho kimepungua kwa takriban shilingi 17.04 bilioni. Punguzo hili ni kubwa pamoja na kwamba fedha
nyengine zitafidiwa kupitia mradi wa Maendeleo unaofadhiliwa na Washirika wa
Maendeleo ambapo utegemezi wa fedha hizo hauna uhakika zaidi. Kwa kuelewa
umuhimu uliowekwa na Serikali yetu ya kuhimiza kilimo cha kibiashara cha
umwagiliaji maji, ni busara kifungu hicho kikaongezewa bajeti ili kiedane na
utekelezaji wa azma hiyo.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu
pia ilihoji kifungu kinachotoa Huduma za Utibabu wa Mimea na Karantini na
Ukaguzi wa Mazao (HL01010303) kwamba
kimepangiwa fedha nyingi mno shilingi
113.11 milioni kwa mwaka huu 2018/2019 ukilinganisha na shilingi 3.06 milioni za mwaka jana 20017/2018 sawa na tofauti ya shilingi 110.04 milioni. Fedha hizo
zinaonekana kuwa nyingi pamoja na kwamba matibabu hayo yanafanyika nchi nzima.
Mheshimiwa
Spika,
Wakulima wetu
ni masikini sana ambao wanahitaji msukumo wa hali ya juu kutoka Serikalini ili
kuimarisha kilimo kwa lengo la kujipatia kipato bora kitakachowasaidia wao
wenyewe, familia zao na Taifa letu. Katika kuhakikisha hilo linafanyika, Kamati
yetu inaendelea kuipongeza Wizara ya Kilimo kwa utekelezaji mzuri wa shabaha ya
ununuzi wa tani 900 za mbolea ya kupandia mpunga na tani 900 kwa ajili ya
kukuzia mpunga, tani 170 za mbegu na lita 17,400 za dawa ya kuulia magugu
ambazo zimesambazwa Unguja na Pemba. Pamoja na juhudi hizo, bado kuna
changamoto kubwa inayowakabili wakulima wetu ya kukosa baadhi ya pembejeo hizo.
Kamati yetu ilithibitisha hilo ilipotembelea bonde la Pangeni na kukuta
msongomano wa wakulima wakifuatilia ugawaji wa dawa za kuulia magugu. Kamati
yetu haikuridhishwa na utaratibu uliokuwa ukitumika kwani dawa hizo zilikuwa
zikitolewa kwa wakulima wa Pangeni na kuwaacha wakulima wa Kilombero na Upenja
wakilalamika. Aidha, hao wakulima waliopatiwa dawa hizo walipatiwa nusu ya
mahitaji yao.
PROGRAMU KUU YA MAENDELEO YA MIFUGO
Mheshimiwa Spika,
Programu Kuu
hii inayo Programu Ndogo ya Wakala wa Tafiti za Mifugo inayohusiana kufanya
Tafiti za Mifugo (kifungu kidogo SL010303). Mwaka 2017/2018 kifungu
hicho kinaonekana hakijapangiwa fedha lakini mwaka 2018/2019 kimepangiwa
shilingi 829 milioni. Kamati ilitaka
ufafanuzi na kuelezwa kwamba masuala ya tafiti za mifugo zimeundiwa Idara yake
na fedha za kutekeleza shughuli hiyo zitapatikana katika Idara husika. Kamati
inashauri Idara hiyo ipangiwe fedha za kutosha kwani bila ya kufanyika tafiti
za mifugo, Wizara haitoweza kupiga hatua mbele kwa vile mifugo yetu
inasumbuliwa na maradhi ya aina tofauti.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu
imeshangazwa na kusikitishwa sana na vitendo vya baadhi ya watendaji wa Wizara
ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi kwa kushindwa kutekeleza baadhi ya maagizo
na maelekezo ya Kamati na Viongozi wao, Hili limetokea baada ya Waziri wa
Kilimo aliyepita Mheshimiwa Hamad Rashid Mohammed kuridhia na kukubali
kuipeleka Kamati Bagamoyo kwenda kuliangalia Shamba la Serikali
lililobadilishwa matumizi yake kutoka shamba la Mifugo na kuwa Maeneo yaliyopimwa,
kuchorwa na kugaiwa kwa kazi za Maendeleo. Ni matumaini ya Kamati kwamba kama
ingepata fursa ya kwenda kuliona shamba hilo, baadhi ya changamoto zingeweza
kutatuka kutokana na maelekezo na ushauri ambao Kamati ingeutoa.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu
inaendelea kuitaka Wizara kwamba bado haja ya Kamati kulitembelea shamba hilo
ni ya msingi ili kuweza kujua rasilimali za Serikali zinatumikaje,
zinahifadhiwa vipi na kuendelezwa katika mazingira ya aina gani. Kwa vile Kamati
yetu inafikia ukingoni, tunaishauri Kamati ijayo ya Fedha, Biashara na Kilimo
iitake Wizara ikamilishe ahadi hiyo ili Kamati hiyo iweze kupata fursa ya kulitembelea
eneo hilo na kuishauri Serikali yetu ipasavyo kwa kile watakachokiona na sio
kukaa na kusubiri maelezo ya watendaji wa Wizara pekee. Tunaitanabahisha Wizara
kwamba fedha nyingi za Wakulima na Wakwezi wa nchi hii zimetumika na
zinaendelea kutumika katika uimarishaji wa shamba hilo.
