Habari za Punde

Taarifa Kwa Umma Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Limefanikiwa Kuudhibiti na Kuuzima Moto Kariakoo.

WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI JESHI LA ZIMAMOTO NA UOKOAJI

 Jeshi la Zimamoto na Uokoaji nchini, limefanikiwa kuuzima na kuudhibiti moto mkubwa uliotokea jana asubuhi, kwenye jengo la biashara la ghorofa mbili linalomilikiwa na Ndugu Jonasi Nyagawa katika eneo la Kariakoo kwenye Makutano ya Mtaa wa Agrey na Livingstone jijini Dar es Salaam.

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limefanikiwa kuudhibiti na kuuzima moto huo kwa asilimia 100, hivyo kuzuia madhara na hasara kubwa ambayo ingeweza kutokea kwa wafanyabiashara wanaolizungula eneo hilo, pamoja na eneo la chini la jengo ambalo lina maduka ya wafanyabiashara.

Moto huo ulioanza majira ya saa 4:05 asubuhi, ulianzia kwenye ghorofa ya kwanza ya jengo hilo na kusambaa hadi ghorofa ya pili. Jeshi la Zimamoto na Uokoaji baada ya kupata taarifa lilifika eneo la tukio na kuudhibiti na kuuzima moto huo, ili usiweze kusambaa sehemu nyingine.

Hadi sasa chanzo cha moto huo bado hakijajulikana na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linaendelea na Uchunguzi ili kubaini chanzo cha moto huo. Moto ni tukio la hatari sana, hivyo watu wanatakiwa kukaa mbali wanapoona tukio la moto, kwani kusogea karibu na moto unapotokea kunaweza kuwasababishia madhara makubwa kutokana na moshi, kuangukiwa na kuta pamoja na kutokea kwa milipuko inayotokana na bidhaa mbalimbali zinazoweza kusababisha milipuko.

Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linatoa wito kwa wamiliki na wafanyabiashara wote nchini, kuzingatia kanuni za kinga na tahadhari ya majanga ya moto kwenye maeneo yao, ili kuzuia majanga ya moto kutokea pamoja na kutoa taarifa mapema ya matukio ya moto au maokozi, kwa kupiga simu ya dharura namba 114 ambayo ni bure kwa mitandao yote nchini.

Imetolewa na: Joseph K. Mwasabeja Msemaji wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.