Habari za Punde

Fei Toto asajili Singida United na Yanga kwa siku moja

Na Mwandishi Wetu, DAR ES SALAAM



KIUNGO Feisal Salum ‘Fei Toto’ ambaye mchana wa jana ametambulishwa na Singida United – jioni hii ametangazwa Yanga kwamba amejiunga na kwa mkataba wa miaka mitatu.



Fei alikuwepo makao makuu ya klabu ya Yanga akiwa na jezi ya klabu huyo na kutambulishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili wa klabu hiyo, Hussein Nyika kama mchezaji mpya wa klabu hiyo pamoja na kiungo mwingine, Jaffar Mohammed kutoka Maji Maji ambaye amesaini mkataba wa miaka miwili.

Feisal hakutaka kuzungumza chochote kuhusu kuonekana anatambulishwa na Singida United, lakini Meneja wa JKU, Mohammed Kombo aliyekuwapo mkutanoni pia amesema kwamba Yanga imekamilisha taratibu za kumchukua mchezaji huyo.



Mapema leo, Singida United imemtambulisha Fei Toto kwa kutoa picha akisaini mkataba na kukabidhiwa jezi ya timu hiyo. 


Na katika taarifa yake, Mkurugenzi wa Singida United, Sanga Festo amesema kwamba mchezaji huyo wa timu ya taifa ya Zanzibar amesaini mkataba wa miaka mitatu.

Sanga alisema kwamba Fei alikuwa amebakiza miaka miwili katika mkataba wake wa JKU, lakini walizungumza na klabu yake na kufikia makubaliano ya kuununua mkataba huo. 

Bado haijulikani nini kimejificha nyuma ya usajili wa Fei Toto – baada ya kuonekana anasaini Singida United asubuhi na jioni hii anaibukia Yanga.


Lakini kwa mujibu wa kanuni za usajili, iwapo itagundulika Fei amesaini mikataba na timu zote, atachukuliwa hatua kali za kinidhamu ikiwa ni pamoja na kufungiwa kuanzia mwaka mmoja.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.