Habari za Punde

Balozi wa Kuwait Nchini Tanzania Mhe. Jasem Ibrahim Al Najem, Azungumza na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein Ikulu Zanzibar.


RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza Serikali ya Kuwait kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo, Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi wa  Kuwait katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Jasem Ibrahim Al-Najem aliyefika Ikulu kwa ajili ya kuaga baada ya kumaliza muda wake wa utumishi nchini Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi Jasem Ibrahim Al-Najem kuwa Zanzibar inathamini sana hatua za Kuwait za kuendelea kuiunga mkono katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo.

Kutokana na juhudi hizo, Rais Dk. Shein alimuhakikishia Balozi huyo kuwa Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu kati ya pande mbili hizo huku akieleza kuwa Kuwait imekuwa mshirika mzuri wa Tanzania.

Alieleza kuwa hatua hizo zimepelekea kuimarisha na kukuza diplomasia kwa pande mbili hizo ambayo ina historia kubwa ambayo imetokana na wananchi wa Kuwait na ukanda mzima wa Gulf waliweza kufika Zanzibar.

Rais Dk. Shein aliongeza kuwa Kuwait imeweza kuimarisha na kukuza uhusiano na Zanzibar kwa kusaidia miradi mbali mbali ya maendeleo ikiwemo ya kilimo, afya, miundombinu ya barabara ikiwemo Barabara ya Chake Chake Wete, maji na mengineyo.

Dk. Shein pia alitumia fursa hiyo kuipongeza Serikali ya Kuwait kwa kuiunga mkono Zanzibar kwa kusaidia vifaa mbali mbali kwa ajili ya sekta ya kilimo na sekta ya afya ambavyo vilikabidhiwa leo kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Aidha, Rais Dk. Shein  aliipongeza Serikali ya Kuwait kwa kuisaidia Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo ikiwemo miradi ya afya kupitia Jumuiya yake ya ‘Kuwait Red Crescent Society’ huku akitoa shukurani na pongezi kwa nchi hiyo kwa azma yake ya kusaidia ukarabati wa hospitali Kuu ya MnaziMmoja na Mwembeladu.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alimpongeza Balozi huyo wa Kuwait na Serikali yake kwa azma yao ya Shirika la Ndege la nchi hiyo ‘Kuwait Airways’ kuanza safari zake hapa nchini na kusema kuwa hatua hiyo itaimarisha uhusiano na ushirikiano sambamba na kuimarisha sekta ya utalii.

Dk. Shein alimpongeza Balozi huyo kwa juhudi zake kubwa alizozichukua katika  kuhakikisha uhusiano na ushirikiano kati ya nchi yake na Tanzania ikiwemo Zanzibar unaimarika, jambo ambalo amefanikiwa kwa kiasi kikubwa.

Nae Balozi wa Kuwait katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jasem Ibrahim Al-Najem  alimpongeza Rais Dk. Shein kwa mashirikiano makubwa aliyoyapata kutoka kwa viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wananchi wake.

Balozi Jasem Al-Najim alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Kuwait itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha na kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo kwa azma ya kuimarisha uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya pande mbili hizo.

Katika maelezo yake Balozi Jasem Al-Najem alimueleza Dk. Shein, kuwa Shirika la Ndege la nchi hiyo ‘Kuwait Airways’ linatarajia kuanza safari zake hivi karibu hapa nchini hatua ambayo itazidi kuimarisha sekta ya utalii.

Aliongeza kuwa idadi ya watalii wanaokuja kutoka nchini Kuwait imeongeza kwa kiasi kikubwa hivyo kuanza kwa safari kwa ndege za Shirika hilo moja kwa moja kati ya Kuwait na Tanzania ikiwemo Zanzibar kutasaidia kuongeza ujio wa watalii kutoka nchi hiyo ambao kwa hivi sasa wamekuwa wakitumia mashirika mengine ya ndege.

Aidha, Balozi Jasem Al-Najim alimueleza Rais Dk. Shein kuwa vifaa mbali mbali vilivyotolewa na Serikali yake ambavyo vimekabidhiwa leo vikiwemo vifaa kwa ajili ya sekta ya kilimo yakiwemo matrekta na vifaa kwa ajili ya sekta ya afya vikiwemo vifaa kwa ajili ya Benki ya Damu ambayo ni ishara tosha ya kukuza uhusiano wa kihistoria uliopo kati ya pande mbili hizo.

Balozi huyo alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Serikali ya Kuwait inathamini uhusiano uliopo na kuahidi kuuimarisha huku akitumia futrsa hiyo kueleza kuwa Balozi anayekuja ataendeleza yale yote yaliyoanzushwa pamoja na mengine mapya kutoka nchini humo.

Nae Makamo Mwenyekiti wa ‘Kuwait Red Crescent Society’  Anwar Abdullah Al-Hasawi ambaye alifuatana na Balozi huyo, alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Jumuiya hiyo itaendelea kuiunga mkkono Zanzibar na kuendeleza miradi mbali mbali waliyoianza pamoja na kuanzisha mipya ambapo miongoni mwa miradi inayoiendelea hivi sasa ni mradi wa ‘Mama na Mtoto’.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.