Habari za Punde

Tajiri aiachia Oxfam pesa nyingi baada ya kufariki kwenye ajali na familia yake

Richard Cousins (katikati) aliuawa pamoja na wanawe Edward (kushoto) na William (kulia)
Tajiri mmoja aliyemiliki kampuni ya kuoka mikate ameliachia pesa nyingi shirika la Oxfarm baada ya kufariki na familia yake kwenye ajali ya ndege.
Gazeti la the Sun liliripoti kuwa Richard Cousins aliacha pauni milioni 41 kwa shirika hilo, baada ya kuuawa pamoja na mchumba wake, binti yake na watoto wake wawili wa kiume wakati wa mkesha wa mwaka mpya.
Gazeti hilo lilisema kuwa wosia wake ulisema kuwa pesa hizo zitaenda kwa shirika hilo la misaada kwa sababu watoto wake walikufa pamoja naye.
Oxfam iliiambia BBC kuwa lilikuwa limeachiwa pesa na Bw Cousins lakini halikusema ni ngapi.
Msemaji wa shirika hilo alisema wanashukuru sana kwa msaada huo.
Katika ripoti yake ya kila mwaka ya mwaka 2016-17, shirika hilo lilipata pauni milioni 19.8 kama zawadi zilizoachwa kama wosia.
Bw Cousins, 58, ambaye alikuwa mkurugenzi mkuu wa kampuni ya Compass Group, alikuwa pamoja na mchumba wake Emma Bowden, 48, binti yao wa miaka 11 Heather na watoto wake wa kiume Edward, 23, na William, 25, mjini Sydney mkesha wa mwaka mpya 2017.
Kulingana gazeti la the Sun, mwaka moja kabla ya kutokea ajali, Bw Cousins alikuwa ameongeza kipengee kwenye wosia wake kuwa ikiwa yeye na familia yake wangekufa kwa wakati mmoja, pesa zake zingenda kwa shirika hilo.
Baada ya ajali hiyo, ilimaanisha kuwa pauni milioni 41 zingeenda kwa Oxfam, hata kama ndugu zake wawili watapokea pauni milioni moja kila mmoja.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.