Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein Anaondoka Kuelekea Nchini Indonesia Kwa Ziara ya Wiki Moja.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kushoto) akiagana na Makamu wa Pili wa Rais Mhe.Balozi Seif Ali Iddi (kulia)  katika Uwanja wa Ndge wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume alipokuwa akiondoka Nchini leo  kuelekea Indonesia katika ziara ya Kikazi akifauatana na Mkewe Mama Mwanamwema Shein (hayupo pichani) pamoja na Watendaji wengine wa Serikali,[Picha na Ikulu.] 30/07/2018.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein anaondoka nchini leo kuelekea Indonesia kwa ziara ya wiki moja kufuatia muwaliko wa Makamo wa Rais wa Nchi hiyo Muhammad Jusuf Kalla.
Ziara hiyo ya Dk. Shein inatarajiwa kuanza Agusti 1 na kumaliza Agusti 5 mwaka huu katika nchi hiyo ambapo anatarajiwa kufanya mazungumzo na mwenyeji wake  Makamo wa Rais wa nchi hiyo Muhammad Jusuf Kalla pamoja na viongozi wengine mbali mbali wa ngazi za juu wa Serikali na sekta binafsi wa nchi hiyo.
Katika ziara hiyo Dk. Shein anatarajiwa kutembelea katika kisiwa cha Bali ambacho ni kisiwa maarufu kwa utalii duniani na kufanya mazungumzo ya pamoja na viongozi wakuu wa kisiwa hicho.
Rais Dk. Shein akiwa nchini Indonesia atapata fursa ya kukutana na Wafanyabiashara na Wenyeviwanda kupitia Jumuiya yao ya Wafanyabiashara na Wenyeviwanda wa nchi hiyo huko mjini Jakarta katika mkutano maalum uliotayarishwa kwa ajili ya Rais Dk. Shein na ujumbe wake na Jumuiya hiyo.
Pia, Rais Dk. Shein anatarajiwa kutembelea Kampuni ya Uvuvi pamoja na Hospitali ya Harapan Kita iliyopo mjini Jakarta.
Akiwa katika kisiwa cha Bali Rais Dk. Shein atapata fursa ya kutembelea Chuo Kikuu cha Udayana, Jimbaran kiliopo mjini Bali pamoja na kutembelea kituo Kikuu cha Utalii katika mji huo.
Rais Dk. Shein pia, atatembelea katika kiwanda cha mafuta ya nazi na kutembelea eneo la mashamba ya mpunga huko Tabanan pamoja na kutembelea maeneo ya utamaduni pamoja na kutembelea kiwanda cha kusarifu mwani.

Katika ziara hiyo, Dk. Shein amefuatana na viongozi mbali mbali akiwemo Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein, Waziri wa Biashara na Viwanda, Balozi Amina Salum Ali, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk. Susan Alphonce Kolimba, Mshauri wa Rais Masuala ya Ushirikiano wa Kimataifa, Uchumi na Fedha Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa.
Wengine ni Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mariam Saadalla, Balozi Mohamed Haji Hamza Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ofisi ya Zanzibar pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi Zanzibar (ZIPA) Salum Khamis Nassor na watendaji wengine wa Serikali. 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein anatarajiwa kurejea nchini Jumatatu ya tarehe 6 Agosti, 2018.
Katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume Dk. Shein aliagwa na viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali, viongozi wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama pamoja na  wananchi ambao waliongozwa na Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.