PROGRAMU KUU YA MAENDELEO YA UVUVI
Mheshimiwa Spika,
Katika kuhakikisha
Zanzibar inakuwa na wavuvi wenye ujuzi wa kuweza kuvua uvuvi wa Bahari Kuu,
Wizara imefanikiwa kuwaingiza katika meli za kigeni vijana 26 ili kupata uzoefu
wa namna ya uvuvi huo unavyofanyika. Aidha, wavuvi vijana 25 wamepelekwa Chuo
cha Uvuvi Mbegani - Bagamoyo kujifunza mbinu za uvuvi wa kisasa. Huu ni mwanzo
mzuri ambao Wizara yetu ya Kilimo inahitaji kupongezwa ili rasilimali
tulizonazo Zanzibar ziweze kuvunwa na kutumiwa kwa kuwanufaisha Wazanzibari
wenyewe na sio kuwaachia watu wengine kunyonya utajiri wetu. Kamati inaitaka
Wizara kuwatumia ipasavyo vijana hao kwa maslahi ya Taifa letu na sio kuwawacha
wakazagaa mitaani baada ya kupata ujuzi wao.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yetu inaipongeza
Wizara ya Kilimo kupitia Kampuni ya Uvuvi kwa kuanza vyema utekelezaji wa
majukumu yake kwani tayari Bodi imeshaundwa na kuingiziwa shilingi 2.2 bilioni kati ya jumla ya shilingi 7.0 bilioni za mtaji kutoka kwa Washirika
wake yaani ZSSF, ZSTC, Shirika la Bima la Zanzibar na Shirika la Bandari kulingana
na mgao waliokubaliana. Fedha hizo zimeelekezwa katika ununuzi wa Meli mbili za
uvuvi zitakazokuwa na uwezo wa kuchukua wavuvi sita na kubeba tani 43 za
samaki. Wizara tayari imeanza taratibu za zabuni na ‘quotation’ tayari zimeshatolewa.
Kamati inaendelea kuisisitiza Wizara kuwa makini katika ununuzi huo kwa kununua
meli zitakazokuwa mpya zenye thamani halisi ya fedha zinazohitajika.
Mheshimiwa Spika,
Wizara ya
kilimo imekamilisha ujenzi wa kituo cha kuzalishia vifaranga vya samaki kiliopo
hapo Maruhubi. Kuwepo kwa kituo hicho kutaleta faraja kubwa kwa wafugaji wetu
wa samaki kuweza kupata vifaranga vya uhakika kwa lengo la kuwafuga kibiashara.
Mradi huu ni mkubwa uliogharimu dola za
kimarekani 943.94 milioni na unauwezo wa kuzalisha vifaranga milioni 10 vya
samaki, majongoo 70 elfu na kaa 50 elfu. Kamati inashauri kwamba kwa vile huu
ni mradi unaohitaji kuendelezwa hata baada ya kuondoka wawezeshaji, ni vyema
Serikali ikahakikisha inakuwa na watendaji pamoja na wataalamu wa kutosha
watakaomudu kuvaa viatu vyao ili mradi uweze kuishi na kutupatia faida kwa
kipindi kirefu zaidi.
