Habari za Punde

Juhudi za Viongozi wa Dini na Vitendo Vya Udhalilishaji Wanawake na Watoto Zanzibar.


Na.Abdi Shamnah.
WASHIRIKI wa mkutano uliotathmini juhudi za viongozi wa Dini katika mapambano dhidi ya vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto, wamesema kuwepo kwa kumbi za starehe katika maeneo ya kambi za vyombo vya Ulinzi na Usalama, kunachochea ongezeko la vitendo vya udhalilishaji miongoni mwa jamii.

Wamesema kuwepo kwa kumbi huru zenye kutowa fursa ya watu wote kuingia na kustarehe, ikiwa pamoja na kunywa pombe na kucheza disco, kumeongeza chachu ya kufanyika vitendo vya udhalilishaji, ikiwemo ubakaji.

Changamoto hiyo imeibuliwa na Masheikh na viongozi wa dini ya Kikristo  katika mkutano wa robo mwaka (April hadi Juni, 2018) uliotathmin  juhudi ya viongozi wa dini katika mapambano dhidi ya vitendo vya udhalilishaji katika Wilaya zote za Unguja.
Mkutano huo umefanyika katika ukumbi wa Malaria Mwanakwerekwe, ukiwa chini ya uratibu wa Idara ya Wanawake.

Wamesema uwepo wa Baa katika maeneo ya Dunga, Mtoni, Entebe na kwengineko nchini, kumekuwa chachu inayochochea ongezeko la vitendo vya udhalilishaji, kwa msingi kuwa wanaozuru maeneo hayo hawazingatii maadili ya dini zao.

Wamesema kumbu kumbu znaonyesha kuwa kumewepo matukio mengi ya udhalilishaji na hata mauaji , ambapo baadhi ay watu wanaokwenda kwenye kumbi hizo huwasibu, hususan nyakati za usiku wa manane pale wanaporejea nyumbani.

Washiriki hao wameitaka Serikali kuingilia kati na kurejesha mfumo wa zamani, ambapo vikosi hivyo vya ulinzi na usalama, vilikuwa na utaratibu maalum wa raia kuingia kambini, tofauti na ilivyo sasa.

“Masuala ya udhalilishaji wa kijinsia, katika vyombo vya ulinzi ndiko yanakolelewa kupitia kumbi za madisko na baa, yako huru kila mmoja anaingia na kufanya atakalo, yafaa Serikali iingilie kati jambo hili’, alisema mmoja wa masheikh walioshiriki mkutano huo.

Katika hatua nyengine ,washiriki hao walieleza kujitokeza kwa matukio kadhaa ya udhalilishaji katika Wilaya zao, huku walimu wa madrasa wakitajwa katika matukio mbali mbali kuhusika na vitendo hivyo.

Aidha, washiriki hao wakaiomba Serikali  kupitia Wizara ya Afya kufanya uchunguzi wa waathirika wa udhalilishaji kuambatana na ukuaji wa tekonolojia.

Walisema katika hali ilivyo hivi sasa, ni jambo lisilokubalika kwa madaktari kuwachunguza waathirika wa udhalilishaji ama kwa kuwaangalia au kuwaingiza mikono katika sehemu zao za siri.

“Hivi sasa dunia imepiga hatua kubwa kiteknolojia, kiasi ambacho uchunguzi wa mtu alieingiliwa au kunajisiwa hauhitaji tena  daktari kuanza kumchungulia au kumtia mikono mdhuriwa, hiyo ni kuendelea kumdhalilisha, mtu ambae tayari ameshadhalilishwa’, alisema mmoja wa washiriki hao. 

Mapema, akifungua mkutano huo, Mkurugenzi wa Idara ya wanawake, Nasima Haji Chum alisema dini ni zana muhimu katika kubadili tabia za waumini kutoka vitendo viovu kuelekea vitendo vyema.

Aliwataka masheikh na viongozi wengine wa dini kutumia nafasi zao kuendelea kuwaongoza waumini wao kutekeleza vitendo vyema, ili kuwa na jamii iliostaarabika na yenye kuishi kwa amani.

Aidha, aliwataka washiriki hao kutumia mkutano huo kubadilishana uzoefu , sambamba na kila mmoja wao kutambuwa jukumu lao na kuhakikisha yote wanayoazimia yanafanyiwa kazi, ili kufikia malengo  yaliowekwa.

“Ni vyema mkaendelea kuvitumia vyombo vya habari kikamilifu ili kuitahadharisha jamii juu ya athari za kuwepo unyanyasaji katika jamii”, alisema.

Pamoja na mambo mengine, viongozi hao wa dini walikuwa na jukumu la kutoa taaluma kwa wananchi juu ya kukabiliana na vitendo vya udhalilishaji wa kijinsia katika maeneo yao, ambapo watu 15,504 walifikiwa kati yao wanawake 8,491 na wanaume 7,013 kutoka  katika Wilaya zote za Unguja.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.