Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Ujumbe wa Kampuni ya Ujenzi ya China Civil


UONGOZI wa Kampuni ya Kimataifa ya Ujenzi ya China (CRCC) kupitia Tawi la Kampuni yake ya Uhandisi wa Ujenzi ya nchini humo (CCECC) imeahidi kujenga barabara ya Bububu-Mahonda-Mkokotoni kwa wakati uliopangwa na kwa ubora zaidi ili kuendeleza sifa ya kuwa Kampuni yenye ubora duniani.

Rais wa Kampuni hiyo Zhuang Shangbiao aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake, kiongozi huyo ambaye amefuatana na Rais wa Kampuni ya (CCECC) Zhao Dianlong alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Kampuni yake ya (CCECC), itaijenga kwa kiwango stahiki barabara hiyo yenye urefu wa kilomika 31 kutokana na uzoefu mkubwa uliyonao.

Kiongozi huyo pia, alimueleza Rais Dk.Shein azma ya Kampuni yake ya kuanzisha kiwanda kikubwa cha kusarifu samaki huko kisiwani Pemba.

Pamoja na hayo, uongozi huo ulitoa shukurani kwa kupata fursa ya kujenga barabara hiyo pamoja na kuahidi kufanya vizuri ili utakapotokea mradi mwengine kampuni yake iweze kushinda na kuendelea na miradi ya ujenzi hapa Zanzibar.

Alisisitiza kuwa azma yao ni kufanya kazi hapa Zanzibar na kuendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na kuendelea kuiunga mkono jamii ya watu wa Zanzibar huku akitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa mapokezi mazuri aliyoyapata yeye na ujumbe wake.

Alieleza kuwa Kampuni hiyo iliyoanzishwa mwaka 1948 ina ofisi zake mjini Hong Kong na Shanghai China ina matawi 500 ya Makampuni yake duniani na tayari imeshaekeza katika nchi 118 duniani ambapo kazi yake kubwa ni ujenzi wa nyumba, reli, ujenzi wa miundombinu kama vile barabara ambapo tayari kwa upande wa Bara la Afrika wana matawi katika nchi zote.

Aliongeza kuwa Kampuni hiyo tayari imejenga barabara ya kurukia na kutulia ndege pamoja na sehemu ya maegesho katika kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Angola, km 700 za reli kutoka Addis Ababa hadi Djibout pamoja na kilimota 1300 za reli katika nchi mbali mbali za Bara la Afrika.

Kwa maelezo ya kiongozi huyo, Kampuni hiyo pia ndiyo iliyojenga reli ya pamoja ya (TAZARA) yenye urefu wa kilomita 1,860 ambapo ukaguzi wa awali wa ujenzi wa njia ya reli hiyo ulifanywa mwaka 1968 na ujenzi ulianza mwaka 1970 hadi Julai mwaka 1976 kutoka bandari ya Dar-es-Salaam Tanzania hadi New Kapiri Mposhi Zambia.

Aidha, uongozi huo ulieleza kuwa mbali ya ujenzi wa reli hiyo, Kampuni hiyo imejenga majengo makubwa barabara, madaraja huko Tanzania Bara.

Mbali ya ujenzi wa barabara hiyo ya Bububu-Mahonda-Mkokotoni yenye kilomita 31 pia, Kampuni ya CCECC itajenga barabara ya Matemwe-Muyuni yenye km 7.58 na barabara ya Fuoni-Kombeni  km 8.59 pamoja na barabara ya Pale hadi Kiongele km 4.61.

Nae Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein alimpongeza kiongozi huyo pamoja na ujumbe wake kwa kufanya uwamuzi wa kuja Zanzibar na kuekeza kuwa hiyo ni ishara nzuri ya kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa China na Zanzibar zina historia tokea karne ya 11 na 12 ambapo wananchi wa nchi hiyo walifika Zanzibar na kuanza kuishi hadi hivi leo hatua ambayo iliimarika zaidi mara baada ya Mapinduzi Matukufu ya Januari 12, 1964 ambapo nchi hiyo ilianza kuiunga mkono Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuanza kuleta Madaktari kutoka Jimbo la Nanjing.

Dk. Shein aliongeza kuwa Zanzibar na China si marafiki tu bali ni ndugu kutokana na historia iliyopo ya pande mbili hizo kwani China imeweza kuisaidia Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya viwanda, kilimo, habari, afya, michezo na nyenginezo.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuvutiwa na azma ya Kampuni hiyo ya kutaka kujenga kiwanda cha kusarifu samaki kwani muelekeo na Sera ya Zanzibar katika uchumi wake ni kuimarisha uchumi wa Bahari (uchumi wa buluu).

Aliongeza kuwa Zanzibar ina rasilimali nyingi sana za bahari lakini bado haijawa na uwezo wa kuvua samaki kwa njia za kisasa kwani samaki wengi wako katika bahari kuu ambapo kutokana na kutokuwepo kwa vifaa na nyenzo zikiwemo boti za kisasa bado hawajaweza kuvuliwa.

Hivyo, alieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kuifanya Zanzibar iweze kutekeleza uchumi wa viwanda kama ilivyo jiwekea kwa upande wake na Tanzania Bara katika kutekeleza uchumi huo wa viwanda kwa kuweka mikakati maalum.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliuahidi uongozi huo kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari na inaikaribisha kuja kuekeza katika sekta hiyo ya uvuvi ambayo pia, itakuwa ndio njia pekee ya kuendeleza miradi mengine kwa Kampuni hiyo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.