Mheshimiwa Spika,
Katika
utekelezaji wa kazi za Kamati kwa mujibu wa kanuni zetu, Kamati ilitembelea
kikundi cha wafuga pweza kiliopo Mtende Mkoa wa Kusini Unguja na kuunga mkono
juhudi zinazofanywa na wananchi hao kwa kuwachangia shilingi 1,500,000/- ili waweze kutatua
changamoto zinazowakabili. Kamati iligundua kwamba changamoto kubwa iliyopo
katika kikundi hicho ni kukosa shughuli ya kufanya baada ya kumaliza uvunaji wa
pweza wanaowafuga. Kamati yetu
imekichangia kikundi hicho na kuwashauri waanzishe utaratibu utakaowawezesha
kupata shughuli ya kufanya baada ya kufunga uvunaji wa pweza ikiwemo kulima
kilimo cha migomba na mazao mengine.
PROGRAMU KUU YA MAENDELEO YA RASILIMALI ZA MISITU NA MALIASILI
ZISIZOREJESHEKA
Mheshimiwa Spika,
Kamati
imeridhishwa na hatua zilizochukuliwa na Wizara kwa upande wa Unguja za
kuanzisha na kuuendeleza utaratibu mpya na mzuri wa kulipia malipo ya Mchanga Benki
ya Watu wa Zanzibar (PBZ). Kupitia utaratibu huo, Kamati inawataka Viongozi na
Watendaji wa Wizara hii kuanzisha utaratibu huo katika Kisiwa cha Pemba.
Kadhalika, Kamati imeitaka Wizara kuutumia utaratibu huu katika Rasilimali
nyengine za mawe, kifusi na kokoto ili mianya ya
uvujaji wa mapato ipungue kama si kuondoka kabisa na Serikali kujiongezea
mapato kwani inaonekana mapato mengi yanapotea katika eneo hilo. Aidha, Kamati yetu
inaiomba Serikali iwe inazifuatilia Bei Elekezi za Mchanga inazozitoa ili ziweze
kufuatwa kikamilifu na wauzaji pamoja na wanunuzi wa mchanga huo.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
imeshuhudia ongezeko kubwa la matumizi ya nishati ya kuni linalotokana na
ukataji mkubwa wa miti. Pamoja na juhudu za Wizara za kutoa mafunzo ya kuhimiza
matumizi ya nishati mbadala pamoja na kufanya doria 104 zilizopelekea kukamata
matukio 92 ya ukataji miti, matukio 13 ya ukamataji misumeno ya moto,
kuwasilisha kesi mbili Mahakamani pamoja na kukamata misumeno ya moto 233
Unguja na Pemba lakini bado miti inakatwa sana kwa kutumia misumeno ya moto.
Takwimu zinaonesha matumizi ya nishati ya kuni kwa mwaka huu yamefikia mita za
ujazo 23,114 ukilinganisha na mita
za ujazo wa 19,532.25 za mwaka jana.
Kwa kweli takwimu hizo zinatishia kupotea kwa uoto wetu wa asili. Sambamba na
hilo, Kamati katika kutekeleza majukumu ya kikanuni, ilitembelea msitu wa
mikoko uliopo Ukongoroni na kushuhudia magogo ya mikoko iliyokatwa na kuona
eneo hilo limebakia kuwa tupu. Hali hiyo inasababisha maji ya bahari kupata mwanya
wa kuvamia katika maeneo ya ardhi yanayotumiwa kwa kilimo na makaazi ya
wananchi wetu.
Mheshimiwa Spika,
Lakushangaza,
baadhi ya viongozi wa Serikali akiwemo Sheha wa Shehia ya Ukongoroni alikuwa
mbele kutetea wananchi wake kwamba hawana kazi ya kufanya isipokuwa kujihusisha
na ukataji wa mikoko kwa ajili ya utengenezaji wa kuni na tanu za mkaa. Viongozi
wa namna hii ndio wanaoisababishia Serikali yetu kuonekana haichukui juhudi
yoyote katika harakati za kupambana na uharibifu wa mazingira. Kamati yetu
inaishauri Wizara inayoshughulikia Tawala za Mikoa kumchukulia hatua stahiki
Sheha huyo wa Ukongoroni. Aidha, Kamati inaitaka Wizara ya Kilimo kuchukua
hatua za kudhibiti matumizi ya Misumeno ya moto kama ilivyofanya Kisiwani
Pemba. Kadhalika, Wizara isimamie ipasavyo Sheria ya Uhifadhi wa Maliasili za
Misitu namba 10 ya mwaka 1996 pamoja na Kanuni zake ikiwemo kupiga marufuku
usafirishaji wa kuni kutoka shamba kuja mjini. Hatua hizo kama zitatekelezwa
kikamilifu, basi uteketezaji wa mikoko Zanzibar utabakia kuwa historia.
PROGRAMU KUU YA UENDESHAJI NA URATIBU WA WIZARA YA KILIMO
Mheshimiwa Spika,
Katika
programu hii, kuna kifugu kinachotoa Huduma ya Ununuzi wa Vifaa vya Ofisi (HL01050101) ambacho mwaka jana
kilipangiwa pesa nyingi shilingi 269.63
milioni ambazo hazikukidhi kikamilifu mahitaji ya upatikanaji wa vifaa vya
kutosha katika Wizara hii, lakusikitisha mwaka huu ndio kimezidi kupunguziwa
bajeti. Wakati Kamati yetu ilipokuwa ikipitia kifungu hiki kilikuwa kimepangiwa
shilingi 10.31 milioni sawa na
upungufu wa shilingi 259.32 milioni.
Tunaishukuru Wizara kwa kukiangalia upya kifungu hicho na hatimae kukiongezea fedha
hadi kufikia shilingi 50.32 milioni kama
inavyoonekana katika kitabu tulichokabidhiwa. Pamoja na marekebisho hayo,
Kamati yetu bado inaieleza Wizara kwamba kifungu hicho kinahitaji kuongezewa
tena bajeti vyenginevyo Wizara inaweza ikakosa hata fedha za kununnulia vifaa
vya kutosha vya kuandikia na kuishia kukopa jambo ambalo litaleta picha mbaya
kwa Wizara hii na Serikali kwa ujumla.
Mheshimiwa Spika,
Kamati
inaipongeza tena Wizara hii kwa kufufua matumaini mapya ya kuyaendeleza
mashamba ya mpira ambayo yalikuwa yanatumika kiholela na kuikosesha Serikali
mapato. Kwasasa Wizara ya Kilimo imepanga kuyaendeleza mashamba hayo kwa
kupanda mazao mbadala yakiwemo pililimanga na vanila na kuondosha dhana iliyokuwepo
kwamba mashamba hayo yamezeeka na mipira iliyopo inahitaji kukatwa. Matumizi
mapya hayo yatayaongezea thamani mashamba hayo na kuweza kutumika tena kwa
manufaa ya Taifa letu.
Mheshimiwa Spika,
Kwa namna ya
pekee naomba kutumia nafasi hii kumshukuru na kumpongeza Waziri wa Wizara ya
Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mheshimiwa Rashid Ali Juma; Naibu Waziri
Mheshimiwa Dr. Makame Ali Ussi; Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu pamoja na
Watendaji wengine wote wa Wizara hii kwa juhudi wanazozichukua katika
kutekeleza majukumu yao pamoja na mashirikiano yao ya dhati waliyotupatia
wakati wote wa kupitia na kujadili Bajeti ya Wizara hii. Kwa vile wao ni
Viongozi wapya katika Wizara hii, Kamati inawaeleza kwamba “wasiwe
na sifa kama ya muhogo ambapo ukiwa mtamu sana watu watautafuna mpaka waumalize
na ukiwa mchungu sana watu watashindwa kuutumia”.
Mheshimiwa Spika,
Mwisho
kabisa, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako Tukufu kwa
kunisikiliza kwa utulivu wa hali ya juu wakati wote nilipokuwa nikiwasilisha
hotuba hii. Kwa vile Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo imepitia, imejadili na
kuyakubali mapendekezo ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara hii ya
Kilimo, Maliasili, Mifugo na uvuvi. Sasa naomba nichukue fursa hii kwa mara
nyengine nikuombeni nyinyi Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza hili muijadili, mutoe
ushauri pamoja na mapendekezo yenu na hatimae muiunge mkono bajeti hii ili tumuwezeshe
Waziri kwenda kutekeleza na kufanikisha yale waliyojipangia katika mwaka wa
Fedha wa 2018/2019 na baadae nasi tupate fursa ya kuja kumuhoji kwa kile
alichoingiziwa na matokeo halisi ya kile alichokitekeleza.
Mheshimiwa Spika,
Baada ya
kusema hayo machache, Kwa niaba ya Mwenyekiti na Kamati yetu ya Fedha, Biashara
na Kilimo, naunga mkono hoja.
Mheshimiwa
Spika,
Naomba kuwasilisha.
Asante sana,
……………………..,
Hamida Abdalla Issa,
Makamo Mwenyekiti
Kamati ya Kudumu ya Fedha, Biashara na
Kilimo,
Baraza la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment